March 11, 2013




Na Saleh Ally
SIMBA wameonyesha kuchoshwa na longolongo za Waarabu wa Etoile du Sahel ya Tunisia na kutengeneza timu ya watu wawili ambayo itafunga safari kwenda Tunisia ikiongozwa na Rahma Al Kharusi maarufu kama Malkia wa Nyuki.

Okwi aliuzwa na SImba kwa Etoile du Sahel kwa kitita cha dola 300,000 (zaidi ya Sh 480), lakini hadi leo, Msimbazi wamekuwa wakiendelea kuangalia hesabu hizo kwenye makaratasi bila ya hata senti moja mkononi.


Timu hiyo huenda ikawa na watu wawili au watatu ambao wataondoka kwenda Tunisia kuzungumza na uongozi wa Etoile du Sahel kuhusiana na malipo ya fedha za mauzo ya mshambuliaji wao, Emmanuel Okwi.

Habari za uhakika kutoka ndani ya Simba, zinaeleza timu hiyo itaongozwa na mlezi wa Simba, Rahma kwenda kukutana na uongozi wa timu hiyo.

“Kweli kuna timu inapanga kuondoka kwenda Tunisia, inawezekana kabisa kukawa na watu wawili au watatu ila mama (Malkia wa nyuki) ndiyo ataongoza msafara huo maana tumemuomba afanye hivyo kama atakuwa na nafasi,” kilieleza chanzo.

“Lengo ni kujaribu kuwahisha suala hilo, maana tunajua Fifa ina mambo mengi. Uamuzi ulifikiwa kwenye kile kikao cha wiki iliyopita kilichofanyika pale Serena.”

Awali Watunisia hao waliwaahidi Simba nusu ya fedha hizo zingetua Dar es Salaam Januari 29 kabla ya kuwamalizia Februari 28, lakini mambo hayakwenda hivyo.

Uongozi wa Simba ukaamua kuandika barua ukitaka ulipwe zote ilipofika Februari nao wakakubali, lakini baada ya hapo wameendelea kuwa kimya hadi Simba walipoamua kuandika barua ya malalamiko kwa Shirikisho la Soka la Kimataifa (Fifa).

Barua hiyo imetaka Etoile du Sahel washinikizwe kuilipa Simba na kama itashindikana basi Okwi arejeshwe nchini na kuendelea kuichezea timu hiyo ambayo mwendo wake ni wa kinyonga.

Hata hivyo, Malkia wa nyuki ameona suala hilo huenda likachukua muda mrefu kwa kuwa Fifa ina mambo mengi ya kushughulikia katika soka na fedha hizo wanaweza wakaona ni kiwango kidogo tu kwao.

Hivyo bora kuwafuata moja kwa moja na kujadiliana nao kuhusiana na malipo hayo mara moja au kuvunja mkataba wa Okwi ambaye bado alikuwa anahitajika Simba.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic