December 5, 2014


 
HANS POPPE.
Na Saleh Ally
ZOEZI la usajili katika Klabu ya Simba linaongozwa na Zacharia Hans Poppe, mwanajeshi mstaafu ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili Msimbazi.


Kamati ya Hans Poppe ambayo makamu wake ni Kassim Dewji ndiyo ilifanya usajili ambao uliaminika ni bora, lakini katika mechi saba za Ligi Kuu Bara, ilitoka sare sita na kushinda moja!

Hali hiyo iliashiria kutofanyika vizuri kwa usajili na sasa kamati hiyo imekuwa ikifanya usajili kuhakikisha inarekebisha mambo. Katika mahojiano maalum na Championi Ijumaa, Hans Poppe anafunguka wazi kwa kila swali.

Mgambia:
Kiungo mshambuliaji Omar Mboob kutoka Gambia ametua nchini kwa ajili ya majaribio, ikitokea amefuzu yupi kati ya Amissi Tambwe na Pierre Kwizera ataachwa?
Kwanza nianze kuelezea kuhusiana na huyo Mgambia, nilikutana na wakala wake yuko huko Hispani. Akasisitiza aje afanye majaribio akiamini ana uwezo mkubwa pia ni aina ya mchezaji anayeweza kucheza barani Ulaya.

Tumekubali, tumempa nafasi ya kumuona ila mawili yatatokea. Kutegemeana na uzuri wake, ukiwa wa kawaida, basi atasubiri msimu ujao kwenye usajili mkubwa.

Akiwa mzuri na tunaona atatusaidia, kweli tutahitaji nafasi moja. Mwalimu (Patrick Phiri) ndiye ataamua kati ya Tambwe na Kwizera, kwamba nani aende. Maana kweli Simba tunahitaji offensive midfield (kiungo mshambulizi) aliyeiva.

 
HANS POPPE AKIWA NA TALIB HILAL.
Kiongera:
Kiongera mmemuacha, nafasi yake inachukuliwa na Danny Sserunkuma. Vipi mmevunja mkataba kwa kutumia mfumo upi?
Kwanza nifafanue, hatujavunja mkataba na Kiongera. Bado yuko chini yetu, sisi ndiye tunaogharimia matibabu yake, pia tutaendelea kumlipa mshahara hadi hapo atakaporudi maana tunamhitaji, tatizo limekuwa ni majeraha tu.
Mapumziko yake ni marefu baada ya kutibiwa, zaidi ya miezi mitatu. Hatuwezi kuendelea kuifunga nafasi wakati tunaihitaji, hivyo tumekubaliana vizuri na yeye ameleelewa.

Chanongo:
Bado haijajulikana, taarifa zinaeleza Haruna Chanongo anatakiwa na Mtibwa Sugar, lakini wako wanasema Simba inamshusha timu B, wewe kama bosi wa usajili, ukweli hasa ni upi?
Wakati mwingine naona kama Chanongo mpira wake kama ndiyo umefikia hapo. Nimewahi kuzungumza naye kama mzazi mara kadhaa, nilimueleza namna anavyoshindwa kufanya uamuzi kila anapoingia kwenye 18 ya adui.
Hauwezi kuwa mchezaji uko kwenye lango la adui, unarudisha mpira kwa namba tatu wenu. Hii imefanya hadi watu waanze kuamini anaihujumu timu, inaweza isiwe hivyo.
Mchezaji gani asiyebadilika, angalia Simba tulivyompa nafasi tukionyesha tunamuamini. Nimesikia hata alipoitwa kuzungumza na viongozi alionyesha utovu wa nidhamu wa hali ya juu.

Sikuwepo, nilikuwa safari. Nimesikia anarudishwa kikosi B. Lengo akajifunze zaidi, ikishindikana basi. Nimesikia wakala wake anataka aachiwe aende, sasa sijajua hili limeishia wapi hadi sasa.

Unajua kuna timu zinamtaka kwa mkopo, sheria ya mkopo sisi ndiyo tumlipe. Sasa kama tunamlipa sisi, kuliko kuwa kwenye timu nyingine, basi bora acheze timu ya vijana ambako anaweza kubadilika.


Kessy:
Kuna taarifa mnataka kumsajili beki wa kulia wa Mtibwa Sugar?
Hassan Ramadhani ‘Kessy’, kweli huyu ni beki wa kulia wa Mtibwa Sugar. Tayari tumeanza kuzungumza na uongozi wa klabu hiyo.

Nafikiri hatuko pabaya na tayari walikuwa wametoa ofa na tunaifanyia kazi, ninaamini baada ya siku mbili hizi tutakuwa naye kikosini.

 
CASILLAS
Casillas:
Kuna taarifa za kwamba mnataka kumuacha kipa Cassilas?
Kwa kweli suala hilo bado hakuna taarifa za uhakika kama anaachwa. Kikubwa ni kuangalia matibabu yake na kamati ya utendaji ndiyo inaweza kuamua siku ya mwisho, hivyo siwezi kutoa jibu la moja kwa moja.

Mechi 7:
Mlikosea nini hasa katika usajili wa mwanzo wa msimu hadi timu ikapata sare sita katika mechi saba?
Hatujawahi kukaa tukafanya analysis (uchambuzi), lakini kama ni maoni yangu binafsi, kikosi hakikuwa kibaya sana ingawa kweli tumefanya mabadiliko. Kambi ya Zanzibar timu ilikuwa vizuri, tulipoanza ligi, mechi dhidi ya Coastal tulicheza nzuri sana, tukafunga mabao mawili.

Mwamuzi wa siku hiyo alianza kutuvuruga, bao la kwanza halikuwa sahihi. Bao la pili la mkwaju wa adhabu, niliona si sahihi Ivo (Mapunda) kufungwa bao rahisi hivyo, tukaondoka mchezoni. Baada ya hapo, hatukucheza vizuri na inaonekana tatizo ni la safu ya ushambuliaji na si mabeki.

Tatizo:
Unaposema tatizo ni washambuliaji, una maanisha Simba ina safu nzuri ya ulinzi na imewaridhisha?
Nianzie na Isihaka Hassan, naamini atakuwa ni mmoja wa mabeki bora kabisa Tanzania. Amefanya kazi yake vizuri, lakini bado kiungo hakikuwa bora, safu ya ushambuliaji ndiyo ilikuwa tatizo zaidi.

Kama kiungo kinayumba, mabeki hawawezi kufanya vizuri na utaona katika mechi saba, mechi moja tu ya Coastal ndiyo safu ya ulinzi iliruhusu mabao mawili. Nyingine safu haikuruhusu hata bao moja, au tulifungwa moja.

Sasa, safu ya ushambuliaji siku tumefungwa moja, kwa nini haikufunga mbili? Siku tulifungwa mbili mbona haikufunga tatu? Ndiyo maana nasema ushambuliaji ni tatizo kubwa.

Kingine sub (ubadilishaji wachezaji) haukuwa mzuri, huenda kocha alikuwa ni mwenye hofu kila wakati.
 
PHIRI AKIWA MAZOEZINI NA VIJANA WAKE.
Sub za Phiri:
Kivipi sub za Kocha Phiri hazikuwa nzuri, unafikiri zilichangia kuwaangusha?
Kabisa, naona kama alikuwa muoga wakati mwingine, hataki kuchukua risk (kujaribu). Sub ile ya (Amri) Kiemba dhidi ya Prisons ndiyo ilitumaliza. Pia alikuwa akiangalia mazoea, hata mchezaji anazembea, ila kwa kuwa amemzoea, basi lazima acheze. Vipi wengine ambao lazima wapewe nafasi ili uwezo wao uonekane. Kwani (Peter) Manyika tulimuona vipi kama isingekuwa kumpa nafasi na majukumu mazito?

Mnawapangia timu makocha:
Kuna taarifa mmekuwa mkiwapangia timu makocha na wewe ni mmoja wapo?
Hizo ni hadithi tu, lakini wakati mwingine unaweza kumshauri kocha na baadaye yeye na timu yake ya benchi la ufundi wakaamua.
Nitakutolea mfano, ile mechi ya 3-3 na Yanga, hadi mapumziko tulikuwa tumefungwa tatu. Tumeingia vyumbani, (Abdallah) Kibadeni akaanza kuwaambia wachezaji kwamba tumeishafungwa bao tatu, basi zinatosha tusiruhusu nyingine, hivyo tu basi!

Mimi uvumilivu ukanishinda, nikamueleza kocha kiungo cha Abdulhalim (Humud) na Chanongo, kimekufa, wawape nafasi vijana. Wakaingizwa Said Ndemla na Gallas na wakafanya kazi tukasawazisha hadi mwamuzi akamaliza mpira kabla ya dakika hazijaisha.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic