December 12, 2014



Na Saleh Ally
MTANZANIA Idris Sultan amefanikiwa kuipa nchi yetu sifa, ameshinda taji la Big Brother HotShots 2014 na kutwaa kitita cha zaidi ya Sh milioni 510.


Hongera kwake, si fedha kidogo kwa mashindano ya miezi miwili na robo tu, lakini amezidi kuwahamasisha watu kuwa Tanzania ina vijana wenye vipaji.

Pamoja na heshima kubwa kwa taifa, suala au gumzo ni fedha zake, atazifanyia nini? Zitamsaidia vipi au atazitumia vibaya kupitia mgawo wa kijinga ili afulie?

Ukweli huu ndiyo wakati wa lawama kwa Idris, huenda kila mmoja anataka apewe shukurani kwa kuwa aliwahi kumsaidia hiki au kile au alishiriki kwenye ishu ile au hii ya kumsaidia ashinde.

Huu ndiyo wakati ambao Idris hapaswi kuwa muoga hata kidogo, asihofie lawama kutoka kwa yeyote, badala yake aangalie anafanya nini.

Hili namnong’oneza, (wewe msomaji unaweza kuruka hapa)-bora ukubali lawama, maana usipoiheshimu Sh 100, ikapungua kwenye Sh milioni 1, basi haiwezi kuitwa milioni moja, itakuwa Sh 999,900. Maana yake hata hiyo Sh milioni 520 na ushee, inaweza kuyayuka kama ukijidai mtu wa bata sana au msamalia mwema kama nanihii, umekwisha.

Hakika sijui Richard Bezuidenhout aliyeshinda dola 100,000 (Sh milioni 170) alizitumiaje. Sijui kama aliingia kwenye mgawo wa kijinga!

Dua mbaya na nzuri tayari ziko hewani, si kweli wote wamefurahia ushinde. Wako waliofurahia na waliokasirika bila ya wewe kujua. Muhimu chunga makundi haya matatu, maana yataugeuza mgawo wa fedha zako kuwa wa kijinga kabisa!

Ndugu:
Kundi la ndugu ni kubwa, lakini unaweza kuligawanya katika makundi mawili. Waswahili wanasema ndugu lawama, kila ndugu hataki kukosolewa, kuhojiwa wala kunyimwa ili mradi ajue kipo.

Kundi la kwanza ni lile la wale walioshughulika kumsaidia Idris, mfano kampeni kuhakikisha anashinda au kumuunga mkono tu.

Kundi la pili ni lile ambalo lilikuwa limekaa kando, halikujua kuhusu Big Brother au kama lilijua, lilidharau Idris angeweza kushinda.

Makundi yote mawili yana haki sawa hasa ukija katika neno ndugu. Hapo ndiyo kuna shida, Idris ana zaidi ya Sh milioni 510 mkononi. Sasa kwa nini asiwape hata Sh milioni 5, kila ndugu!

Ninaamini kuna ndugu angelalamika hata kama angepewa Sh milioni 10, maana anaona Sh milioni 500 na zaidi ni nyingi sana!

Huu ndiyo wakati wa lawama kwa Idris, wakati wa kipimo cha uwezo wa kuamua, kutafakari na baadaye kusonga au aamue, asitafakari na arudi nyuma.

Hii inaonyesha lazima akubali kugombana na watu, asemwe, alaumiwe, lakini kikubwa aangalie kipi ni sahihi.

Sh milioni 500 ni ndogo sana na huenda zikawa ndogo zaidi kuliko Sh milioni moja kama zitatumika bila mahesabu sahihi, mpangilio wa uhakika na plani za kitaalamu.

Wapambe:
Hawa wapo tu, tayari sasa wako sehemu wanapiga mazoezi ya ‘nyimbo’ za kumuimbia Idris.

Kwa lawama, hawatofautiani sana na ndugu ingawa wenyewe hawana nguvu ya ule ‘undugu wa damu’, lakini wanaamini wana hakika.

Unakumbuka Idris aliwahi kupewa nauli ya kwenda sehemu fulani na nanihii, halafu alipelekwa klabu na nanihii. Sasa akina nanihii wote nao wanataka angalau wale bata maana mshikaji wao ana mamilioni. Watamkubusha Idris maisha ni mafupi. Shauri yake!

Ukweli, akidhubutu tu akaingia mkenge na kuwasikiliza, hapo ndiyo atajua wapambe nuksi, siku akikwama, wao ndiyo watakuwa wa kwanza kumcheka wakimtangaza kuwa mjinga kuzidi watu wote duniani, hapa pia, lazima akubali lawama. Potelea mbali.

Warembo:
Hawa ndiyo professional zaidi, wanajua wanataka nini kwa watu wenye chochote kitu mkononi. Idris alikuwa mpiga picha tu, nani alimjua, kwa nini wamjali?

Warembo wa mjini wengi wanajali kwenye kitu, wako walioruka juu kufurahia ushindi wa Idris alipotangazwa kupitia runinga, si kwamba wanaipenda sana Tanzania, wanafurahia ‘duka’ jipya limefunguliwa nchini, wanajua watafanyaje.

Usisahau Idris ni kijana, hata kama atawaza biashara ili kujiendeleza, usinidanganye ‘hatapoza’ moyo.

Anaupozaje? Mimi na wewe hatujui, lakini vema akawa makini asije akaubwaga kabisa na mwisho akafulia.

Warembo wana kila njia, kamwe hawawezi kushindwa kumfikia. Si kama zile enzi zetu za barua, halafu unachora kopa kibao, kati zina mshale uliokatiza.

Siku hizi kuna Instagram, Whatsapp, Viber na takataka kibao. Watamfikia tu, lakini usisahau kuna wanaume wanaishi jijii Dar kwa ukuwadi tu, wapo, unabisha nini?

Wao pia watahitaji kamisheni yao, hapo ndiyo wataanza kazi ya kuwatafutia wasichana njia zote za kumfikia kijana huyo wa Big Brother. Inawezekana kwa kufanya urafiki na ndugu zake, rafiki zake lakini ili mradi wamfikie ili waweze kugawana kijinga fedha zake.

Wanapenda kugawana kijinga na mwisho watamcheka kwa ujinga. Yeye ndiye anaweza kuamua azigawe kijinga au akatae kuwa mjinga, maisha yasonge mbele.

SOURCE: CHAMPIONI 

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic