December 6, 2014

EMERSON
Kocha Mkuu wa Yanga, Mbrazili, Marcio Maximo, amemshtukia kiungo wake mpya mkabaji, Emerson De Oliviera kuwa ni mzito na kutakiwa kuufanyia kazi mwili wake ili ahakikishe anapata wepesi.

Awali, ‘ugonjwa’ huo wa uzito aliwahi kuwa nao mshambuliaji wa timu hiyo Mbrazili, Geilson Santos Santana ‘Jaja’ licha ya kufanyishwa mazoezi magumu ili apunguze uzito huo.

Emerson yeye alitua kuichezea timu hiyo wiki moja iliyopita akitokea nyumbani kwao Brazil, amesaini mkataba wa mwaka mmoja wa kuichezea Yanga.

Katika kuhakikisha kiungo huyo anapunguza uzito, Maximo amemuandalia programu maalumu ya mazoezi uwanjani pamoja na gym.

Katika mazoezi ya jana Ijumaa asubuhi yaliyofanyika kwenye Uwanja wa Loyola, Mabibo jijini Dar es Salaam, Maximo alimzuia kugusa mpira kiungo huyo huku akimtaka kufanya mazoezi ya mbio fupi na ndefu uwanjani.

Programu hiyo, ilisimamiwa na kocha msaidizi, Leonard Neiva raia wa Brazil ambaye alianza peke yake kwa kukimbia kuuzunguka uwanja kabla ya kuchanganywa na akina Said Bahanuzi, Hussein Javu na Khamis Thabiti ambao walikimbizwa kwa raundi kumi.

Wakati wakiendelea kukimbia, Neiva alionekana kuwaongezea programu nyingine ya kuruka koni ndefu sita na fupi tano zilizopangwa uwanjani hapo.

Neiva, pia alimtaka Emerson na wenzake kukaa chini na kunyanyuka kwa haraka wakifuata mlio wa filimbi aliyokuwa akiipuliza na baada ya zoezi hilo wachezaji walionekana kuchoka.


Wakati Emerson na wenzake wakiendelea na programu hiyo ya mazoezi magumu, wengine walikuwa wakicheza mpira wakisimamiwa na Maximo ambaye alionekana akiwanoa kwa mbinu mbalimbali.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic