January 5, 2015



Na Saleh Ally
STEVE Mwamwala aliyezaliwa Kyela mkoani Mbeya alipata umaarufu mkubwa ndani na nje ya Tanzania baada ya Yanga kuchapwa mabao 5-0, mwaka 2012.


Shabiki huyo wa Yanga wakati huo, alishindwa kujizuia, akamwaga chozi kwa uchungu na kusababisha wengi kumuonea huruma na umaarufu wake, ukazaliwa.

Hakuwa tena Steve Mwamwala, badala yake akaanza kujulikana kama Steve Yanga na umaarufu wake ukapaa haraka mno. Sasa anajulikana kama Steve Azam.


Steve Azam ni jina jipya baada ya kutangaza kuhamia Azam FC ambao sasa ndiyo mabingwa wa Ligi Kuu Bara.

Kijana huyo ameamua kuhamia Azam FC hali ambayo imewaudhi kwa kiasi kikubwa mashabiki wa Yanga, lakini kubwa zaidi, anasema amepoteza kazi na kuondolewa sehemu aliyokuwa akiishi.


Hili la kuondokewa kwenye nyumba uliyokuwa ukiishi lina ukweli?
Ndiyo, nimefukuzwa kwenye nyumba. Nilikuwa nikiishi Tabata Segerea siku zote lakini baadaye kigogo mmoja wa Yanga (anamtaja) alinipa kazi na nyumba nzuri. Nilikuwa nikifanya kwenye Supermarket moja huko Mbezi Beach.

Baada ya kusikia nimehamia Azam FC, mara moja akanifukuza kazi na kuniondoa kwenye nyumba. Nimerudi Tabata Segerea.

Vipi kuhusu urafiki wako na mashabiki wa Yanga? Umekuwa mbaya sana kaka, hawataki kuniona na wamekuwa wakisema vibaya kila wanaponiona. Najiona kama nimetengwa na siishi na wenzangu.

Kuna taarifa Azam FC, wanakulipa mshahara?
Nani kasema? Haya ni maneno ya kizushi kabisa. Kweli Azam FC wameniahidi fedha kwa ajili ya mtaji, lakini hilo lilikuja baada ya mimi mwenye kuhamia kwenye timu yao, hawakuniomba.

Zaidi ninachopata kwao ni pale timu inaposafiri, wananijumuisha, naungana nao kwenda kuwapa nguvu. Hakuna zaidi.

Nasikia umekuwa ukikumbana na vitisho kutoka kwa mashabiki wa Yanga?
Kweli kiasi fulani ninaishi kwa hofu. Wengi wao wananiita msaliti, wapo waliokuja hadi nyumbani na kunitishia lakini sioni kama ni sahihi, maana mimi si adui, nimeamua kuhama kwa hiyari yangu.

Kweli shabiki anaweza kuhama, hivyo siku moja tutegemee kukusikia ukiitwa Steve Simba?
Haitatokea milele. Najua Simba wana watu wengi wenye ushirikiano, wananivitua kwa hilo na hiyo ni sifa yao nzuri lakini siwezi kuwa Simba, nimehamia Azam baada ya Yanga na haiwezi kuwa zaidi, siwezi kwenda Simba.

Nini hasa kilichokuondoa Yanga Steve, ni kweli njaa kama wanavyosema watu wengi?
Njaa kila mmoja anayo! Hata wewe una njaa Saleh ndiyo maana unaamka asubuhi kuwahi kazini.

Ila tatizo kubwa lililonifanya niondoke kulikuwa na kipindi kinaitwa Kwetu House kilichoendeshwa na Azam TV, nikaenda kushiriki, hapo ndiyo ugomvi ulianza.

Nilikwenda kama shabiki maarufu wa Yanga. Walikuwepo wa Simba na timu nyingine. Yanga hawakulifurahia wakawa wananiita msaliti, nikijaribu kufafanya hawakuelewa na walisisitiza sisi tuna ugomvi na Azam.

Nikawaeleza mchezo uko Azam TV si Azam FC, lakini wapi. Siku alipokuja Kocha (Marcio) Maximo nikaenda kumpokea uwanja wa ndege, hapo ndiyo tatizo lilianza.

Mashabiki kama 50 wa Yanga walinivamia, wakataka kunipiga wakidai mimi ni msaliti. Nikaokolewa na polisi wa uwanja wa ndege.

Hiyo tabia ikaendelea, mwisho nikaona hakuna furaha ya ushabiki. Nikaona hata wachezaji huwa wanahama, nikahamia Azam FC.

Ungeweza kuwa mvumilivu, mwisho wangekuelewa?
Niliishakuwa mvumilivu sana, kuna wakati tena mashabiki wa Yanga walitaka kunipiga kwa kuwa niliwazuia wasivunje kamera za Azam TV, nikawaambia hiyo si Azam FC, likawa kosa.

Mara mbili kuna viongozi wa Yanga (anawataja) waliwahi kunitukana matusi makubwa. Sikuelewa kisa, wao ndiyo waliniambia niwatafute, halafu wakanitukana.

Sasa unaishi maisha ya namna gani, unataka uishi vipi zaidi ya hapo?
Maisha yangu ni ya kawaida, bado sijapata kazi, naendelea kutafuta. Wale rafiki zangu niliokuwa nao Yanga, sasa wananipita, hata lifti tu ya gari sipati!

Inaniuma sana maana Azam FC ni timu kama ilivyo Yanga, sielewi chanzo cha uadui na michezo haisemi hivyo.

Kuhusu maisha, nataka niishi maisha mazuri, nioe msichana mzuri kama Wema Sepetu ambaye ninampenda sana.

Angalia Idris, leo kama zaidi ya Sh milioni 500. Nilisoma naye huyu Idris, hivyo na mimi natamani maisha hayo.

Usisahau, ishu ya kujulikana kama shabiki wa Yanga nilielia, imenipa umaarufu mkubwa ambao wakati mwingine unanitenda!



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic