January 26, 2015


MAPEMA mwezi huu waamuzi mbalimbali katika mechi za Ligi Kuu Daraja la Kwanza walikutana na dhoruba kali ya kupigwa kama wezi.

Kupitia gazeti hili tuliona mwamuzi aliyechezesha mechi ya Toto African dhidi ya Polisi Dodoma akikimbizwa kama kibaka huku akipigwa na mchezaji ambaye sura yake ilionekana dhahiri ni nani. Hii ilitokea kwenye Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza.

Siku chache badaye kwenye Uwanja wa CCM Kirumba tena, wachezaji wa Polisi Tabora nao waliwapiga waamuzi huku wakiwakimbiza kama vibaka pia.

Kwa kuwa hali hiyo ilionyesha mashabiki, walifikia uamuzi wa kuteremka jukwaani na kuanza kutaka kupambana na wachezaji wa Polisi Tabora lakini askari Polisi wakapoza vurugu hizo na mwisho wakamrudisha mwamuzi uwanjani chini ili amalize mpira.

Usisahau mara ya kwanza, yule mchezaji wa Polisi Dodoma alimkimbiza mwamuzi hadi jukwaani naye akakutana na kipigo kutoka kwa mashabiki.

Kila kitu kilikuwa wazi, tena nyongeza vurugu kama hizo zilitokea kwenye Uwanja wa Karume mjini Musoma na mwisho TFF ikatangaza kuufungia uwanja huo ambako wachezaji wa Mwadui FC, Kocha wao, Jamhuri Kihwelo Julio na Mwenyekiti wa Chama cha Soka Mkoa wa Shinyanga (Shirefa), Kangi Lugola nao walipogwa kama wezi.

Ajabu TFF imeanza kulishughulikia suala hilo huku wakionyesha wazi kwamba wale wachezaji waliowapiga waamuzi huku wakiwakimbiza si wote walioshitakiwa.

Wachezaji Dihe Makonga, Swalehe Idd Hussein, Ramadhan Mwinyimbegu na Shaibu Nayopa wa Oljoro JKT na Nassib Lugusha wa Polisi Dodoma wanalalmikiwa katika Kamati ya Nidhamu kwa kushambulia waamuzi na kufanya vurugu kwenye benchi la timu pinzani.

Lakini wengine waliofikishwa kwenye kamati ya nidhamu ni watunza vifaa wa Polisi Mara, Rhino na JKT Oljoro. Kocha wa Polisi Tabora, Kim Christopher analalamikiwa kumtolea mwamuzi lugha chafu.
Sasa swali langu linafuatia hapo, wako wapi wale wachezaji ambaow anaonekana wazi wakiwakimbiza waamuzi huku wakiwashambulia kwa ngumi na mateke.

Angalia mchezaji wa Polisi Dodoma, alimkimbiza mwamuzi ambaye alianza kumpiga uwanjani, akatoka naye hadi jukwaani ambako alipigwa na mashabiki. Hali kadhalika, wachezaji wa Polisi Tabora ambao walimpiga mwamuzi kama kibaka.

Picha zinaonyesha wakiwa wamempiga mateke na kuna picha inaonyesha mchezaji mmoja wa Polisi Tabora akiwa amempiga ngumi mwamuzi wa akiba!

Jamani, kama kweli waliofanya vile wameachiwa tu na TFF inaona ni sawa, basi hapa tutaanza kujenga hisia timu za majeshi zinaogopwa hadi na shirikisho hilo.

Jiulize, vipi mchezaji anayempiga mwamuzi kama kibaka, haladu anaonekana kabisa kwamba ni yeye na adhabu haitoki. Tunautengeneza vipi mpira wetu.

Inawezekana kabisa jambo hilo limechukuliwa kwa uzito wa chini kabisa, kitu ambacho kinadhibitisha hakuna anayewajali waamuzi.

Sitaki kuwatetea waamuzi kwamba ni watu safi kuliko wengine wote. Kuna matukio mengi sana yanathibitisha wanapokea rushwa ingawa wanatumia nguzo ya usiri kama sehemu ya kufunika kombe.

Lakini bado hatuwezi kuunga mkono wapigwe kwa wezi hali ambayo inaleta taswira tofauti inayolenga kuuporomosha mpira wa Tanzania na kuuonyesha kama ni mchezo wa wahuni fulani.

Wakati mwingine najiuliza au TFF inaona haya kwa kuwa picha zimetoka kwenye gazeti hivyo haiwezi kuchukua uamuzi wowote kwa kuwa itaonekana “imefanya kazi kupitia gazeti au blogu?”

Inapaswa kujifunza, gazeti katika kamati ya nidhamu linaweza kutumika kama ushahidi. Raha zaidi ni picha na si maandishi na huenda gazeti linaweza kuaminika zaidi hata kuliko ripoti ya kamisaa na hasa picha zikitumika.

Kuna kila sababu ya wachezaji wa Polisi Dodoma na Tabora waliowapiga kuadhibiwa. Pia wenzao wa Polisi Mara na uongozi wao. Mkiwaacha hao maana yake mnatoa ruhusa na wengine wafanye.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic