February 28, 2015


Na Saleh Ally
AWALI nilidhani ni mashabiki wa Arsenal wa nyumbani Tanzania pekee ambao wamekuwa wakimlalamikia Kocha Arsene Wenger kuwa ni tatizo hasa kila Arsenal inapopoteza mchezo.


Nikiwa katika mazungumzo ya kawaida na rafiki yangu anayeishi London, tena shabiki wa kutupwa wa Arsenal, naye alianza kuangusha lawama kwa Wenger kwamba ndiye anawakwamisha hasa baada ya kufungwa mabao 3-1 na Monaco.

Mtu mwingine ambaye ni  mchambuzi wa michezo nchini Msumbiji alikuwa akinisimulia maendeleo ya soka la Ureno ambako alifanya ziara hivi karibuni. Hakuacha kumponda Wenger pia, kuwa ni ‘kirusi’ ndani ya Arsenal!

Watu hawa wawili walinirudisha nyuma na kuanza kutafakari kwamba huenda mashabiki wa Arsenal ndiyo wanaoongoza kuliko wote kwa jazba. Au wao wanaongoza kwa kuwa na lawama, bila ya kufuatilia.

Watu wawili niliozungumza nao katika mazingira tofauti, wote ni wataalamu katika masuala ya michezo, kwa nini hawaelewi? Kama wao hawaelewi, vipi kwa shabiki wa kawaida?
Mechi 10:

Nikaamua kurejea kwenye takwimu za mechi 10 za Arsenal ikiwemo hiyo dhidi ya Monaco. Hesabu zikazidi kunishangaza zaidi kuhusiana na Wenger, kwamba wanamuonea, watamuua huyu mzee.

Kuanzia Januari 4, hadi Februari 25 mwaka huu walipocheza mechi na Monaco, Arsenal walikuwa wamecheza mechi kumi mfululizo.

Walicheza mechi hizo kumi za michuano ya Kombe la FA, Ligi Kuu England na Ligi ya Mabingwa ndani ya siku 53, tena wakiwa wamepoteza michezo miwili tu.

Mechi ya kwanza walipoteza Februari 4 wakiwa ugenini kwenye Uwanja wa White Lane, London baada ya kufungwa mabao 2-1 dhidi ya Tottenham Hotspur kabla ya kuchapwa  na Monaco kwa mabao 3-1 wakiwa kwao Emirates.

Ukiachana na hapo, Arsenal imecheza mechi sita za nyumbani na kushinda tano, huku ikipiga nne za ugenini na kushinda tatu.

Ukimya:

Wakati Arsenal ikiendelea kushinda mechi mfululizo, hakuna shabiki aliyekuwa akilalamika zaidi ya kusifia wachezaji walivyokuwa wakifanya vizuri.

Mfano, wengi walisifia kurejea kwa Mesut Ozil, kwamba sasa atakuwa tishio na alivyokuwa anakwenda ilionekana wazi hakuna wa kumzuia.

Mwingine ni Santi Cazorla, yuko vizuri na hilo ni kweli. Wengi walimwaga sifa kutokana na uwezo ambao amekuwa akiuonyesha katika mechi za hivi karibuni.

Ingawa kumekuwa na hofu kwamba, Alexis Sanchez amepunguza kasi lakini kurejea kwa Theo Walcott pia kumeamsha matumaini kwamba Arsenal sasa ina kikosi kipana. Usisahau Olivier Giroud amekuwa akiwasha moto ile mbaya.

Utagundua kitu hapa, hakuna aliyekuwa akimzungumzia Wenger kwa ubora wa upangaji timu au vyovyote vile. Lakini kupoteza mechi mbili ndani ya 10, limekuwa tatizo kubwa sana! Lawama zote kwake, mtamuua.

Ligi kuu:

Rekodi ya mechi sita zilizopita kwenye Ligi Kuu England zinaoneysha Arsenal imeshinda tano na kupoteza moja na iko katika nafasi ya tatu.

Ukichukua timu tano za juu katika msimamo, zinaonyesha Arsenal ndiyo yenye rekodi bora zaidi angalau vinara Chelsea ambao katika mechi sita wana sare mbili. Wengine wote kama Man City, Man United na Southampton, hawaifikii Arsenal kwa kuwa wamepoteza zaidi au lundo la sare.

Dhidi ya Monaco:

Mashabiki wa Arsenal hawana lolote la kumlaumu Wenger. Hata wakati wanakwenda katika mechi dhidi ya Monaco walikuwa na matumaini makubwa kwa kuwa uchezaji wa timu katika mechi za nyuma ulikuwa bora.

Kufeli kwa kikosi cha siku hiyo kikiwa na Cazorla, Sanchez, Ozil, Giroud, Danny Welbeck na wengine wote waliokuwa wanalaumiwa, tatizo ni kwa Wenger pia? Alikosea nini hasa?

Mchezo wa soka una mambo mengi, wakati mwingine mchezo hukataa kwa mchezaji mmoja, lakini mchezo unaweza kukataa kwa timu kabisa.

Bado rekodi zinailinda Arsenal, kwani ndani ya mechi 10 za nyumbani na ugenini, imepoteza mbili tu. Imefunga mabao 23 na kufungwa manane tu.

Lakini bado mashabiki wa Arsenal ‘wamekalili’ na wanaamini Wenger ni tatizo, tena wanasema bila ya kufanya uchunguzi kwanza. Msisahau hata wakati Sir Alex Ferguson akiwa Manchester United wengi walisema ni tatizo, aondoke. Leo kila mmoja anamlilia. Mtamkumbuka huyu Wenger.


MICHEZO:

Jan 4

Arsenal 2 – 0 Hull City

Jan 11

Arsenal 3 – 0 Stoke City

Jan 18

Man City 0 – 2 Arsenal

Jan 25

Brighton 2 – 3 Arsenal

Feb Mosi

Arsenal 5 – 0 Aston Villa

Feb 7

Tottenham 2 – 1 Arsenal

Feb 10

Arsenal 2 – 1 Leicester City

Feb 15

Arsenal 2 – 0 Middlesbrough

Feb 21

Crystal Palace 1 – 2 Arsenal

Feb 25

Arsenal 1 – 3 Monaco



TAKWIMU:

Mechi 10

Wameshinda 8

Wamefungwa 2

MABAO:

Wamefunga 23

Wamefungwa 8

Ndani ya siku 53, wamecheza mechi 10 ambazo ni dakika 900.



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic