February 6, 2015


Baraka Kizuguto umepata nafasi ya kuwa Msemaji wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) ikiwa ni miezi kadhaa baada ya kuondoka Yanga.
Nafasi uliyoipata, haiwezi kuwa bahati nasibu kwa kuwa tumeelezwa kuna wengine takribani kumi walijitokeza kuiwania.


TFF wamekupa nafasi hiyo kwa kuwa wanatambua una taaluma mbili, kwanza uandishi wa habari na pili IT (teknolijia ya mitandao).

Kwamba unaweza kubuni au kutengeneza tovuti za aina mbali, lakini unaweza kuendesha tovuti. Pia ni mmoja wa Watanzania wachache wanaoweza kufanya kazi wakati wa dirisha la usajili kupitia utaalamu wa TMS.

Katika hili narudia kauli yangu kwamba haukubahatisha, badala yake vitu ulivyonavyo vimekupa nafasi hiyo.

Kabla haujaondoka Yanga ulikuwa na malumbano mara kadhaa na waandishi wa habari, mimi mmoja wapo.
Lakini tuliwahi kukutana, nilikueleza malalamiko yangu na vitu ambavyo sikupendezewa, mwisho tulifikia mwafaka na tukashirikiana kikazi.

Sikuwahi kushirikiana nawe kikazi tokea umeondoka Yanga, hivyo nakukaribisha tena nikiamini kupitia Yanga utakuwa umejifunza mengi ingawa utakuwa una changamoto kupitia Boniface Wambura.

Wambura ni kati ya waandishi wakongwe wa michezo nchini, naamini utendaji wake ulikuwa wa kiwango cha juu na utalazimika kujifunza zaidi.

Wako wanaotamani ukosee na huenda wakakaa mkao wa kula wakisubiri lini utateleza. Lakini kama unataka kujifunza, haupaswi kuwa na hofu na unaweza kutenda kwa kuangalia mazuri na mabaya.

Maadui hawawezi kukosekana, hauwezi kujua nafasi uliyoitaka, huenda wako walioitaka au walitaka wapate rafiki zao wa karibu, hivyo wanaweza wasipendezewe.
Ushauri wangu, haupaswi “kutanua masikio” na kuyafanya yasikilize hata visivyokuwa vya msingi badala yako majibu yawe kwa vitendo.

Kwa kuwa unafanya kwenye taasisi ya umma, pia usiwe mbishi kukosolewa inapotokea na kikubwa ni kuwa mtu unayeamini, kila unapokosea unapata nafasi ya kujua jambo jipya na kujirekebisha, maana yake faida ni mara mbili.

Kawaida yangu sijawahi kukata tamaa au kukatishwa tamaa na wale wanaosema wakiamini kusema ni kunichanganya.

Kila mtu ana aina yake, wewe unaweza kuwa tofauti na kuumizwa. Lakini kazi yako ndiyo Watanzania wanaoisubiri na huenda wale wasiofurahia hatua zako wakakosa la msingi la kuzungumza kama utakuwa mchapakazi.

Kubaki ukishindana nao ni kupoteza muda, kulazimisha kujibizana nao ni kupunguza kasi ya utendaji wako.

Kwangu nikuahidi ukiwa tayari tutashirikiana, ukiwa hauelewi nitakukosoa lakini nikuhakikishie nakuombea ufanikiwe kwa kuwa utendaji wako ukiwa bora, tutaendelea kuusaidia mpira wetu wa Tanzania na hilo ndilo lengo namba moja.

Kumlazimisha punda akimbie kama farasi, ni kumtafutia kifo. Kuyalazimisha masikio yako yasikie yasiyo na maana ni kupoteza wakati, piga kazi tushirikiane kuusongesha mpira wetu na kuthibitisha kwamba taaluma ya habari ni sehemu ya mchango.

Ahadi yangu ni kukuunga mkono bila ya woga, kukosoa inabidi bila ya kuyumba na kuungana na wewe panapokuwa panahitaji utaifa.

Karibu tuungane mkono, karibu tena tukosoane kwa ajili ya kuusaidia mpira.


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic