February 14, 2015

Giza jijini Milan….


Na Saleh Ally
KILA timu ya Ligi Kuu Italia ‘Serie A’ imebakiza mechi 16 kuhitimisha msimu wa 2014-15 na pia kupata uhakika nani atakuwa bingwa tena.


Juventus kutoka Turin ambayo safu yake ya ushambuliaji inaongozwa na Muargentina, Carlos Tevez inaendelea kukimbiza ile mbaya kwa kuwa na pointi 53 kileleni.

Timu mbili pekee za AS Roma yenye pointi 46 na Napoli yenye pointi 42 ndizo zinazoonekana kuifukuza kwa kasi timu hiyo ya Turin kuuwania ubingwa huo wa Italia.
Kazi si rahisi, Juventus inatakiwa kushinda wastani wa mechi 10 kati ya hizo 16 ili kujihakikishia nafasi ya kuwa mabingwa tena.

Wakati Juventus ikiwa inapambana kuendeleza heshima ya ubingwa, mambo katika Jiji la Milan yanaonekana kuwa hovyo kabisa na unaweza kuyafananisha na kiza au giza.

Miaka minne iliyopita, kawaida timu tatu za AC Milan, Juventus na Inter Milan ndizo zilizokuwa zinafukuzana kwa kasi kileleni hasa inapofikia hatua kama hii.

Leo, baada ya mechi 22, AC Milan na Inter Milan kutoka katika jiji hilo la kimahaba wana pointi 29 tu kila upande, tena zikiwa katika nafasi ya 10 na 11!

Kila timu kati ya hizo mbili imewahi kuwa bingwa wa Ulaya kwa nyakati tofauti. Ndiyo baadhi ya timu chache zilizobeba heshima ya soka la Italia.

Kama unakumbuka zinatumia uwanja mmoja, lakini unakuwa na majina mawili, San Siro na Giuseppe Meazza, kulingana na unatumiwa na timu ipi. Ndiyo timu zenye upinzani mkali Ulaya lakini zinatumia uwanja mmoja kama ilivyo kwa Simba na Yanga, hapa nchini.
Lakini sasa zinaonekana kupotea na hata kufikia hatua ya kutia hofu kutokana na mwenendo wake wa kupapasa gizani ili kutafuta njia sahihi.

Inter Milan:
Baada ya kushuka dimbani mara 22, ina pointi 29 ikiwa katika nafasi ya 10. Hii ni baada ya kushinda mechi saba, sare nane na kupoteza saba.

Kwa upande wa takwimu za mabao, washambuliaji wake wamefunga mabao 33 wakati kinara wa Serie A, Juventus ana 47.

Angalia, mabao ya kufunga ni hayo 33, lakini utaona kuwa ina safu nyanya ya ulinzi baada ya kuruhusu kufungwa mara 29, ikiwa ni tofauti ya mabao manne tu.


AC Milan:
Iko katika nafasi ya 11, katika mechi zake tano zilizopita imeshinda moja, sare moja na kupoteza tatu. Rekodi inaonyesha katika mechi 22 ilizocheza imeshinda saba, sare nane na kupoteza saba.

Wakati safu ya ushambuliaji ya AS Roma iliyo katika nafasi ya pili ikiwa imefunga mabao 36, AC Milan imejikongoja na kufikisha 32, lakini ushindi ndiyo tatizo kwao.
Kwa upande wa mabao ya kufunga, AC Milan nao wametikisa nyavu mara 32 na kufungwa 29, ikiwa na tofauti ya mabao manne tu.

Kwa mwendo wa timu zote mbili, kamwe hauwezi kuzipigia hesabu ya kushinda mechi 10 kati ya 16 zilizobakiza.

Hata kama watashinda nusu ya mechi hizo, mfano washinde nane, watakusanya pointi 24, ambazo ukijumlisha na walizonazo sasa watakuwa na pointi 53 ambazo sasa Juventus tayari wamefikisha.

Kwa mwendo wa Juventus, kama itashinda mechi tano tu, itakuwa na uhakika wa asilimia mia, haiwezi kufikiwa na timu yoyote.

Swali la kujiuliza giza lililotamba jijini Milan chanzo chake ni nini? Maana lilikuwa linajulikana kama jiji la soka!

Sasa limebaki kuwa jiji la wanamitindo na mambo si mazuri kwa timu zake za soka zenye majina makubwa zilivyokuwa zinafanya hapo awali na sasa ni aibu tu. Soka limeikimbia Milan.


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic