March 27, 2015


Na Saleh Ally
KIUNGO mshambuliaji wa Yanga, Simon Happygod Msuva amefikisha mabao 11 huku Yanga ikiwa kileleni kwa pointi 40 baada ya kucheza mechi 19.


Kasi ya Msuva imekuwa gumzo kwa kuwa ameonyesha uwezo mkubwa katika mambo mengi. Ingawa kitaalamu unaweza kusema si mzuri sana katika umaliziaji.

Kila anavyocheza, anavyoaminiwa ana nafasi ya kubadilika na kufanya vizuri zaidi ya hapo maana ndiyo ana miaka 22 tu.

Miaka 22 ya Msuva tayari ameanza kuchukuana na wachezaji mahiri kama Didier Kavumbagu, Emmanuel Okwi katika ufungaji. Hii ni sehemu ya kuonyesha ubora sahihi alionao na unaweza kuongezeka kama ataendeleza juhudi.

Hakuna anayeweza kusema Msuva amefikia hapo kwa kuwa ana bahati. Kila mmoja anajua alianzia katika muziki, alicheza shoo lakini mwisho mambo yamekwenda vizuri katika soka. Je, Msuva anataka kumalizia soka lake Tanzania?

Jibu ni hapana, mara kadhaa ameweka wazi ndoto zake za kutaka kucheza nje ya Tanzania. Anataka kwenda lini? Au kama haondoki sasa anasubiri nini?

Mara kadhaa, wachezaji wengi wamekuwa wakikosea wakikosea wakati wa kwenda kucheza nje ya Tanzania. Wanaendelea kubaki, huku wakitamani sifa na ufalme wanaopewa kwa wakati husika uendelee.

Samatta&Ulimwengu:
Wako wengi walifeli na kutaka kuondoka nchini kwenda Ulaya wakati umri ukiwa unaingia ‘jioni’, unawajua. Lakini wako walioshituka na kuwahi na mfano unao.

Mbwana Samatta na Thomas Ulimwengu sasa wanacheza TP MAzembe ya DR Congo, moja ya timu bora barani Afrika na inayojulikana karibu duniani kote.

Samatta na Ulimwengu ni tegemeo la Mazembe na imekuwa hivyo kutokana na vipaji na juhudi zao lakini ‘target’ sahihi, wameondoka nyumbani mapema, umri ukiwa unawaruhusu.

Msuva anasubiri lini? Anasubiri kesho? Kama ni kwenda nje ya Tanzania, hakika ana uwezo ambao utawashawishi.

Kama ni kwenda Ulaya, basi Msuva hapaswi kuwa na hofu hata kidogo kwa kuwa tayari ameaminiwa na lundo la Wazungu tena kutoka nchi tofauti.

Mzungu aliyeanza kuonyesha imani kubwa kwake ni Kim Poulsen akiwa na timu za vijana. Wako hawakuamini Msuva angeweza, yeye aliamini tofauti na hilo likawezekana.

Baada ya hapo ikawa ni nafasi pia kwa Mzungu mwingine kutoka Uholanzi, Ernie Brandts kumuamini. Aliendelea kufanya hivyo hata kama wengine hawakuona anafaa sana.

Kocha kutoka Brazil, Marcio Maximo yeye hakumpa nafasi kubwa sana. Hata hivyo mara kadhaa alioenekana angalau kumuamini kidogo na akaendelea kuonyesha anastahili kuaminiwa.

Ujio wa Hans van der Pluijm raia wa Uholanzi ambaye alishamwamini Msuva awali, umezidi kuthibitisha kwamba kweli ana uwezo ingawa anatakiwa kujifunza zaidi.
Wazungu kutoka Uholanzi na Denmark wameonyesha wanamwamini Msuva. Vipi wa Hispania, Ureno au kwingineko watashindwa kumwamini?
Utaona tofauti kubwa kipindi hiki namna anavyokokota mpira, anavyokimbia nao hata kutoa pasi, kuna tofauti kubwa na ulivyomuona miezi sita iliyopita.

Meneja:
Huu ndiyo wakati wa meneja au wakala wa Msuva kufanya kazi ya kuhakikisha anapata timu nje ya Tanzania.

Akisubiri akafikisha miaka 28 au 29 ndiyo aanze kutafuta atakuwa amechelewa. Msuva mwenyewe akiona ni raha sasa kupambwa au kuonekana mfalme hapa nyumbani, pia atachelewa.

Hakuna Yanga wanaopaswa kulaumu kuondoka kwa Msuva. Simba walikubali Samatta ameondoka, leo kuna nyota kibao wanaendelea kuibuka, huo mfumo wa maisha ya soka.

Unazaliwa hapa, unakulia huku halafu unafanikiwa kule. Vitu vinapishana na Msuva ana ndoto zake. Wampe nafasi azifikie ndoto zake, pia aipe Yanga cha kujivunia na kujitangaza zaidi duniani. Hakuna haja ya kusubiri kesho ambayo haiwezi kuwa kama anavyofanya leo.




0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic