April 11, 2015


Na Saleh Ally
YANGA sasa inaweza kuwa mfano ikiwezekana kwa kila klabu kutokana na mwenendo wao mzuri katika kila eneo.


Hata kama si kwa asilimia mia, lakini asilimia nyingi zaidi inaonyesha kuna utulivu, ushirikiano na umoja.

Kwa upande wa timu, Yanga ndiyo wana kikosi imara zaidi ambacho kina kila dalili ya kuwa bingwa wa Tanzania Bara na kuipokonya taji Azam FC kama si maajabu ya mpira. Kufikia hivyo, haiwezi kuwa kazi rahisi.

Katika mahojiano maalum na Makamu Mwenyekiti wa Yanga, Clement Sanga ambaye anaeleza mambo mbalimbali yaliyofanya Yanga kuwa imara zaidi msimu huu, lakini pia walipofeli na kipi wamepanga kukifanya ili kuimarika zaidi.


Yanga ina tofauti kubwa na miaka ya nyuma, sasa kuna utulivu na mshikamano. Je, nini siri ya hili?

Sanga: Kweli klabu kwa sasa ina utulivu mkubwa kwa kuwa uongozi ni ule ulio tayari kupokea changamoto na kuzifanyia kazi.

Lakini utaona, viongozi ni wale wanaojituma na kutakiwa na wanachama. Yaani hawapo tayari kuharibu kwa hofu watakosa nafasi ya uongozi, badala yake wanataka kufanya kile kilicho sahihi.

Hii imesaidia kuwaunganisha watu ambao nao wapo tayari kushirikiana nao.

Kuna marekebisho ya katiba, nini faida yake?
Sanga: Yamekuwa na faida, pia hasara zake. Lakini utaona sasa kuna watu maalum kwa ajili ya kufanya kazi fulani, si kila mtu anaweza kufanya.

Hiyo inaipa klabu nguvu na kazi kufanyika kwa mpangilio zaidi kwa kuwa klabu inaweka mambo wazi, yaende vipi na hakuna utata.

Awali kila mmoja alikuwa anataka afanye anavyotaka yeye. Lakini pia mabadiliko hayo pamoja na utendaji wa uongozi wa juu, mimi na mwenyekiti wangu (Yusuf Manji) tunaendana kimawazo, nini tunataka kufanya kwa manufaa ya klabu na hata tukipishana bado inakuwa ni kwa faida ya klabu.

Kuifuata katiba, kunasaidia kutokuwa na migogoro. Halafu uongozi wa juu unapoelewana, unasaidia kutoibuka kwa migogoro pia.

Kuna shida kidogo, bado kuna wale ambao wako katika kamati mbalimbali hasa wa kuteuliwa. Wanakuwa hawana morali maana wana mambo yao mengi. Hapa ni lazima kuwe na mabadiliko kwa kuwa kazi hii ni ya kujitolea.

Pamoja na majukumu yangu, nimekuwa nikijitolea zaidi, lakini bado naona sijafanya vya kutosha kuisaidia Yanga.

Sasa kuna umoja wa hali ya juu kwa wazee na vijana kutaka kuisaidia klabu. Nini kimefanyika kuwashawishi hadi wanajitolea kiasi cha juu kabisa?

Sanga: Kwanza tuliwaeleza ukweli kwamba kikatiba hawatambuliki, lakini bado tukaendelea kuyaenzi makundi haya. Hata kitaifa hakuna wazee wa Dar es Salaam. Lakini rais huwaita na kuzungumza nao, wana umuhimu wao.

Hali kadhalika, uongozi wetu ulilitambua hilo. Tumeendelea kuwaenzi, tunafanya nao kazi vizuri. Tunachukua maoni yao na tunayafanyia kazi kwa niaba ya klabu.

Wachezaji wanaonekana kucheza kwa ari kubwa, mmeweza kuwashawishi kwa kipi, mishahara mikubwa au kwa njia zipi?

Sanga: Sisi ni binadamu, huenda kuna makosa tunafanya. Lakini ukizungumzia kulipa, mara nyingi tunajitahidi malipo yawe kwa wakati.

Tuko karibu na wachezaji na benchi la ufundi na tunawapa nafasi ya kufanya kazi yao kitaalamu.

Mlimuondoa Marcio Maximo ikiwa ni siku chache baada ya kumleta kutoka Brazil. Unafikiri mlikurupuka kumleta, pia mkafanya hivyo kumuondoa?

Sanga: Kila kocha ana falsafa yake, (Hans van Der) Pluijm ameonyesha ni kama mzazi, anajua namna ya kukaa na wachezaji, anajua afanye nini kupandisha viwango vyao.

Kama unakumbuka tuliamua kumleta Maximo baada ya kuondoka kwa Pluijm ambaye alipata ofa kubwa sana Saudi Arabia. Tusingeweza kumzuia yeye na (Boniface) Mkwasa, nao ni binadamu na wanatafuta maisha.

Tulimleta Maximo ingawa kweli tulipata ushauri kwa baadhi ya watu wakieleza matatizo yake. Lakini bado tuliamini atatusaidia, kama unakumbuka Taifa Stars yake ilifanya vema kiasi fulani.

Lakini kufanya naye kazi ilikuwa ni kazi ngumu, hapokei ushauri, anaamini anajua zaidi na yeye ni kocha mkubwa. Ikatushinda, tuliamua kumrudisha Pluijm.

Utaona, anafanya kazi vizuri. Wachezaji kama Msuva sasa wamepanda tena viwango baada ya kuwakuta wameporomoka kabisa.

Amejenga timu kwa muda kidogo, utaona tulishinda mbili, tatu. Sasa ni hadi tano au nane. Kikosi kinakwenda kinaimarika.

Mnafanya vizuri michuano ya kimataifa na nyumbani, sasa mnakutana na Etoile du Sahel ya Tunisia. Hawa ni Waarabu, mnalitambua hilo?
Sanga: Tunalitambua hilo, Yanga ya sasa imebadilika, hata wachezaji wanajua wanataka nini. Wanataka wafanye kitu kipi, mshikamano na wanachama na mashabiki uko juu.

Ndiyo maana Yanga imepoteza dhidi ya Simba, siku chache watu wamesahau kwa kuwa wanajua wanataka nini.
Maandalizi yameanza, tunaweza hata kuwahi Tunisia. Msimu uliopita Yanga iliifunga Al Ahly Dar es Salaam, tukatolewa kwa penalti kule Alexandria, Misri. Tulivunja mwiko wa kutowafunga Waarabu hasa wa Misri. Tunataka kuendeleza zaidi ya hapo.

Mnajitahidi kufanya mazuri, lakini Simba inaonekana kuwashinda kabisa, kwa nini?
Sanga: Naamini uongozi wetu hauko madarakani kuifunga tu Simba. Kwanza ni kuchukua ubingwa. Ingekuwa lengo ni kuwashinda Simba pekee, tusingekuwa hapa leo. Lakini tunaendelea kujiweka sawa, siku tutafanikiwa.

Unafikiri uongozi wa juu wa TFF kuwa na Yanga wengi inawasaidia?
Sanga: Yamekuwa ni mawazo ya wengi, kwanza tunakubali TFF ina Yanga wengi. Lakini kwetu tunaona ndiyo inatuumiza zaidi, huenda wanahofia kutenda haki kwa kuonekana Yanga. Angalia suala la kadi tatu za njano za Ibrahim Ajibu wa Simba, liko wazi ni tatizo lakini TFF imeshindwa kuchukua hatua.

Yanga inahusika katika historia ya uchumi wa nchi hii. Tena kupitia CCM, sasa kabla hawajachagua mgombea, mnamuunga mkono nani?

Sanga: Hatutaingia katika kundi lolote, hatumuungi mkono mwanachama yeyote wa CCM, Chadema au chama kingine chochote. Wala hatutajiingiza kwenye kampeni za wagombea.

Ila tunaweza kufanya mambo ya kijamii, mfano kuhimiza watu wapige kura. Watu wawe makini kuepusha vurugu na kuipoteza amani yetu na si vinginevyo.

Naona kama unakimbia kuingia ndani ya CCM, wakati hata mkishinda, mashabiki wenu huimba “CCM, CCM”

Sanga: Nafikiri ni historia, pia ishu ya rangi za njano na kijani. Lakini unaweza kuwa CCM ukawa Simba. Mfano mzuri ni Profesa Philemon Sarungi, Juma Kapuya au Ismail Aden Rage na wengine wengi.

Inaonekana kujenga uwanja kumewashinda kabisa, ni kweli?

Sanga: Tuna maombi yetu ya kuongezewa sehemu tuliyapeleka serikalini. Hadi sasa tunaendelea kusubiri na hilo ndilo linalotukwamisha.






1 COMMENTS:

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic