April 22, 2015


Na Saleh Ally
MWISHO ilikuwa mwaka 2012 baada ya Simba kuonja utamu wa ubingwa wa Ligi Kuu Bara, baada ya hapo imekuwa ni sawa na hadithi tu.


Taji la mwaka 2012 lilikuwa na kumbukumbu ya aina yake kwa kuwa Simba ilibeba ubingwa baada ya kuwaadhibu watani wake Yanga kwa kichapo cha kukumbukwa. Simba ilishinda kwa mabao 5-0 katika mechi ya mwisho ya ligi.

Baada ya hapo, Simba imefanikiwa kujipoza na makombe ya michuano mifupi kama Kombe la Mapinduzi, ubingwa wa mechi ya kirafiki ya Nani Mtani Jembe na kadhalika.

Hata iwe vipi, Simba inastahili ubingwa. Hilo ni lazima na hakuna anayeweza kupinga kwa kuwa ni klabu kubwa na historia yake inaweza ikawa inawahukumu kwa kuwadai ubingwa.

Miaka mitatu sasa, msimu huu bado Simba haina uhakika wa kubeba ubingwa wa Tanzania Bara. Yanga wana asilimia 90 ya kubwa mabingwa, Azam FC 78% na Simba 46%.

Bila shaka Simba haiwezi kuwa bingwa, lakini katika nafasi ya pili, Azam FC ina 93% ya kuishika nafasi hiyo na Simba 79%.

Inaonekana hata nafasi ya pili kwa msimu wa tatu kwenda wa nne ni uhakika Simba haiwezi kushinda nafasi zote mbili za juu ambazo Yanga na Azam wamekuwa wakizitawala.

Miaka mitatu yote, Yanga imebeba ubingwa mara mbili na Azam mara moja. Simba imeendelea kuambulia patupu na nafasi zake ni ya tatu hadi tano, inatia huzuni.

Kinachoonekana Simba haiko vizuri, baada ya timu yake ya msimu wa 2011-12 kuvurugika, kuanzia hapo imeanza kuyumba na hakukuwa na mipango dhabiti ya kuitengeneza upya.

Wachezaji takribani sita wa kikosi cha kwanza wakiwemo Kelvin Yondani, Emmanuel Okwi na wengine wengi waliondoka na hawakupata warithi sahihi, japokuwa Okwi amerejea sasa.

Simba iliamua kujipanga kwa kutumia vijana zaidi. Imewalea na kuwakuza wengi, baadhi yao kama Jonas Mkude, Ramadhani Singano ‘Messi’, Hassan Isihaka sasa ni tegemeo.

Hali kadhalika Ibrahim Ajibu, Said Ndemla na wengine wengi sasa wamekuwa tegemeo kwa Simba na wanapambana kuisaidia timu. Ni jambo zuri.
Pamoja na mazuri ya vijana hao, huu ni wakati mwingine mwafaka, Simba inapaswa ibadilike na kuamini sasa inatosha kuendelea kusajili wachezaji wengi kwa ajili ya kujifunza.

Simba inahitaji wachezaji hasa ambao wana uwezo wa kucheza. Haina maana wawatupe wachezaji vijana. Utaona imetumia chipukizi wengi zaidi kwa miaka mitatu sasa na jibu liko wazi, hawawezi kubeba kombe.

Makocha wawili walikuwa wazi na kusema Simba haiwezi kubeba ubingwa kwa kikosi cha watoto wengi. Kocha Milovan Cirkovic ndiye aliyekuwa wa mwisho mwenye kikosi imara zaidi, alipotua Patrick Liewig ‘akatiwa ndimu’ kuhusu vijana, akawatupa wakongwe wote.

Ujio wa Zdravko Logarusic ulikuwa na mabadiliko kwa kuwa alikuwa mkweli zaidi na kueleza si rahisi kubeba kombe na watoto. Alionekana hakuwa sahihi na ana tabia ya kikorofi.

Patrick Phiri raia wa Zambia ambaye amewahi kuinoa Simba na kuipa mafanikio makubwa naye alilisema hilo la vijana. Kwamba timu yake ina watoto na vijana wengi, hivyo si rahisi kuzungumzia ubingwa.

Kama Simba wanataka ubingwa, basi suala la kujaza vijana wengi kwa madai wanawakuza, sasa basi imetosha. Vijana waliowakuza kama akina Ndemla, Mkude na wengine wanawatosha.

Wanaweza kuendelea kuwakuza wengine kwa kuwaingiza wachache katika kikosi kikubwa na wengi vijana wakabaki katika kikosi cha vijana lakini si vijana wengi kuwa katika kikosi kikubwa, hakika Simba haitafanikiwa.

Kama Simba inataka kuwa timu ya kuwania ubingwa, bado ina nafasi iwatumie vijana ilionao sasa kwani tayari wameanza kukomaa. Halafu iongeze angalau wachezaji 10 wa uhakika. Mfano wageni watano, pia wachezaji wa nyumbani watano.

Suala la kukuza vipaji ni zuri na la uhakika lakini Simba lazima ikubali kuwa inatakiwa kuchagua. Kuendelea kukuza vijana au kugombea kutwaa ubingwa.



1 COMMENTS:

  1. Simba waache kusingizia kukuza vipaji wakati kila wakikutana na yanga wanaifunga,sasa kwanini wasiwafunge na Mbeya city?Mipira ya kishirikina ndio tatizo la simba hawachezi kwa ufundi uwanjani zaidi ya kuroga tuu.
    Simba ina wachezaji wakigeni watano,pia ina Ivo mapunda,cholo,Baba ubaya na wengine kadhaa wote ni watu wazima kumkaribia Saleh Ally,sasa utoto wao ukowapi?
    Mwandishi wa makala hii naye anaegemea kulekule eti wanakuza vipaji,huu sasa ni mwaka watatu hivyo vipaji havikui tuu/
    Acheni longolongo chezeni mpira.

    ReplyDelete

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic