April 13, 2015


MASHABIKI wa Yanga kutoka katika kundi linalojulikana kama Yanga Facebook Family, wamejitokeza na kutoa tuzo kwa kikosi kizima cha Yanga.


Zawadi hizo zilikabidhiwa juzi kwenye Uwanja wa Karume, Ilala jijini Dar es Salaam wakati Yanga ikiendelea na maandalizi yao kujiandaa na mechi ya leo dhidi ya Mbeya City.

Uamuzi wa mashabiki hao ambao sasa taratibu wanakua na huenda wakawa taasisi inayotambulika unaonyesha kiasi gani mapenzi ya dhati yanavyoweza kupita katika njia sahihi.

Walichofanya ni kutoa tuzo kwa kikosi kizima cha Yanga wakianza na wachezaji, mtunza vifaa, mchua misuri, daktari, meneja, kocha msaidizi na kocha mkuu.


Zawadi walizotoa ukiziangalia unaweza kudharau, lakini hakika wanaonyesha ni watu waliojipanga na walikusudia kufanya jambo kwa ufasaha kabisa.
Walitoa flemu maalum zilizoandikwa majina ya wahusika kukiwa na picha zao, walitoa vinyago hii wakionyesha kudumisha thamani ya utamaduni wa Mwafrika.

Pia walitoa picha maalum, kubwa zenye ujumbe unaoonyesha kuthamini kazi ya mchezaji husika ikiwa ni sehemu ya morali kukitaka kikosi chao kiendelee kupambana vilivyo kwa kuwa kazi bado.

Sijuo Yanga Facebook Family wanaendesha mambo yao namna gani. Lakini ni watu ambao wameonyesha mabadiliko makubwa kwa kuwa safari hii mashabiki ambao wako karibu na timu wamekubali kutoa chao mfukoni ili kuipa timu morali.

Huenda wako wachache waliwahi kufanya hivyo huko nyuma, hongera zao. Lakini leo Yanga Facebook Family ndiyo wanastahili pongezi kwa kuwa wameonyesha unaweza kuipenda Yanga bila kupata chochote unachoweza kuingiza mfukoni.

Mashabiki wengi wa Yanga au wanachama nimekuwa nikipambana nao kuwaeleza ukweli kuhusiana na suala la mapenzi feki kwa klabu zao, wanajidai wanazipenda kumbe ndiyo sehemu yao ya kuchumia riziki.

Wako wale ambao ni wapambe wa baadhi ya viongozi wa klabu hizo. Wanajua watapata chochote kila watakapomuona kiongozi wa klabu. Wanasingizia mapenzi, kumbe ni ahueni ya njaa zao.

Wako ambao wamekuwa wakigombana na viongozi wanaopeleka mambo yakiwa yamenyooka. Lakini wanawachukia kwa kuwa tu hawawapi fedha au ‘hawawapozi’ ili wapate kupunguza ukali wa maisha.
Mashabiki au wanachama hao wako tayari hata kumuumiza mtu wakisingizia eti wanaipenda sana Yanga. Wanafanya hivyo kwa kuwa Yanga ni mtaji wao wa kujipatia riziki.

Najua mmekuwa mkikasirika sana kueleza ukweli. Mimi natumia nafasi hii kuwakasirisha tena kwa kuwakumbusha kuwa Yanga Facebook Family wamewaumbua na wanaonyesha unaweza kuipenda Yanga bila ya kuwa katika kundi la Makomandoo wenye jeshi feki.
Wanachama na mashabiki hao wamekuwa wakisababisha chokochoko mara kwa mara ndani ya klabu ya Yanga kwa kuwa tu hawakupewa fedha, hawakupewa nafasi ya kukaa milangoni au vinginevyo.

Wamekuwa wakianzisha vita na waandishi bila ya sababu za msingi, kisa eti bosi fulani kasemwa vibaya. Ukiulizwa utaambiwa ndiye ambaye amekuwa ‘akiwapoza’, hivyo wanataka kumuonyesha hasira na machungu yao kwake, ili awapoze zaidi.

Usipokuwa makini, utaona kweli ni watu wanaoipenda klabu hiyo, kumbe ni wale wanaothamini matumbo yao na mapenzi yao kwa klabu ni kunufaisha nafsi zao. Hii ipo hata kwa jirani au watani wao Simba ambao pia wana hao wanaoamini wao ni makomandoo ambao kwangu nimekuwa nikiamini ni feki na hawana msaada wowote katika klabu hizo mbili kongwe.

Kundi la Facebook Family, walisafiri kwa wingi hadi Zimbabwe kupambana kuhakikisha Yanga inasonga mbele. Kweli imekuwa hivyo.

Sasa wametoa zawadi, ambayo ni motisha ya juu, ikiwezekana hata uongozi au wadhamini wa klabu hiyo hawakuwahi kufanya.

Ukiangalia vitu walivyotoa, kwangu nakadiria haiwezi kuwa chini ya milioni nne tano. Sasa hauoni hawa watu wanaipenda klabu yao? Vipi wewe unayetaka klabu ndiyo ikupe fedha, acheni kabisa. Iko siku nitawataja kwa majina, mmoja baada ya mwingine. Subirini tu.




0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic