April 13, 2015


Na Saleh Ally
UJIO wa Klabu ya Azam FC umekuwa ukizungumzwa kama sehemu ya mapinduzi ya mchezo wa soka nchini.


Kwamba ndiyo wakati mwafaka wa kuhakikisha mabadiliko yanapatikana na kuachana na mengi yaliyotufelisha huko tulikopita. Unaweza kusema ndiyo kwa kuwa walianza kuonyesha mfano.
Azam FC wamejenga sehemu nzuri kwa ajili ya kukuza vipaji na wana uwanja wao ambao ni kati ya viwanja vinavyotumiwa katika Ligi Kuu Bara.

Ndani ya misimu minne, tayari Azam FC wamefanikiwa kutwaa ubingwa wa Tanzania Bara. Lakini walifanikiwa kushika nafasi ya pili mara mbili.

Utaona ni kikosi kilicho na mwendo mzuri na wa kuvutia. Lakini baada ya hapo, yakaanza kuingia mambo mengi ya “Kiswahili”.

Haikuwa rahisi viongozi wa Azam FC kukubali kwamba kuna mambo hayafai yamekuwa yakiingia ndani ya klabu hiyo, huenda kutokana na suala la kimaslahi.

 Kunapokuwa na maslahi kawaida fitna haikosekani, huo ndiyo ulikuwa mwanzo wa Azam FC kuwa na maneno mengi ya chinichini.
Huenda hii ilikuwa na tofauti kubwa ukilinganisha na wamiliki wake walikuwa wanataka nini hasa katika maendeleo ya klabu hiyo.

Sifa moja ya Azam FC wakati ikipanda lilikuwa ni suala la maendeleo na kwenda mwendo tofauti na wakongwe wa soka nchini. Huenda wapo wengi walioitumia Azam FC kama fimbo kuzichapa Yanga na Simba. Lakini sasa mbona ndani ya klabu hiyo changa ni yaleyale kama ya Simba?


Tunajua kumekuwa kuna hali ya kutoelewana kati ya viongozi na wachezaji au wachezaji na viongozi. Hilo likizungumzwa kwa kuwa Azam FC wamekuwa wakijiona ni bora, wasiotakiwa kuambiwa na kila wanachoambiwa wanaona wanapigwa vita, mambo yamekuwa yakijificha.

Mficha maradhi, kifo humuumbua. Juzijuzi viongozi wa Azam FC wametaka kuzichapa hadharani, tena mbele ya kundi la watu wengi. Sasa hii si siri tena!

Swali langu la kwanza, tuache kuzungumzia kwa kuwa Azam FC watasema hatuwapendi au wanasakamwa? Kwani Azam FC ni nani hasa wasiambiwe ukweli, eti watanuna? Wanune lakini ukweli unaanza leo.

Kwamba wapo watu wawe viongozi au wengineo wanaingiza maisha yao ya mfumo uleule wa Yanga na Simba uliokuwa ukionekana haufai. Ndiyo maana si rahisi wao kusikilizana.

Waliotaka kupigana hadharani ni meneja wa timu, Jemedari Said dhidi ya bosi wake, Mtendaji Mkuu, Saad Kawemba.

Juhudi za baadhi ya viongozi wengine akiwemo Iddi Cheche kama unavyoona kwenye picha ndizo zilisaidia kuzuia wawili hao kutotandikana ngumi kwa kuwa kila mmoja alikuwa tayari.

Fedheha ya kutaka kupigana mbele ya watu, tena kwenye Uwanja wa Chamazi ambako ni nyumbani kwao haileti picha nzuri. Acha hivyo, iweje hata kama wamepishana kauli walishindwa kutembea hatua 20 au 30 kuingia kwenye vyumba au ofisi zao na kulijadili hilo?

Jemedari amecheza soka, anajua namna wachezaji wanavyoweza kumuamini na kujivunia kiongozi wao ambaye ana uwezo wa kufanya maamuzi, busara pia katika uongozi.

Kawemba alikuwa TFF, mama wa soka Tanzania. Leo anaonekana anataka kupigana hadharani kwa kuwa amri yake haikuweza kutekelezwa, hili ni sawa?

Bado naamini wao ni binadamu kama walivyosema, lakini walikuwa Chamazi, sehemu ambayo ilikuwa rahisi kwao kukaa na kuzungumza au kuondoka katika macho ya watu na kuzungumza pamoja kuhusiana na hilo.

Kitendo cha viongozi hao wa juu katika kikosi cha Azam FC kutaka kupigana hadharani, kinaanza kutoa majibu kuwa kuna mambo ambayo si sahihi yanaendelea chinichini.

Azam FC wamekuwa wakijitahidi kuyaficha kutaka kuonyesha hawapendwi au vinginevyo, lakini mara kadhaa nimekuwa nikisema wazi wanataka kujikweza waonekane kama Yanga au Simba, lakini si sahihi kwa kuwa bado wanahitaji muda.

Kwangu Jemedari ni mtu mwelewa na amekuwa akitoa ushirikiano kwa wanahabari. Sijui jibu alilopewa ni nini hadi kufikia kutaka kupigana na Kawemba. Lakini lazima akubali, kwamba kuna tatizo na hawawezi kutaka kupigana kwa tatizo la siku moja tu.

Zengwe ni sumu ya soka hapa nyumbani, ingawa wapo wanaoamini mambo hayaendi bila ya zengwe. Azam FC hata kama imepata mafanikio ya haraka kwa kuwa wamiliki wana fedha nyingi, lazima ikubali kuna mengi inastahili kujifunza.

Wakati inajifunza, basi ipite njia ya kuyafanya mabaya ya Yanga na Simba ni somo kwao badala ya kurudi na kuanza kupita mulemule halafu waamini kuwa wao ni bora.

Kawemba aliyetoka TFF, anapaswa kuwa mfano. Hata kama anatoa maagizo kwa watu wake lazima akubali kutumia njia nzuri badala ya ukiwa bosi, kutaka kujifanya “Mungu”.

TFF ni kati ya taasisi kubwa zilizofeli kwa miaka nenda rudi, hata kabla ya kuingia kwa Leodegar Tenga hadi leo akiwepo Jamal Malinzi. Sasa kuna kila sababu ya Kawemba kuonyesha yuko Azam FC kuisukuma mbele na si kuingiza ‘damu’ ya TFF ambayo majibu yake ni kufeli.






0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic