May 8, 2015


KIUNGO mwenye kasi wa Yanga, Simon Happygod Msuva ameondoka nchini kwenda katika Klabu ya Bidvest Wits ya Afrika Kusini kwa ajili ya kufanya majaribio.


Rasmi Msuva ameanza majaribio jana katika timu hiyo inayomilikiwa na kitengo cha michezo cha moja ya vyuo vikuu vikongwe kabisa barani Afrika cha Wits.

Chuo hicho kipo katikati kabisa ya Jiji la Johannesburg, sehemu inayojulikana kama Sturrock Park.

Msuva ana hamu ya mafanikio, tumeona juhudi zake zilivyo na wakati Yanga inachukua ubingwa, tayari ndiye kinara wa washambuliaji waliofunga mabao mengi baada ya kuwa ametupia mabao 17.

Anakwenda kufanya majaribio akiwa mmoja wa wachezaji tegemeo katika kikosi cha Yanga na kikosi cha timu ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars.

Wakati anakwenda kufanya majaribio, lazima Msuva awe mtu anayejitambua kwamba sifa au kiwango chake ni kipi na anastahili kupata huduma ipi au ya namna gani.

Nani anayemsimamia Msuva katika suala hilo? Kama ni wakala au meneja. Je, yeye amelenga kupata nini hasa? Nia au lengo lake ni lile sawa na anachotaka kiungo huyo mwenye kasi au kila mmoja ana lake analolitaka?

Wakala wa Zlatan Ibrahimović alimkataza mchezaji wake kufanya majaribio Arsenal. Baada ya kuwa wamefika, Kocha Arsene Wenger aliwaonyesha nyodo.

Alitaka mchezaji huyo kufanya majaribio wakati wakala aliamini kwamba mchezaji wake hakuwa kwa ajili ya kufanya majaribio. Akaondoka naye, wakasafiri hadi Monaco nchini Ufaransa, kule pia mambo yakawa hayohayo.

Wakala alishikilia msimamo wake hadi Zlatan aliponunuliwa na Ajax. Leo ni kati ya wachezaji bora na matajiri. Anazeeka na mpira wake mguuni.

Utaona hapo, alichokuwa akikitaka wakala ni mafanikio ya baadaye ya mchezaji wake. Si kiasi gani cha fedha angekipata kama Zlatan angesajiliwa na Arsenal.

Sisemi wakala wa Msuva naye amkataze Msuva kufanya majaribio. Badala yake lazima awe mtu ambaye amekaa chini na kiungo huyo na kumuelewa anataka nini. Vizuri kuangalia mafanikio pia yatakuwaje kuliko kujali watalipwa nini.

Biashara ya kuuza mchezaji, inaweza kulingana na ile ya kuuza nyanya. Kwani nipunguzie ipo na kama ilivyo katika uuzaji nyanya unaposema kuwa inaonekana kuharibika upunguziwe bei, hata mchezaji unaweza kusema anatumia mguu mmoja hivyo bei yake ishuke.

Msimamo wa wakala au meneja ukoje? Msimamo huo unaendana vipi na Msuva, naye anakubaliana nao au ana hamu tu ya kucheza soka nje ya Tanzania na hasa Afrika Kusini bila ya kujali mambo sahihi yako vipi?

Bado Msuva hajafanikiwa kwa kuwa ndiyo ameanza majaribio. Kufanikiwa ni jambo moja, bei na maslahi husika ni jambo jingine. Lazima tukubaliane kwamba mtu asiye na tamaa na mzoefu ndiye anapaswa kushughulikia suala la kiungo huyo.

Kama mtu asipokuwa mzoefu, Wazungu watampiga kwa kuwa ni wajanja na wazoefu wa bishara hizo.
Tamaa pia ni jambo baya katika biashara ya uuzwaji mchezaji. Kwani meneja au wakala akiwa ni mtu mwenye tamaa, ni rahisi Msuva kuuzwa katika bei isiyo sahihi. Kumbuka Yanga walivyomuuza Nonda Shabani ‘Papii’ kwa dola 10,000 kwa Vaal Professional halafu wakaanza kujuta miaka nenda rudi.

Msisitizo, wakati yote yanafanyika. Msuva lazima ajitambue na aachane na hofu ya kufeli pia aachane na hofu kucheza ya Afrika Kusini. Ajiamini kwa kuijua thamani yake. Kila la kheri.



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic