July 20, 2015


Saleh Ally na Mtandao
UVUMILIVU wa makocha wakati mwingine umekuwa ukilipa, mfano mzuri ni pale Arsene Wenger alipoonyesha uvumilifu mkubwa wakati Robin van Persie akiwa ‘kimeo’.


Karibu misimu miwili, van Persie alikuwa ‘tiamaji tiamaji’, Wenger akamvumilia hadi aliporejea kikosini na kuwa msaada mkubwa.

Mwisho, van Persie aliipatia Arsenal faida baada ya kuuzwa kwa kitita cha pauni milioni 22.5, safi kabisa.

Safari hii ni zamu ya Theo Walcott, mchezaji ambaye amekuwa akijulikana kama kinda. Ingawa kwa sasa ameshaondoka huko, maana ana umri wa miaka 26, kisoka huyu tayari ni mchezaji aliyepevuka.

Msimu ujao wa 2015-16 utakuwa ndiyo wa uamuzi hasa kwa Walcott na dalili zote zinaonyesha kuwa ndiye atakuwa shujaa wa Arsenal kwa mambo mengi tu yakiwemo kitakwimu, kwani tayari ameshaanza kuonekana tishio kwenye mechi za maandalizi, utakumbuka juzi alifunga bao wakati Arsenal ikiichapa Everton 3-1.


Uzoefu:
Ingawa alikuwa nje ya uwanja kwa muda mrefu, Walcott mwenye asili ya Jamaica, anabaki kuwa ndiye fowadi mwenye uzoefu zaidi na soka la England katika kikosi hicho cha Wenger.

Hauwezi kumlinganisha na Mesut Ozil, Olivier Giroud au Alexis Sanchez, hivyo ndiye anayeweza kuwa kiongozi wa jahazi la utengenezaji na upachikaji mabao.

Ameonyesha kuwa atakuwa tegemeo, kwani baada ya kurejea msimu uliopita, ingawa alikuwa akipata nafasi chache za kucheza, lakini alifunga mabao na kutengeneza kadhaa.

Kwa kushirikiana na wakali ambao Arsenal imejaza katika safu yake ya ushambuliaji, Walcott anaweza kuwa msaada zaidi na kiongozi wa kufunga.

Tayari amefunga mabao 50 ya Ligi Kuu England akiwa na Arsenal aliyojiunga nayo mwaka 2005 akitokea Southampton aliyoichezea msimu mmoja katika Ligi Daraja la Kwanza England.

Kufunga hakiwezi kuwa kitu kigumu kwake, wala hawezi kuwa na hofu na beki wa aina yoyote.


Uchezaji:
Tayari Wenger amelizungumzia hilo, kwamba uchezaji wa Walcott unaonyesha kuwa ni mchezaji aliyepevuka.

Miaka mitano iliyopita, Walcott alitaka kuzichapa uwanjani na van Persie aliyemtuhumu kuwa na tabia za ‘kitoto’ kung’ang’ania mpira bila sababu za msingi. Kweli moja ya matatizo ya wachezaji makinda ni “anao anao”.

Kwa sasa inaonekana kuwa ana uchezaji tofauti, zaidi anachoangalia ni faida kwa timu na kwa kuwa ameichezea Arsenal mechi 208 za Premier League, inatosha kuthibitisha kwamba ni mchezaji anayefanya anachokijua.

Miaka 10:
Tayari amekamilisha misimu 10 ya Premier League. Si haba, tena anakuwa mchezaji anayeongoza kwa kuitumikia Arsenal kwa miaka mingi katika safu ya ushambuliaji.

Uzoefu huo unampa urahisi wa kufanya vizuri zaidi. Lazima ukumbuke Arsenal inashiriki michuano ya aina tatu England ambayo ni Premier League, Kombe la FA na Kombe la Ligi na yote Walcott amecheza.

Sasa ndiyo wakati mwafaka wa yeye kuonyesha kweli anapaswa kuwa msaada na ana uwezo wa kusaidia Arsenal iwapo atashindwa msimu huu, huenda ikawa ameshindwa kabisa.


Jezi namba 14:
Wakati anakabidhiwa jezi namba 14, kwake ilikuwa mzigo mkubwa. Unakumbuka kabla ya yeye kuichukua, ilikuwa mali ya nani?

Si unamkumbuka Thierry Henry? Gwiji, jamaa hatari aliyekuwa anajua afanye nini na mpira kwa ajili ya matokeo bora katika kikosi chake.

Wakati Walcott alipokabidhiwa, alieleza namna ambavyo alifurahia kuivaa jezi hiyo, lakini deni lilikuwa likimtafuna.

Huenda huu ndiyo wakati mzuri kwake kulipa na msimu ujao unapaswa kuwa majibu. Kama atashindwa kuwa kiongozi au nyota wa mashambulizi ya Arsenal, dalili zinaonyesha atakuwa anajisogeza mlangoni.

Kama Arsenal itashindwa kuona inamtegemea Walcott msimu ujao, maana yake utakuwa ni mwaka wa 11 ikiwa naye. Hivyo itakuwa ni kipindi mwafaka cha kuangalia haya mawili; kumuuza au kumuacha azeekee Emirates.

Maana yake Arsenal wanaweza kuwa na mawili, kumuangalia msimu ujao kwamba ameonyesha yeye ni tegemeo na ana msaada mkubwa, basi abaki.

Ikionekana pamoja na uvumilivu wa Wenger, bado ni tiamaji tiamaji, basi ili kuepusha miaka 30 kumkuta akiwa hapo, watampiga bei.

Huu ndiyo wakati mwafaka kwa Walcott kuamua mwenyewe. Msimu wa 2015-16 utakuwa fainali kwake ambayo itakuwa inaamua kumbakiza au kumuondoa Arsenal aliyoitumikia kwa miaka 10 katika Premier League.

Mabao yake 50 ya Premier League, bado hayampi nafasi ya kuwa gwiji wa Arsenal kwani kwa misimu 10 ukiyagawanya utapata 5 kila msimu.

Walcott hajafanikiwa kubeba ubingwa wa Premier League akiwa na Arsenal. Amebeba Kombe la FA na Kombe la Ligi.

Huu ndiyo wakati wa kuisaidia Arsenal kutimiza kiu yake hiyo kwani haijabeba kombe hilo tangu mwaka 2004, pia inataka kufika mbali zaidi katika michuano ya kimataifa.

Kikosi chake ni bora, Walcott anacheza katikati ya mafundi wenzake. Bila shaka hawezi kulalamika kukosa msaada. Kwa watu anaocheza nao, halafu akashindwa kufanya vema dalili za safari zitakuwa wazi maana Arsenal nayo kama timu makini itaanza kuhofia ‘uzee’ wake au ‘ukimeo’ wake kwa kuwa ni timu yenye filosofia ya ujana.

Kama ni kutengeneza rekodi nzuri yenye majibu ni sasa, yaani msimu ujao. Kwani tayari ni mzoefu, mwenyeji na yuko fiti na kwa mwonekano wa msimu uliopita baada ya kurejea, inaonekana hivi; asipoumia, hakika hakuna atakayemzuia kuwa tishio, ila akishindwa, safari itamkuta.



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic