July 15, 2015


Na Saleh Ally
ALIYEKUWA mshambuliaji wa Simba, Emmanuel Okwi inawezekana ndiye mchezaji mwenye akili kuliko wengine wote waliowahi kucheza katika Ligi Kuu Tanzania Bara tangu kuanzishwa kwake.


Utakapozungumzia mafanikio, basi Nonda Shabani ‘Papii’ anaweza kuwa ndiye mwenye mafanikio zaidi baada ya kupata nafasi ya kucheza Afrika Kusini, Italia, Ufaransa na England.

Unapozungumzia suala la biashara, basi haliwezi kupita bila ya kuwataja Wachaga. Okwi anabaki kuwa mchezaji mwenye akili zaidi ya biashara kwani ndani ya miaka saba aliyocheza Tanzania, amefanya biashara iliyotengeneza zaidi ya Sh bilioni 1.7.

Fedha hizo, hakuna mchezaji yeyote wa Tanzania au mgeni ukiachana na Nonda ambaye amewahi kuifanya isipokuwa Okwi ambaye amecheza zaidi ya timu nne katika nchi nne.


Alitua Tanzania mwaka 2008 akitokea SC Villa, binafsi ameweza kutengeneza zaidi ya Sh milioni 500 kama sehemu ya uhamisho tu, lakini ukijumlisha malipo yake yote anakuwa ni mchezaji ghali zaidi kwa ukanda wa Afrika Mashariki.

Lakini utagundua kuwa Okwi si mchezaji mwenye kipaji cha uwanjani tu, badala yake ni mchezaji anayejua kwa nini anacheza mpira na anataka nini ndani na nje ya uwanja, ndiyo maana ameweza kuchota fedha nyingi kuliko wachezaji wote walio katika Ligi Kuu Bara.

Huenda unaweza kufikiri Mbwana Samatta anayelipwa mshahara wa dola 10,000 (Sh milioni 20) anaweza kuwa na fedha nyingi kuliko Okwi. Hapana! Mganda huyo, ameweza kuingiza fedha nyingi haraka katika masuala ya uhamisho.

Karibu kila uhamisho alioufanya, Okwi anaonekana aliutengeneza kutokana na mahitaji ya timu husika. Ingawa kikubwa namba moja imekuwa ni ngao yake ya juhudi na utendaji bora kabisa anapokuwa uwanjani. Baada ya hapo timu humhitaji, naye hafanyi ajizi.


Wakati anatoka SC Villa kujiunga na Simba, Waganda hao walilipwa Sh milioni 20, huku Okwi akipata Sh milioni 5. Simba ilimuuliza Etoile du Sahel kwa dola 300 (Wakati huo zikiwa ni Sh mil 480).

Wakati Simba haikupata kitu, Okwi alilamba dola 100,000 (Sh milioni 160 wakati huo) kulingana na makubaliano. Simba ikaambulia patupu.

Baadaye Yanga ikatoa Sh milioni 160 kumsajili Okwi ikidai imemtoa SC Villa ingawa hali halisi alikuwa mchezaji wa Etoile. Okwi alilamba Sh milioni 100 ingawa hakumaliziwa na Yanga na mgogoro ndipo ulipoanzia hadi akatimkia Simba ambao walimpa mshahara mzuri wa dola 3,500 lakini hawakumlipa fedha za usajili.

Baada ya muda mchache walimpa miezi sita kufanya awe na mkataba wa mwaka mmoja, wakamlipa dola 20,000 (zaidi ya milioni 36 wakati huo). Simba wakaona itakuwa vizuri kumuongezea mwaka mzima tena, hilo likafanyika nao wakatoa dola 40,000 (zaidi ya Sh milioni 72) ingawa hadi anaondoka hakuwa amemaliziwa dola 5,000.

Simba imemuuza Sonderjyske kwa dola 110,000 (zaidi ya Sh milioni 220), naye amedaka chake. Hii inamfanya awe ameingiza zaidi ya Sh milioni 500 kwa upande wake.


Upande wa biashara kwa maana ya timu, biashara ya zaidi ya Sh bilioni 1.5 timu kwa timu imefanyika ingawa kuna fedha hazikulipwa kama zile alizotokea Simba kwenda Etoile.

Okwi ni mchezaji anayejua anafanya nini na huu ni mfano ambao unauona amegundua mambo mawili makuu katika maisha yake ya soka. Kutokana na kujiamini amekuwa akiyafanya.

Kwanza, Tanzania ni “Shamba la Bibi” hivyo ni rahisi kwake kuendelea kuchuma, wachezaji wa Kitanzania na viongozi wa Kitanzania wapo tu. Kwa wachezaji hakuna mwenye juhudi ya kufanya kazi ili apambane hapa nyumbani au nje naye aingize mamilioni kama ya Okwi.

Pili amegundua katika soka kuna fedha, pamoja na matatizo yake amekuwa akijituma kwa kila namna kuhakikisha anakuwa tegemeo katika timu, nyota kila anapokwenda. Usishangae ukaambiwa ametoka Denmark kurejea Tanzania, safari hii akiwa Azam FC ambao wanaweza kuwa tayari kutoka Sh milioni 300 kumsajili!


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic