July 15, 2015



Simba wamezinduka! Katika kile kinachoonekana Simba imepata uongozi makini, timu hiyo imeshtuka kutoka mikono kapa katika mauzo ya kiungo mshambuliaji wao, Emmanuel Okwi, aliyejiunga na Klabu ya Sonderjyske ya Dernmark na kuweka ngumu kuachia ITC yake ili kuwa mchezaji halali wa klabu hiyo.


Bado Simba wanakumbuka machungu ya kunyimwa kitita cha dola 300,000 kwa mauzo ya nyota huyo mwaka 2012, katika Klabu ya Etoile du Sahel ya Tunisia, wakati wa utawala wa Ismail Aden Rage, ambazo zimekuwa zikipigwa danadana hadi leo hii.

Hata hivyo, katika kuhakikisha hawarudii makosa, utawala mpya chini ya rais Evans Aveva, ulimuachia nyota huyo kwa masharti magumu na mojawapo ni kwamba ITC yake itatoka pindi watakapoleta malipo ya mchezaji huyo.

Habari zinaeleza kuwa, Simba watakunja kitita cha dola laki moja na kumi (110,000) ambazo ni zaidi ya Sh mil 200 kwa ajili ya mauzo ya staa huyo raia wa Uganda.

Mjumbe wa kamati ya utendaji ya klabu hiyo, Said Tully, alisema tayari makubaliano kuhusu malipo yamekamilika na wanatarajia kuingiziwa mkwanja wao ndani ya wiki hii.

“Kuna mchakato mrefu kidogo katika ulipaji, lakini tunashukuru kuwa tumekubaliana kwa kila kitu na ndani ya wiki hii tutapewa chetu. Hatuna shaka na malipo na bahati mbaya au nzuri, bado ITC yake haijatoka, maana ndiyo yalikuwa makubaliano ya pande mbili, kwamba ITC itatoka tu baada ya kukamilisha malipo ya kumuuza,” alisema Tully.

Aidha, amewatoa hofu mashabiki wa klabu hiyo kwa kusema kuwa hawana sababu ya kuumiza vichwa kuwaza nani mwenye kuziba pengo lake, kwa kuwa ndani ya timu hiyo kuna wachezaji wenye uwezo wa hali ya juu.


“Wapo wachezaji wenye uwezo wa kucheza nafasi yake, lakini pia ni changamoto kwa vijana wengine ambao watakuwa na ari ya kutaka kuwa kama Okwi ili waonekane na kupata maisha mazuri,” aliongeza Tully.

1 COMMENTS:

  1. Kweli haya mambo ya ajabu,miaka minne nyuma Okwi aliuzwa kwa dola 300,000;leo Okwi anauzwa kwa dola 110,000!?
    Hapa ni usanii wa viongozi wetu kutaka kujirudishia pesa zao za usajili tuu.Kiwango cha Okwi hiwezekani akauzwa kwa chini ya dola 300,000 kwasasa.Viongozi acheni ujanja wenu kama mliotumia kwa Singano!

    ReplyDelete

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic