July 17, 2015


Na Saleh Ally
LIGI Kuu Bara inatarajiwa kuanza Agosti 22, mwaka huu, safari hii ikiwa na timu 16. Hadi sasa bado ratiba haijatoka na imeelezwa Bodi ya Ligi Tanzania (TPLB) ndiyo wanaifanyia kazi!


Ratiba ya ligi kuu imekuwa sehemu kubwa ya matatizo yanayoyumbisha soka nchini, huenda kwa kuwa umakini umekuwa si asilimia kubwa na Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) imeshindwa kulithibitisha hilo.

TPLB inapaswa kujua ratiba inapokuwa na viraka rundo au figisufigisu, basi inaleta madhara rundo, pia inachangia kupunguza utamu wa ushindani na ladha ya wengi kutaka kushuhudia mechi za ligi. Kwa kuwa Bodi ya Ligi bado haijatoa ratiba hiyo, mambo haya matano kama yatafuatiliwa, basi yanaweza kusaidia kuwa na ratiba bora ambayo itazaa ligi bora.


Mapema:
Miezi miwili kabla ya ligi kuanza, klabu za Ligi Kuu England zimeshajua ratiba, zitacheza na nani na kipindi kipi.

Kwa Tanzania hilo limekuwa tatizo, lakini utaona timu zinazoshiriki tayari zimejulikana, viwanja vinajulikana. Hivyo hakuna sababu ya kuendelea na utaratibu huo wa zamani. Inapaswa kuanzia wiki ijayo ratiba iwe imetoka na timu zijipange mapema kabla ya kuanza safari za ligi hiyo.

Wakati mwingine, inakuwa rahisi timu kupata hata wadhamini wa kusaidia safari zao kwa kuwa tayari mapema zinajua tarehe ipi zitakwenda wapi.


Biashara:
Hakuna ujanja, wahusika lazima wakubali yote yanafanyika lakini ili kuzimudu gharama za uendeshaji wa timu na klabu kwa jumla lazima faida ipatikane.
Inawezekana udogo wa timu ukachangia timu kutoingiza faida kubwa lakini upangwaji wa ratiba ukiwa wa kitaalamu, una nafasi ya kupunguza gharama kwa timu husika.

Mfano timu inayotoka Mbeya kwenda Tanga, inapofika ni vizuri ikacheza mechi mbili kwa kuwa pale kuna timu tatu. Inawezekana pia isiwe vizuri kuipa nafasi ya kucheza mechi tatu pale Tanga, nayo itakuwa si nzuri kwa kuwa itaondoa hamu ya mashabiki kuiona timu hiyo mara tatu mfululizo.

Angalau mechi mbili, mechi nyingine itarejea mzunguko ujao. Kikubwa ni kuziweka timu katika mazingira mazuri ambayo yatasaidia upunguzaji wa gharama angalau zijimudu kwenye uendeshaji kwa asilimia mia, ikiwezekana zipate hata faida kidogo.


Mechi 2 wilaya moja:
Mara kadhaa katika mizunguko miwili iliyopita, zimekuwa zikichezwa mechi mbili siku moja. Tena zinachezwa katika wilaya moja ya Temeke, umbali wa kilomita chache kutoka uwanja mmoja kwenda mwingine.

Yanga inacheza na Mtibwa Sugar, Uwanja wa Taifa, halafu Stand inacheza na Ruvu JKT pale Azam Complex. Hii ni kuziua kabisa hizi timu nyingine. Kuna uwezekano wa ratiba ikapangwa vizuri, nazo zikapata mashabiki zaidi, maana bado hazijawa na nguvu kama ile ya Simba au Mtibwa Sugar. Pia vizuri kukumbuka Stand wamesafiri kutoka Shinyanga na wanahitaji fedha za geti kama kikuza mapato.

Muda:
Kuwa na timu 16 kusiifanye ligi ichezwe mechi nyingi zaidi katikati ya wiki. Mara nyingi watu wanashindwa kujitokeza katika mechi zinazochezwa katika kipindi hicho.

TPLB na TFF lazima wajue soka sasa ni biashara, hivyo ziangalie timu ambazo zinapaswa kucheza wikiendi kwa kuwa zitavuta watu wengi iwe uwanjani hata kwenye runinga.

Kupeleka mambo harakaharaka yaishe tu haitakuwa sawasawa. Maslahi ni sehemu ya kutengeneza ligi bora kwa kuwa timu zinapopata fedha nyingi, zinakuwa imara na kuongeza ushindani.

Kuahirishwa:
Huu ni ugonjwa mkubwa sana, TPLB na TFF kama wanataka mapinduzi, huu ndiyo wakati mwafaka wa kuhakikisha wanaanza kupambana na jambo hili, kuahirishwa kwa mechi za ligi bila sababu zisizokuwa na msingi hata kidogo.

Tabia ya kuahirisha mechi hovyo inazua hisia rundo na nyingine zinakuwa na mwelekeo wa ukweli, kwamba kuna timu inajengewa mazingira mazuri ili iwe na nafasi ya kuwa bingwa.

Lakini ni gharama kubwa. Tumeona msimu uliopita, timu zilishafika kwenye kituo na bado mechi zikaahirishwa. Hii ilisababisha zitumie fedha zaidi, jambo ambalo si sahihi.

TPLB na TFF hawawezi kuingia hasara yoyote na wanajua timu husika lazima itasubiri. Lakini si sahihi, zinapaswa kujua timu zinapocheza, ndiyo TFF na TPLB zinatambulika na kuweza kujiendesha. Hivyo lazima zijenge utamaduni wa kuzisaidia klabu, angalau kwa kuwa na mpangilio mzuri utakaowezesha kuzipunguzia gharama zisizo rasmi.



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic