July 17, 2015


Na Saleh Ally
KUNA mjadala mkubwa sana kuhusiana na suala la ushirikina michezoni na hasa kwenye soka. Kwamba kila timu imekuwa ni lazima iende kwa mganga kwa ajili ya ushirikina ili iweze kushinda.


Hili linafanyika hadi katika timu za mchangani, jambo ambalo mara zote nimekuwa nikilikemea na kuliita miradi ya wajanja wachache.

Najiuliza mara kadhaa, kwamba vipi timu zinaamini suala la ushirikina ni lazima? Kwani hakuna ambaye amewahi kulijengea hoja za msingi kwamba si lazima lifanyike na kuna mara kadhaa halikufanyika na timu zikashinda?

Niliwahi kuvuliwa unahodha nikiwa nacheza madaraja ya chini, kisa nilikataa kushiriki kwenda kwa mganga. Mwisho timu ikafungwa mabao 4-2. Mechi iliyofuata, hatukwenda kwa mganga, tukashinda. Ndiyo maana naona ushirikina, ni miradi ya watu fulani.

Nilishtushwa baada ya hivi karibuni kuzagaa mitandaoni kwa picha za video zikiwaonyesha wachezaji wa Coastal Union wakiwa ufukweni wakishiriki masuala ya ushirikina.
Wachezaji hao, wengine maarufu walionekana kwa sura zao waziwazi wakiwa wametulia na mganga yuko katikati yao akifanya kazi ya kuzika kitu, sijui ni kiumbe au tunguri!

Baadhi yao wanasisitiza, “zika zika”. Kuonyesha kwamba ni jambo walilolizoea. Mganga naye anafanya kazi yake huku wachezaji hao wakiendelea na stori za kawaida. Ajabu zaidi, wachezaji hao wamevaa jezi za rangi nyekundu na nyeupe ambazo huvaliwa na Coastal Union, tena wakiwa na furaha tele!
Kwanza ikanishtua, kumbe kwa mganga wachezaji wanatakiwa kuvaa sare kama wanakwenda uwanjani au wako safarini! Swali langu la msingi likawa hivi, sasa mbona wachezaji nao hawakatai kwenda kwa mganga?

Inawezekana pia wanapenda? Au wanaamini masuala hayo ndiyo maana nao wanaingia kwenye kashfa hizo za ushirikina, maarufu kama “kupigana” misumari?

Swali lililofuata, kama Coastal Union wanakwenda kwa mganga namna hiyo, iweje Ligi Kuu Bara msimu uliopita iliisha wakipigania kuokoka kuteremka daraja? Mganga wao hakuwa mkali, hivyo msimu ujao watabadilisha?

Najua Yanga, Simba na timu nyingine za ligi kuu zinakwenda kwa waganga lakini kuna kila sababu watu walio timamu kiakili waamke na kuanza kupambana na tabia hizi za kizamani ambazo zinatufanya tuendelee kubaki tulipo.

Mafanikio makubwa ya soka yako Ulaya, hatusikii suala la waganga au uchawi ili watu washinde au kufanya vizuri badala yake wanapambana vilivyo kuhakikisha kinachofanyika kinakuwa kina uwezo.

Mazoezi ya kutosha, malipo mazuri, matunzo kwa wachezaji, vifaa bora vya maandalizi na baada ya hapo ni juhudi na maarifa.

Tabia ya kuabudu ushirikina ni kujikwamisha na haina maana yoyote katika ushindi. Najua kama timu ikifungwa, mganga atawaambia hamkufuata masharti yake, ambalo ni jibu rahisi na la kipuuzi kabisa.
Sasa wachezaji mbona hamuachi kwenda kwa waganga kama mnaamini uwezo wenu na maandalizi mliyofanya ya kutosha? Si sahihi na aibu kubwa wachezaji wakubwa kwenda kwa waganga mkiwa mnaonyesha kiasi gani imani zenu haziendani na wachezaji mnaotaka kuwa kama wao, yaani kina Cristiano Ronaldo, Lionel Messi, Paul Pogba na wengine.

Katika klabu karibu zote kongwe, kuna ujanja unafanyika wa watu kusingizia kuwa waganga ni msaada. Kumbe ni miradi ya baadhi ya wanachama ambao wamekuwa wakipewa fedha kila mechi kwenda kwa waganga.
Kama ni hivyo, basi timu ziache kufanya mazoezi halafu waganga waamue matokeo. Au ziachane na kununua wachezaji wazuri ili kutoa nafasi kwa waganga kufanya kazi ili zipate ushindi na mafanikio.

Video ya Coastal Union wakiwa kwa mganga inaonyesha kiasi gani safari ndefu iliyo mbele ya mchezo wa soka hapa nyumbani. Lazima tubadilike, tupite njia sahihi wanayopita wenzetu. Huku sasa imetosha.



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic