August 19, 2015


Na Saleh Ally
NIMEKUWA nikizungumzia sana kuhusiana na suala la Simba kulipwa zile fedha dola 300,000 (sasa Sh milioni 600), walizomuuza mshambuliaji Mganda Emmanuel Okwi kwa Etoile du Sahel ya Tunisia.


Nirudie leo kwenye kukumbusha kwamba, biashara ya kumuuza Okwi kutoka Simba kwenda Etoile ilikuwa ni ya kisanii, haikuwa ya kitaalamu, waliohusika pia hawakuwa watu makini hata kidogo.

Nimekuwa nikisisitiza hilo tangu siku ya kwanza biashara ilipofanyika, nikaeleza inaonyesha wazi kuna mianya mingi ya Waarabu hao kutolipa fedha hizo.

Lakini nilisisitiza tena baada ya Okwi kurejea nchini na kuanza kuichezea Yanga. Bahati nzuri Etoile ikaja nchini kucheza na Yanga, nikafanya mahojiano na bosi wa Etoile pamoja na Shirikisho la Soka Tunisia (FTF).

Matamshi yao, yalionyesha wazi hakukuwa na mpango wa kulipa fedha hizo, mmoja alisema: “Simba wanataka fedha ya nini wakati Okwi yuko hapa anaichezea Simba?” Pia nikalieleza hilo.


Inawezekana Simba ikalipwa kwa kuwa imelifikisha suala hilo kwenye Shirikisho la Soka la Kimataifa (Fifa), tukaelezwa limetoa agizo kuwa wawalipe Simba haraka. Hadi leo bado, sijajua haraka inachukua kipindi gani.

Jaribu kuangalia hili, Simba ilimrejesha Okwi akitokea Yanga. Pamoja na tafrani zilizotokea, alifanikiwa kubaki Msimbazi na kuitumikia kwa ufanisi mkubwa kwa msimu mmoja.

Baada ya hapo, kupitia makubaliano ya kila upande, Simba ikamuuza Okwi Denmark katika Klabu ya Sonderjyske kwa Sh milioni 120, safari hii hakukuwa na longolongo.

Kwanza baada ya Wazungu hao wa Ulaya Kaskazini kuweka ahadi, Simba waliendelea kubaki na haki za mchezaji huyo kwa maana ya uhamisho na malipo yalipofanyika, Okwi akawa huru kuitumikia timu yake mpya.

Kidogo hapa unaona tofauti kubwa kati ya biashara ile ya kwanza na hii. Simba walibaki na haki za Okwi, kwamba hawakufanya uhamisho wa kimataifa wakisubiri kulipwa. Lakini mauzo kwenda Etoile, aliyekuwa Mwenyekiti wa Simba, Ismail Aden Rage, alisisitiza uhamisho ufanyike tu.


Nikaibuka nikasema Simba imemuuza Okwi ‘bure’ na hilo ndilo linaloendelea kuthibitika hadi leo, licha ya ubishi mwingi na kuzuka kwa makundi kwamba namsakama Rage.

Nilitamani sana Simba ilipwe ili Simba na wale waliokuwa mashabiki wa uongozi uliopita walioutetea kwa kufanya upuuzi huo katika mauzo, waweze kunisema. Lakini binafsi ningenyamaza kimya na kujipongeza kwa kuanzisha presha iliyochangia wao kuchangamka na kufanikisha malipo.

Lakini sasa bado roho inaniuma kuona klabu kutoka katika nchi niliyozaliwa na kukulia inadhulumiwa fedha Sh milioni 600, tena kijinga kabisa huku sababu zisizo na mashiko zikitolewa kutaka kuwalainisha Wanasimba.

Inavyokwenda, Simba watafikia watakaa kimya tu na kuachana na fedha hizo zipotee. Ni ahadi inayorudi nyuma badala ya kwenda mbele.
Badala ya kutumia kanda kusikiliza muziki huo, sasa tutoke kwenye kanda hizo maarufu kama kaseti na twende kwenye CD.



Fedha zile si za Rage, si za Zacharia Hans Poppe, si za Saleh Ally ni za Wanasimba. Usisahau wenye fedha hizo ni Watanzania na ndiyo maana ninakuwa nina haki ya kuhoji na nitaendelea kutumia ujinga huu wa Simba kama sehemu ya mfano katika muda wangu wote wa maisha ya uandishi wa habari.

Nitawakumbusha viongozi wengine kutorudia upungufu mkubwa wa umakini uliofanywa na Rage halafu baadaye wakajaribu kuutetea na kutaka kulazimisha ionekane kama wanadharauliwa au kuonewa ili wapate watu wasio waelewa waweze kuwatetea ili nionekane sina nidhamu kudharau wakubwa. Nasisitiza, kuna kila sababu ya kutofautisha kuelezana ukweli na heshima, sijawahi kumdharau mtu.

Rage kaboronga, sasa wote tukae kimya au tuunge mkono alichokifanya? Ukweli hauna mwenyewe, ukimwagwa kwenye mchanga, kamwe haukauki na hilo ndilo linaloendelea kubaki.

Usisahau Simba imetumia fedha nyingi sana ikiwa ni juhudi ya kutaka kulipwa fedha hizo. Gharama zimekwenda juu sababu tu ya umakini uliokosekana siku ya mauzo.


Niongeze kidogo, inapofikia suala la hoja za msingi, basi tuache ushabiki. Hata kama utakuwa na urafiki na aliyekosea, basi msaidie kwa kumueleza ukweli, upambe si jambo jema katika maisha ya mwanadamu imara.

Simba inaendelea kudai fedha za Okwi katika biashara ya miaka mitatu iliyopita, wakati tayari imeshalipwa kwenye biashara ya Okwi ya mwaka huu, kichekesho!

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic