August 12, 2015


Kocha Mkuu wa Simba, Muingereza, Dylan Kerr, amesema anahitaji wachezaji wake kucheza soka la pasi za harakaharaka wanapokuwa na mpira wakati wanashambulia lango la timu pinzani.


Kauli hiyo aliitoa mara baada ya kumalizika kwa mechi ya kirafiki ya kimataifa dhidi ya SC Villa iliyochezwa kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam wikiendi iliyopita na  Simba kushinda kwa bao 1-0.

Hiyo ni mechi ya sita kocha huyo kukaa kwenye benchi la Simba tangu apewa kibarua cha kukinoa kikosi hicho kinachojiandaa na Ligi Kuu Bara.

Soka hilo la pasi za haraka haraka wakati timu ikiwa na mpira, linatumiwa sana na klabu ya Barcelona ya nchini Hispania.
Kerr amesema bado kikosi chake kinahitaji marekebisho kabla ya kuanza kwa ligi kuu, yakiwemo ya kucheza soka la kupiga pasi za haraka wanapomiliki mpira.

Kerr alisema tatizo hilo la timu yake kutocheza soka la pasi za haraka, ameliona kwenye mechi tano za kirafiki walizozicheza ikiwemo dhidi ya KMKM, Polisi Zanzibar na Taifa Jang’ombe, zote za kirafiki.

“Bado wachezaji wangu hawajaushika mfumo ninaoutaka wa kucheza soka la pasi za haraka wakati tukiwa na mpira sisi tukishambulia kwenye goli la timu pinzani.

“Hivyo nimepanga kulifanyia kazi hilo kuhakikisha timu inacheza soka lile ninalolihitaji ambalo ninaamini kama wachezaji wangu wakilizoea, basi timu yangu itapata ushindi.


“Kwa mfano mechi hii dhidi ya SC Villa ya Uganda tulivyocheza utaona wachezaji wangu walikuwa wanakaa na mpira muda mrefu bila ya kupigiana pasi kwa wakati, hivyo ninataka kuona timu yangu inacheza soka la aina hiyo,” alisema Kerr.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic