August 14, 2015


MGOSI AKITAMBULISHWA SIMBA DAY...

Na Saleh Ally
SIKU chache tu baada ya Simba kucheza mechi ya kirafiki na kuibuka na ushindi wa bao 1-0 katika Simba Day, mshambuliaji wake, Mussa Hassan Mgosi aliisaidia timu ya Faru Jeuri kuibuka na ushindi katika michuano ya Ndondo Cup.


Mgosi alikwenda Faru Jeuri kama timu yake ya ‘kulipwa’ ambayo amekuwa akiipa kampani katika michuano hiyo maarufu ya Ndondo Cup.

Mgosi aliichezea timu hiyo ikiwa ni siku chache tu baada ya kukabidhiwa unahodha wa Simba, jambo ambalo niliona ulikuwa uamuzi sahihi.

Niliwahi kueleza namna nilivyoshangazwa na uamuzi wa uongozi wa Simba kukubali Hassan Isihaka awe nahodha wa Simba kutokana udogo wake katika soka, alishindwa hata kujieleza.

Haikuwa sawasawa kuona nahodha wa Mbeya City, timu changa akijieleza vizuri kabisa, halafu nahodha wa timu kubwa na kongwe akishindwa hata kujieleza mbele ya waandishi wa habari.
 
MGOSI AKIPAMBANA DHIDI YA SC VILLA...
Hivyo uamuzi wa kumpa Mgosi ambaye ninaamini kama ni miaka mingi na Simba huenda ikawa miwili au mitatu. Ukongwe wake unaweza ukawa njia ya busara kuwasaidia wakongwe wenzake pamoja na vijana, kuifanya Simba iende katika njia sahihi.

Lakini niliona si sahihi kwa mara nyingine, Mgosi kuiba gharama za maandalizi ya Simba ya kambi ya Lushoto na Zanzibar na kuitumia katika michuano ya Ndondo Cup huku akijua si sahihi.

Pia niliona haikuwa sawa, Mgosi kujiingiza katika hatari kubwa ya kuumia wakati akijua maandalizi wanayofanya Simba wanategemea kumuona akiwa msaada kwenye ligi mwezi ujao.

Tunajua mchangani ushindani ulivyo, tunaelewa ulinzi kwa maana ya ule unaotolewa kwa waamuzi ni tofauti angalau na ligi kuu.

Anayecheza ndondo, haoni shida kumuumiza mchezaji fulani iwe hata kwa makusudi kwa kuwa sidhani kama kuna kanuni kali za faini au kufungiwa.
 
MGOSI AKIWA KATIKA MECHI YA MICHUANO YA NDONDO CUP....
Kama Mgosi ataumia kwenye Ndondo Cup wakati yeye ni ‘mali’ ya Simba ambayo inamlipa mshahara na posho zote, pia inaingia gharama kubwa kumuandaa, pia si sahihi.

Makala haya yanaweza kuzua mjadala mkubwa, kwani wachezaji maarufu wanapokwenda kwenye Ndondo Cup, ndiyo wanaongeza utamu wa mashindano hayo. Mimi pia kama shabiki au mpenda soka ningependa kuona hivyo.

Lakini unaangalia kwa maana ya maendeleo tunayoyataka kwenda katika kiwango cha kuonekana tunafanana na soka la kulipwa, halafu hayo yanayofanyika mfano kwa Mgosi au wenzake, tutafika huko?

Huenda wakati wa mapumziko aliopewa na Simba angeweza kupumzika na kufanya mazoezi lakini si kujisogeza kwenye hatari kwa kuwa mechi na mazoezi ni mambo mawili tofauti hata kokote mtu anaweza kuumia. Si vizuri kuifanya bahati mbaya ikawa malengo!

Mgosi ni mshikaji wangu, huenda tunaweza kuzungumza kando lakini kwa faida ya soka ya hapa nyumbani lazima tuliweke hili wazi kwa maana ya mkongwe kama Mgosi anapaswa kuwa wa kwanza kutambua kuwa huu kwake si wakati wa kucheza mashindano ya mchangani nje ya Simba katika kipindi ambacho wako kwenye mapambano ya kuifanya Simba iwe imara, irudi katika hadhi yake na yeye ni kati ya tegemeo.

Kamwe siidharau hiyo michuano ya Ndondo Cup au mingine ya mchangani kwa kuwa pia nimecheza sana, lakini jiulize swali hili rahisi. Kama Mgosi akiumia, unafikiri Faru Jeuri wanaweza kuchukua gharama za kumpa matibabu sahihi? Huo mzigo utarudi kwa Simba tena ambayo imegharimika kumuandaa.

Inawezekana Faru Jeuri nao wanalipa vizuri, au ni mapenzi ya Mgosi kutokana na masela wake wengi kuwa pande hizo, lakini ifikie wakati yeye aelewe, awe wazi kwao na hao masela wamuelewe kuwa si sahihi kufanya hivyo katika kipindi hiki. Akikataa asionekane kama anaringa, waangalie hali halisi.

Mgosi anapaswa kuwa wazi au mkweli kwao, kama kweli anaipenda aionee huruma namna inavyogharimika kwake na aipe heshima yake na baada ya ligi, basi huenda atakuwa na nafasi ya kucheza michuano hiyo.


Bado Mgosi ni kati ya washambuliaji wa kuigwa hapa nyumbani. Kama ni hivyo anapaswa kuwa mfano uwanjani, lakini pia fikra tafakuri zake zinakuwaje hata nje ya uwanja! Acha hoja ianze.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic