August 14, 2015


Na Saleh Ally
KAMPUNI ya simu za mikononi ya Vodacom imekubali kuingia mkataba wa miaka mitatu mingine kuendelea kudhamini Ligi Kuu ya Tanzania Bara.


Kwa maana ya kuhakikisha mambo yanakwenda vizuri, lazima kuwashukuru Vodacom hata kama wao pia wanafaidika kwa kiasi kikubwa. Kamwe hawawezi kusema mambo hayaendi vizuri.

Lazima wanapata faida ya kujitangaza kwa kuwa soka ni mchezo wenye nguvu hapa nyumbani lakini lazima tukubali hata wangeacha kudhamini, bado wasingepata hasara.

Mkataba wao mpya wa miaka mitatu, wameongeza hadi Sh bilioni 6.9, maana yake itakuwa ni Sh bilioni 2.3 kila mwaka wanazotoa kwenye udhamini wao.

Hongera tena kwa kuwa wameongeza fungu, awali ilikuwa ni Sh bilioni 4.8 sawa na Sh bilioni 1.6 kwa mwaka. Maana yake safari hii si haba ingawa bado ninaweza kukosoa katika mkataba huo.


Kwamba vipengele kadhaa vimeboreshwa, lakini lile muhimu la zawadi limeachwa vile vile. Fedha za zawadi kwa jumla zinabaki kuwa Sh milioni 174 huku tuzo za kila mwezi zikitolewa kila mara.

Kwa kiasi fulani wamejitutumua, lakini bado walikuwa na nafasi ya kuongeza hata Sh milioni 50 kwenye fungu la zawadi kwa kuwa ni changamoto ya kufanya mashindano ya ligi hiyo kuzidi kuwa juu zaidi.

Zawadi inapozidi kuwa nono, inajenga hamasa ya juu kwa wanaoshinda, hali inayochangia ushindani kuwa juu na watu kuwa tayari kufanya vizuri zaidi.

Wakati yote yanafanyika, Vodacom imeamua kuwekeza zaidi katika suala la nauli za timu ikizingatia timu mbili zimeongezeka kutoka 14 hadi 16.

Lengo ni kuhakikisha kila timu inafika kwenye kituo kwa wakati mwafaka na kuepusha kisingizio kingine.

Hilo ni sehemu ya jambo zuri, lakini tunajua kwamba timu nyingi zina vyanzo vingi vinavyoweza kuwasaidia kufika sehemu husika na fedha zilizotolewa zikabaki.

Angalia timu zenye mabasi, zinaweza kufika vituoni kwa kutumia fedha nusu ya zile zinazotolewa na Vodacom.

Hofu yangu ni kwamba, baada ya Vodacom kuongeza fungu kwenye fedha hizo za nauli, hazipaswi kuwa sherehe kwa viongozi wasio waadilifu kwa klabu zao. Najua mtapinga lakini ukweli viongozi wengi wa klabu kubwa na ndogo ni wezi.

Wamekuwa wakizitumia klabu kama sehemu ya kuendeshea maisha yao, ingawa wanajificha kwenye mwamvuli wa mapenzi. Kwamba wanazipenda sana klabu hizo na wanateseka kutokana na mapenzi yao kwa klabu zao, hakuna lolote.

Mapenzi halafu ulale njaa, mapenzi halafu ushindwe kuhudumia familia yako. Ubaki tu pale klabu ukiihudumia klabu, acheni kuwafanya watu hawana akili vichwani mwao.

Kama fedha za safari zimeongezwa, basi ni wakati mwafaka hata kama zitatumika katika kipengele kingine, basi kiwe kwa ajili ya kuboresha huduma za wachezaji wa timu hizo za Ligi Kuu Bara.

Kama wachezaji walikuwa kila wanapofika kambini hasa mikoani wanalala kwenye hoteli za kubahatisha na wakakubali kwa kuwa wanajua timu haiko vizuri kifedha, basi sasa ni wakati wa kuwaonyesha mapenzi.

Kwamba walivumilia katika kipindi kigumu na sasa ni kipindi cha nafuu. Hivyo wanaweza kuishi kwa hali nzuri zaidi.

Ikiwezekana fedha hizo zinawea kutumika kama sehemu ya motisha ili wachezaji wa timu husika wapige soka kwa moyo wa kujiamini zaidi.

Fedha hizo zisiingie kwenye mchezo wa viongozi kuanza kufanya sherehe wakiamini sasa ndiyo neema kwao, wachezaji waumie uwanjani mwisho fedha ziingie matumboni mwa viongozi wajanjawajanja.

Kweli kama viongozi, mnapambana sana lakini lazima mkubali ndiyo kazi yenu na ufahari au mafanikio kwa kiongozi bora, pia ni kuongoza watu ambao wana amani ya mioyo yao na kufanya kila linalowezekana kuwasaidia kufanya kazi yao vizuri.


Ongezeko hilo la Vodacom, liwe na faida kwa wachezaji na huenda hamasa itaonekana kwa wachezaji hali itakayosaidia mechi kuwa ngumu zaidi na kuamsha ushindani zaidi katika Ligi Kuu Bara.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic