August 28, 2015


Kiungo Mzimbabwe wa Yanga, Thabani Kamusoko ameonyesha kweli ni makini na kazi yake baada ya kwenda kuishuhudia Simba ikicheza mechi ya kirafiki.

Kamusoko ambaye ni kiungo mchezeshaji mwenye uwezo mkubwa wa kupiga pasi za uhakika, alipewa ruhusa na klabu yake ya Yanga kwenda kwao kuichezea timu ya taifa lakini alilazimika kubaki nchini, kisa kikiwa ni Simba.

Kiungo huyo aliamua hivyo baada ya kusikia habari za Simba na kuambiwa ni wapinzani wa jadi wa Yanga na ndiyo ambao wamekuwa wakitoa upinzani mkali, hivyo baada ya kupewa ruhusa Jumapili iliyopita, akaamua kuipotezea na kubaki Dar es Salaam ili aione Simba ikicheza katika mechi ya kirafiki dhidi ya Mwadui FC kwenye Uwanja wa Taifa.

Kiungo huyo mwenye rasta, alisaini mkataba wa miaka miwili kuichezea Yanga hivi karibuni akitokea FC Platinum ya Zimbabwe aliyokuwa anaichezea Donald Ngoma, aliiona Simba kisha akatoa neno juu ya timu hiyo.

Kamusoko alifika uwanjani hapo saa 9:30 alasiri akiwa ameongozana na Meneja wa Yanga, Hafidh Saleh, ambapo alikaa uwanjani hapo kwa dakika zote 90 huku akionekana kuwa makini kufuatilia kila hatua ya mchezo huo.

“Nilipanga kurudi nyumbani kujiunga na timu ya taifa mara baada ya mechi ya Ngao ya Jamii, lakini niliamua kubaki kuwaona Simba mara baada ya kupata taarifa kuwa wanacheza mechi ya kirafiki.

“Sikuwa nimewahi kuwaona Simba wakiwa wanacheza, unajua lazima niwajue wachezaji wao wenye madhara, pia aina yao ya uchezaji wanayoitumia.

“Nimewaona na nisingependa kuzungumzia chochote juu ya Simba ni mapema sana, lakini nikuhakikishie kuwa nitaizungumzia Simba siku tutakayocheza nayo,” alisema Kamusoko.

Kamusoko alicheza nafasi ya kiungo mshambuliaji katika mechi ya Ngao ya Jamii dhidi ya Azam, Agosti 22, 2015 huku Haruna Niyonzima ambaye amekuwa akicheza nafasi hiyo akianzia benchi.

Mara baada ya mechi hiyo, Kocha wa Yanga, Hans van Der Pluijm, alisifia kiwango cha mchezaji huyo ambapo alisema anaweza kumtumia kama kiungo mkabaji pia.


Simba na Yanga zinatarajiwa kukutana Septemba 26, 2015 katika raundi ya kwanza ya Ligi Kuu Bara.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic