September 5, 2015



Na Saleh Ally
UTURUKI ni moja ya nchi zenye historia ya kuvutia katika soka duniani na kama unaitaja, klabu mbili kubwa za Galatasaray na Fenerbahce ndizo nembo kutokana na ukongwe na ubora wake.


Kuna timu nyingine kama Besiktas na Antalya Spor lakini haziwezi kuwa na rekodi au historia ndefu kama timu hizo mbili kongwe.

Galatasaray ndiyo kongwe zaidi, ilianzishwa Oktoba 30, 1905, bado siku chache ikamilishe miaka 110. Fenerbahce ilianzishwa mwaka 1907, ina umri wa miaka 108.

Klabu hizo ni kongwe, nimeanza kutaja umri kuonyesha kweli ni kongwe na tunaweza kujifunza kupitia zenyewe.


Ndiyo maana nilipokuwa nchini Uturuki nilifanya juu chini kuhakikisha ninafanya ziara katika makao makuu ya klabu zote mbili, pia nikatembelea viwanja vyao vya nyumbani.

Galatasaray inatumia Uwanja wa Turk Telecom Arena wenye uwezo wa kubeba watu 52,652 na Fenerbahce nyumbani ni kwenye Uwanja wa Sukru Saracoglu unaochukua watu 53,715 walioketi.


Saracoglu ni jina la moja wa viongozi wake mashujaa waliowahi kuiongoza klabu hiyo na kuleta mapinduzi makubwa ya kimaendeleo akiwa madarakani kwa miaka 16, pia alikuwa mmoja wa mawaziri wa serikali ya Uturuki.

Wakati nikiwa katika ziara ya makao makuu ya klabu hizo niligundua mambo mengi sana ya kujifunza. Huenda baadhi nitarudia kama nilivyofanya wakati nilipotembelea viwanja na makao makuu ya klabu za Ujerumani za Bayern Munich na Borussia Dortmund.


Nikiwa pale, niliwakumbuka Yanga na Simba, klabu kongwe za Tanzania ambazo hazina viongozi wabunifu hata kidogo.



Viongozi ambao wanafanya kama walivyofanya viongozi wa miaka kibao nyuma. Ni kusajili na kuiandalia timu kambi, baada ya hapo ni ligi, kazi imeisha. Wanachosubiri ni ushindi washerekee, au wapoteze walaumiane.


Fenerbahce:
Uwanja na ofisi zao ziko upande wa Bara la Asia ingawa ni katika Jiji moja la Istanbul.

Uturuki ni nchi moja iliyo katika mabara mawili ya Asia na Ulaya, vivyo hivyo Jiji la Istanbul ambalo lina watu milioni 14 kwa mujibu wa sensa ya Desemba 2014.

Unapofika kwenye Uwanja wa Sukru Saracoglu, mandhari ni bora na kwa kuwa niliwasili pale saa 4 asubuhi, Robin van Persie, Nani, Diego na wengine walikuwa mazoezini. Ulinzi ni wa kutosha katika eneo hilo.


Baada ya matembezi ya sehemu mbalimbali, niligundua mambo mengi mfano kumbukumbu za kutosha za klabu huyo.

Kwenye nyumba ya makumbusho kuna makombe, jezi za zamani zilizochezewa mechi. Jezi za mashujaa wao.

Kuna vikombe zaidi ya 160 ambavyo timu hiyo ilicheza na kuvibeba katika michuano mbalimbali ya Ulaya na ndani ya nchi hiyo. Ngao za Jamii pia medali.

Pamoja na makombe, wamekumbuka kuweka sanamu kadhaa, mfano sanamu tatu zinazowaonyesha watu wakifanya kikao. Hicho ndiyo kilikuwa kikao cha kwanza kilichoizaa klabu hiyo.

Picha za viongozi wa klabu hiyo, kuanzia mwaka 1907 hadi sasa. Huku zikiwa zimetengenezewa sehemu maalum ya viongozi.

 Ukitoka hatua chache kidogo unaingia kwenye duka ambalo linauza vifaa mbalimbali kama jezi, fulana, mabegi, makoti, saa na bidhaa nyingine mbalimbali.

Hata kukiwa hakuna mechi, Fenerbahce imeajiri wafanyakazi 107 kama utazungumzia madereva, wafagizi, wahasibu, watendaji na wengine wengi.


Duka lake la vifaa huweza kuingiza hadi dola 2,100 (Sh milioni 4) kwa siku au zaidi kama si siku ya mechi. Katika siku ya mechi, huingiza hadi dola 15,000 (Sh milioni 30) kwa siku.

Galatasaray:
Huenda hii ni maarufu zaidi kwa hapa nyumbani Tanzania na imekuwa nembo ya Uturuki hasa ukizungumzia soka la nchi hiyo. Uwanja wake upo Istanbul pia lakini upande wa Bara la Ulaya.

Hakuna tofauti yoyote na Fenerbahce kutokana na hifadhi kubwa ya makombe pamoja na kuonyesha thamani kwa watu waliotoa mchango kwa maendeleo au uanzishwaji wa klabu hiyo.

Pia kuna duka lililopo klabuni. Lao linaonekana kuwa kubwa zaidi ya lile la wapizani wao ingawa kimapato wanaonekana hawana tofauti kubwa hata kidogo ila uwanja wake unaingiza watu wengi.

Duka la Galatasaray ni kubwa zaidi na ndani yake kunapatikana kila aina ya jezi na fulana za timu hiyo inayotumia rangi ya njano na damu ya mzee.

Pamoja na fulana na jezi, utaona kuna saa za mkononi na ukutani, vikombe, ‘makava’ ya simu na vibeba ufunguo.

Ami Sukru ambaye ni mmoja wa wasimamizi wa masuala ya waandishi na ulinzi pia katika klabu hiyo, anasema vitu kama vikombe, vibeba ufunguo, saa za ukutani, mezani na mkononi ndiyo zinazoingiza fedha nyingi zaidi.

Anaamini kwa mwezi klabu hiyo huingiza hadi dola 100,000 (zaidi ya Sh milioni 210) baada ya mauzo katika maduka mbalimbali ya Jiji la Istanbul.

Kawaida unapokwenda katika maduka makubwa mfano wa Mlimani City na Quality Centre, unakutana na maduka ya klabu hizo pia. Watu mbalimbali wenyeji na wageni wanaingia kupata huduma.

Mpangilio mzuri, utaona karibu kila sehemu yamegawanywa mara tatu. Sehemu ya wanaume, wanawake na watoto na wote wanapata bidhaa zao zikiwa katika nembo za klabu hiyo.

Biashara ni mtaji; Yanga na Simba wana mtaji mkubwa hata kama utakuwa si sawa na ule wa Galatasaray na Fenerbahce. Wanauza nini? Jezi zimewashinda, fulana hawawezi! Nguo za watoto hawajui. Je, hata vikombe, saa na vibeba ufunguo vinawashinda?

Kila anayeanzisha bishara anajiuliza mtaji atapataje na atauza wapi. Simba na Yanga zina uhakika wa kupata mtaji, hata zikikopa zina uhakika wa kurudisha kwa kuwa wanunuzi ambao ndiyo mtaji mkubwa au uhakika wa biashara wapo. Sasa mbona wanalala tu!


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic