October 15, 2015


Mwenyekiti wa zamani wa Simba ambaye pia alikuwa ni Mwenyekiti wa Chama cha Siasa cha National League for Democracy (NLD), mzee Emmanuel Makaidi, 74, amefariki dunia jana kwenye Hospitali ya Nyangao mkoani Lindi.


Kaimu mganga mkuu wa hospitali hiyo, Betram Makota, ameliambia Championi Ijumaa: “Mzee Makaidi aliletwa hapa akiwa amezimia, tukiwa katika harakati za kumtibu akafariki dunia.”

Mke wa marehemu, Modesta Makaidi, naye alisema: “Marehemu alikuwa akisumbuliwa na shinikizo la damu, alizidiwa na tulipompeleka hospitali akafariki dunia.”

Mzee Makaidi alikuwa mwenyekiti mwenza wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) na pia alikuwa Mgombea Ubunge wa Jimbo la Masasi kwa Tiketi ya NLD.

Licha ya kuwa mwanasiasa, Mzee Makaidi amewahi kushika nafasi kadhaa za uongozi katika Klabu ya Simba ambapo mwaka 1969 alikuwa katibu mwenezi, mwaka 1973 alikuwa katibu mkuu na mwaka 1983 alikaimu nafasi ya mwenyekiti akichukua nafasi ya Joachim Kimwaga.

Mwenyekiti wa zamani wa Simba, Hassan Dalali amesema: “Huyu ni Simba mwenzetu na amewahi kushika nafasi kadhaa za uongozi licha ya kuwa mwanasiasa, huu ni msiba wa Simba na wanamichezo wote nchini.”


Afisa Habari wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Tumaini Makene, aliliambia gazeti hili kuwa, mipango ya mazishi ingepangwa jana usiku kwa pamoja kati ya viongozi wa Ukawa na familia ya marehemu.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic