October 17, 2015


Na Saleh Ally
UKIZUNGUMZIA mchezo wa ngumi za kulipwa hapa nyumbani, hakuna ubishi bondia namba moja utamtaja Francis Cheka ambaye ndiye tegemeo kubwa kwa Watanzania wengi.


Cheka ambaye mama yake ni raia wa Msumbiji, amekuwa gumzo kutokana na kufanya vizuri katika mchezo huo tangu akiwa katika ngumi za ridhaa ingawa yeye analia kwa kusema pamoja na yote, bado ni masikini wa kutupwa.

Anasema amepigwa ngumi nyingi sana, lakini maisha yake yamekuwa na ahueni tu, kamwe hayalingani hata kidogo na sifa au ukubwa wa jina lake katika jamii.

Katika mahojiano na Cheka amesema amekuwa akiishi maisha ya shida sana tofauti na watu wengi wanavyofikiria, hali ambayo imekuwa ikimpa wazo la kuachana kabisa na mchezo wa ngumi.
 
CHEKA AKIWA NA SALEHJEMBE
SALEHJEMBE: Kwa nini unafikiri uache ngumi Cheka?
Cheka: Naumia sana ndugu yangu, najiona najitoa kwa ajili yangu, taifa langu lakini sina thamani na maisha yangu ni magumu sana.


SALEHJEMBE: Unafikiri ukiacha ngumi katika kipindi hiki utafanya kazi ipi?
Cheka: Nina kiwanda cha kusaga plastiki ambacho nilikinunua kwa Mhindi mmoja hivi. Ingawa nako ninapata shida kubwa sana kwa kuwa inahitajika Sh milioni mbili tu ili mambo yakae sawa, lakini siwezi kupata pia.

SALEHJEMBE: Ungeweza kwenda benki na kukopa ili uendeleze biashara, umeshindwa hilo?
Cheka: Nimewahi kujaribu, lakini ikawa shida kubwa kwa kuwa kipato changu hakieleweki, nusura nyumba yangu iuzwe, mke wangu akaokoa jahazi.

SALEHJEMBE:Ilikuwa shilingi ngapi? Ulishindwa kulipa hadi wakachukua hatua hiyo?
Cheka: Nilikopa Sh milioni tano, ikawa imebaki Sh laki saba tu. Sikuwa nimeshindwa, ila nilichelewesha rejesho kwa miezi mitatu. Halikuwa lengo langu, lakini kipato changu ni duni kabisa.

SALEHJEMBE:Wewe ni bondia mkubwa Cheka, unapocheza unalipwa fedha nyingi au matumizi yako hayana nidhamu?
Cheka: Unaweza kufikiri nalipwa fedha nyingi, lakini hapa nyumbani hakuna heshima hiyo maana mapromota hawatoi fedha nyingi, ingawa siwalaumu sana maana nao wanakosa wadhamini.

SALEHJEMBE: Kawaida unalipwa kama kiasi gani kwa pambano moja?
Cheka: Malipo yanatofautiana kulingana na pambano, lakini juu angalau Sh milioni tano. Usisahau kuna maandalizi, nalipia kambi, chakula pia ni lazima niwe na watu zaidi ya wawili. Maandalizi yanahitaji muda, angalau zaidi ya wiki mbili, tatu.
 
CHEKA ULINGONI AKIPAMBANA DHIDI YA MMAREKANI...
SALEHJEMBE:Je, unaweza kusema mchezo wa ngumi haujakusaidia kabisa?
Cheka: Kamwe siwezi kuinua mdomo na kusema hivyo, umenisaidia kwa mengi, umenikutanisha na marafiki wengi sana lakini naona jina linapaa kuliko mafanikio halisi.

SALEHJEMBE: Umewahi kupata gari baada ya kushinda pambano la ngumi, lakini sasa unatembea kwa miguu tu, vipi?
Cheka: Kweli, nilipata gari aina ya Toyota Corolla. Nililazimika kuliuza baada ya kuona baba yangu akiteseka kwa kuishi kwenye nyumba ya kupanga kule Kinondoni. Alikuwa na kiwanja Mbagala, nimejengea nyumba ya vyumba vitatu, angalau anaishi kwake.

Lakini bado sijaridhika, maana nyumba haiko katika hali nzuri, haina hata madirisha ndiyo napambana. Baba yangu ni masikini, hajiwezi na haoni, macho yake yamepoteza nuru, ni kipofu.


SALEHJEMBE: Taarifa zinasema umevuliwa mataji ya dunia, nini hasa tatizo?
Cheka: Kweli nimevuliwa ubingwa, taji la kwanza la WBF ambalo nilimpiga Mmarekani nilivuliwa kwa kuwa nilikwenda kupigana Urusi katika pambano lisilokuwa na ubingwa, nikapoteza.
Nimevuliwa mataji mengine matatu, jumla nimelipiwa mikanda minne bila kuitetea.

SALEHJEMBE:Kama ulijua kufanya vile, vipi ulikubali kwenda kupigana Urusi?
Cheka: Ndugu yangu, ndicho ninachokueleza, njaa. Nitaacha vipi fedha wakati nina nafasi ya kwenda kupigana? Hapa nyumbani pambano halijaandaliwa.


SALEHJEMBE: Mataji mengine pia umevuliwa, huoni kama ni tatizo kwako?
Cheka: Si tatizo, katika hii mikanda mingine miwili, sikuwa na pambano. Hakuna promota aliyejitokeza kuandaa na wenyewe wanalalamika hawana fedha za kutosha.

SALEHJEMBE:Hawana fedha za kuandaa mapambano, kivipi?
Cheka: Unajua pamoja na fedha zao za mfukoni, mapromota nao wanahitaji wadhamini. Nashangazwa sana na makampuni kudharau ngumi za kulipwa jambo ambalo si zuri, nafikiri wabadilike sasa. Mchezo wa ngumi unapendwa sana.


SALEHJEMBE: Unafikiri umeliletea taifa letu sifa kwa kiasi gani?
Cheka: Kama Cheka nimeleta heshima kubwa sana kwa juhudi zangu binafsi. Nimepigiwa wimbo wa taifa, usisahau nimewapiga mabondia kutoka Marekani, Azerbaijan, Malawi, Brazil na kwingine. Mimi ndiye bondia niliyepigiwa zaidi wimbo wa taifa.

SALEHJEMBE:Kuna taarifa ulipewa bati na mifuko ya saruji na serikali baada ya kutwaa ubingwa wa dunia, lakini ukaziuza. Kwa nini ulifanya hivyo?
Cheka: Ndugu yangu watu wazushi sana, hizo bati zilitakiwa kuwa 130, hadi sasa sikuwa nimepewa na hata siku ya tuzo za Taswa nilimkumbusha Rais (Jakaya) Kikwete kwamba bati zangu bado sijapewa.

Kweli Joel Bendera alinipa mifuko 80, pia nikapewa kiwanja. Mabati hadi sasa bado sijapewa, ninaamini Rais Kikwete atafanya hivyo.


SALEHJEMBE:Matarajio ya wengi, ilikuwa ni lazima utapigana pambano dhidi ya bondia wa nje. Umerudi kupigana na Thomas Mashali tena, hauoni kama unashuka?
Cheka: Nitafanyaje sasa, maana hakuna mapromota wanaoleta mapambano ya nje. Nimekuwa nikishinda karibu kila pambano, lakini sipati mapambo ya nje. Nitakachofanya ni kupambana nipate fedha ya kuendeleza kiwanda changu lakini namtwanga Mashali ili kulinda heshima yangu.

SOURCE: CHAMPIONI

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic