October 17, 2015


REKODI zinaonyesha Simba haijawahi kuifunga Mbeya City katika historia yake, pia Yanga haijawahi kuifunga Azam FC katika Ligi Kuu Bara ndani ya misimu miwili iliyopita.
Msimu wa 2013/14, Azam iliifunga Yanga mabao 3-2 halafu wakatoka sare ya bao 1-1, msimu uliopita mechi ya kwanza iliisha kwa sare ya mabao 2-2 halafu Yanga ikafungwa kwenye mvua mabao 2-1.

Nayo Simba msimu wa 2013/14 ilianza kwa kutoka sare ya mabao 2-2 na Mbeya City na ilipoenda Mbeya ikatoka sare tena ya bao 1-1, msimu uliopita Simba ilianza kwa kufungwa nyumbani mabao 2-1 na jijini Mbeya ililala mabao 2-0.

Makocha na wachezaji wa Simba na Yanga, hawataki tena masihara wameshtuka na leo Jumamosi wanataka timu zao kuvunja mwiko huo wa misimu miwili sasa.

Jijini Dar es Salaam kwenye Uwanja wa Taifa, Yanga itacheza na Azam na tayari Kocha wa Yanga, Hans van Der Pluijm amebadilisha vitu kadhaa kikosini ili apate ushindi.


Pluijm abadili kikosi makusudi
Kwa kujua kwamba Azam ina winga mwenye kasi Farid Mussa, Pluijm amepanga kumtumia Juma Abdul katika beki ya kulia badala ya Mbuyu Twite pia amewaingiza kikosi cha kwanza Malimi Busungu na Salum Telela kuendana na kasi ya Azam.

Mbali ya Twite wachezaji wengine walioondolewa kikosi cha kwanza ni Haruna Niyonzima na Simon Msuva, lengo ni kupata ushindi dhidi ya Azam, leo.

“Nimeshamaliza maandalizi yangu kwa mechi na Azam, hii si timu ndogo ni mechi iliyojaza ufundi na ushindani ni mkubwa hivyo kuna mabadiliko nimeyafanya nadhani yatatusaidia,” alisema Pluijm katika mazoezi ya mwisho jana asubuhi.

Hata hivyo, Azam kidogo imeonekana kuwa kimya kuelekea mchezo huo lakini Kocha Stewart Hall ambaye hataki mazoezi yake yahudhuriwe na mtu yeyote yule, alisema; “Tutapambana tukae kileleni.”

Wachezaji wawili wa Azam, Allan Wanga na Jean Baptiste Mugiraneza ‘Migi’ tayari wamerejea kutoka katika majukumu ya timu za taifa ili kuivaa Yanga. Wanga ametokea Kenya na Migi alikuwa Rwanda.


Vita ya pointi zaidi kileleni
Yanga na Azam, zote zina pointi 15 lakini Wanajangwani wapo kileleni kwa kuwa na mabao mengi ya kufunga ambayo ni 13 huku Azam ikiwa nayo tisa tu.

Pia Yanga imefungwa bao moja tu, wakati Azam imeruhusu mabao mawili. Mchezo wa Simba na Mbeya City wenyewe umebaki katika rekodi zaidi kwani Wekundu wa Msimbazi wapo nafasi ya tatu na pointi 12 huku wapinzani wao wakiwa wa 13 na pointi nne tu.

Simba nayo imekataa
Kocha wa Simba, Dylan Kerr na nahodha wake Mussa Mgosi kwa pamoja wamesema sasa ‘nooo!!’ wakimaanisha hawatakubali kukosa pointi ugenini kwenye Uwanja wa Sokoine.

“Tupo hapa kwa zaidi ya wiki sasa, hatutaki kupoteza mchezo huu japokuwa nasikia Simba haijawahi kushinda hapa, wapinzani wetu wana timu nzuri lakini nasi tutapambana kupata pointi,” alisema Kerr.
Kuelekea mchezo huo, kiungo wa zamani wa Simba, Haruna Moshi ‘Boban’ ametua rasmi katika kikosi cha Mbeya City kuitumikia kwa mujibu wa mkataba wake tangu awali.

Kwa upande wake, Mgosi alisema: “Najua Mbeya City wana Boban na Kaseja (Juma), hawa ni wazoefu lakini sipendezwi na rekodi ya Simba kutoifunga timu hii, tutajitahidi tushinde.”

Kuelekea mchezo huo, mashabiki wa Mbeya City waliweka ulinzi kwenye Uwanja wa Sokoine na kutoruhusu mtu yeyote kutazama mazoezi yao wakihofia kuibiwa mbinu zao.

Kocha wa Mbeya City anayekaimu nafasi ya Juma Mwambusi aliyeenda Yanga, Meja Mstaafu, Abdul Mingange alisema; “Naijua Simba inaishiwa na pumzi kipindi cha pili, nitawakamata hapohapo wala hakuna tabu, tuombe wachezaji wetu wawe wazima Jumamosi (leo).”

Viwanja vingine;
Leo Jumamosi, Majimaji itacheza na African Sports Uwanja wa Majimaji, Ndanda FC na Toto Africans Uwanja wa Nangwanda Sijaona, Mtwara, Stand United na Prisons Uwanja wa Kambarage Shinyanga na Tanga kwenye Uwanja wa Mkwakwani, Coastal Union itacheza na Mtibwa Sugar.
Kesho Jumapili, Mgambo Shooting itacheza na Kagera Sugar, Mkwakwani na Mwadui FC itacheza na JKT Ruvu Uwanja wa Mwadui Complex.


SOURCE: CHAMPIONI

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic