October 28, 2015


Na Saleh Ally
NIANZE na kukumbusha, Septemba 29, Yanga ilikuwa mgeni wa Simba kwenye Uwanja wa Taifa. Mechi hiyo ilimalizika kwa wenyeji kulala kwa mabao 2-0.


Halafu, Simba ilikuwa mgeni wa Mbeya City katika mechi iliyopigwa Oktoba 17 kwenye Uwanja wa Sokoine mjini Mbeya. Wageni wakaibuka na ushindi wa bao 1-0.

Tangu mechi ya Simba dhidi ya Yanga imechezwa, leo tayari ni siku 31, mwezi mmoja na siku moja.

Halafu tangu ichezwe mechi ya Simba ikiwa ugenini dhidi ya Mbeya City, leo zimetimia siku 11. Hadi Jumamosi, zitakuwa ni wiki mbili.

Hesabu zote hizi ni kwa ajili ya kutaka kukuonyesha kiasi gani Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) limeamua kukaa kimya kufumbia madhambi bila ya kujali muda unakwenda au la.

Nasema limefumbia macho madhambi tena ya wazi kwa kuwa karibu kila mpenda soka aliona matukio mabaya kabisa yaliyojitokeza ambayo ni taswira mbaya na isiyokuwa na manufaa kwa mpira wa Tanzania.

Katika mechi Simba dhidi ya Yanga, mshambuliaji Donald Ngoma raia wa Zimbabwe alimpiga kiwiko tena kibaya beki Hassan Kessy wa Simba ambaye alianguka na kutolewa nje kwa ajili ya kutibiwa.

Picha za video zipo zikionyesha Ngoma akifanya ujinga huo. Lakini ajabu TFF hadi sasa imekaa kimya na haionyeshi kuchukizwa na hali hiyo!

Hali kadhalika tukio la Mbeya ambalo nalo lipo katika picha za video, ikionekana wazi kabisa Juuko akimtwanga kiwiko mchezaji wa Mbeya City ambaye hakika katika hali ya kawaida, inaonekana aliumizwa!

Tayari nimeona Simba na Mbeya City kila upande umepeleka malalamiko TFF. Lakini ninachoona hakukuwa na sababu ya shirikisho hilo kusubiri malalamiko haya, kitu kibaya zaidi wameendelea kukaa kimya!

Suala la nahodha wa Coastal Union, Juma Nyosso kumdhalilisha nahodha wa Azam FC, TFF ililifanyia kazi kwa kutumia ile kamati ya saa 72 ambayo ilichukua adhabu kali hadi ikalalamikiwa na wadau wengi.

Adhabu ilikuwa kali na ya haraka hadi ikawashangaza wengi. Suala la udhalilishaji halikuwa zuri na niendelee kulikemea kwamba ni baya na Nyosso anapaswa ajifunze.

Lakini hapohapo, najiuliza TFF haioni kuwa si sahihi mchezaji mmoja kukusudia kumuumiza au kumtoa mwenzake uhai kwa makusudi halafu jambo lionekane ni la kawaida? Kwani ile kamati ya saa 72 ni kwa ajili ya wadhalilishaji tu?

Wakati najiuliza maswali tata, kwamba au TFF wana hofu ya kutoa adhabu kwa Ngoma au Juuko kwa kuwa ni wachezaji kutoka katika klabu kubwa?

Halafu najiuliza tena, huenda TFF wanakuwa waoga kutoa adhabu kwa wachezaji wa kigeni kwa kuwa Ngoma anatokea Zimbabwe na Juuko ni raia wa Uganda!


TFF wasisababishe wadau waanze kuzungumza mambo ambayo si sahihi au watetezi wa mambo waanze kufikiria waliofanya hivyo ni wageni na waliofanyiwa ni Watanzania!

Huu ndiyo wakati TFF inapaswa kuitisha kamati husika na mara moja ikae na kutoa uamuzi kwa kuwa kila kitu kipo wazi.

Sitaki kuingia katika masuala ya ushabiki kama isivyo kawaida yangu. Ila nasisitiza, Ngoma na Juuko wamefanya makosa tena ni ya kipuuzi na wanastahili adhabu ili iwe mfano kuanzia kwa wachezaji wa kigeni na wazalendo wengine.

Kumekuwa na uwazi mkubwa katika suala hilo kwa kuwa ushahidi unajitosheleza. TFF inapaswa kulifanyia kazi suala hilo kwa ajili ya kuondoa ukakasi na hakutakuwa na namna zaidi ya wachezaji hao wawili kuadhibiwa na kukumbushwa kwamba wamekuja kucheza soka, wangetaka Kung Fu au karate, wangeweza kuchagua njia nyingine.

Pia nashauri, TFF inapaswa kuwa inachukua hatua haraka kwa matukio kama hayo ili kuwaonyesha wachezaji wenye nia mbaya na afya za wengine kwamba anayefanya hivyo, adhabu kali itafuatia kwa ajili yake.



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic