November 30, 2015




Na Saleh Ally
KATIKA sehemu mbili za mwanzo za makala haya, nilianza kugusa kuhusiana na wale waliokuwa wakipiga kelele na kuidhihaki Taifa Stars eti kwa kuwa ilikuwa inakutana na Algeria kwa kuwa hatuwawezi.


Walisema mengi ikiwa ni pamoja na kusema kwa kuwa hatujakuza vijana ni sawa na kukurupuka na kupita njia ya mkato. Kinachoelezwa ni kitu kizuri, lakini kililetwa katika kipindi ambacho si sahihi Ratiba tunacheza na Algeria, ilikuwa wazi kwa miezi kadhaa.

Angalau wangeza kushauri mapema, waliacha kila mechi ikapita ikiwemo dhidi ya Nigeria, mechi mbili za Malawi na hawakusema. Algeria ndiyo ikawa shida kwa kuwa iliteuliwa kamati ambayo mwisho ilionekana inaingilia maslahi yao binafsi, hapo ndiyo ikawa vita.

Ninaweza kuachana na sehemu hiyo na kuiweka kiporo kutokana na hali halisi ya baadaye. Ninaweza kuelezea mengi zaidi ya hapo ambayo baadhi nina ushahidi nao wa maandishi kama vile malipo kwa baadhi ya waliolipwa katika mechi za nyuma kuitangaza mechi ya Taifa Stars, kamwe hawakupiga kelele kwamba tunatakiwa kukuza vijana. Wakaanza kupiga kelele baada ya kuona maslahi yao yamebanwa, hivyo hawakuwa wazalendo.

Acha niingie kwenye upande wa pili ambao nilieleza ni kuhusiana na viongozi wengi wa TFF kwamba si watu wanaoupenda mpira. Si wapenzi wa kweli wa maendeleo ya soka nchini na zaidi wako pale kwa ajili ya kushibisha matumbo yao.

Nikiwa ndani ya kamati nilishangazwa na mambo mengi sana. Nilianza kuamini kuwa yale ambayo nimekuwa nikiyaandika kwa miaka sasa yana ukweli mwingi sana, ninapaswa kuendelea kuyasisitiza.

Mengi niliyoyajua yalinikatisha tamaa, lakini nikapiga moyo konde na kusimama upya na ndiyo maana leo ninaandika makala haya, ndani ya TFF, kuna lundo la uozo.

TFF ndiyo shirikisho kubwa lililojaza watu wengi wenye uwezo mdogo wanaofanya kila kinachotakiwa kuwa bora na huenda wapo hapo kwa kuwa wanajuana sana na uongozi wa juu, walimsaidia Jamal Malinzi kuingia madarakani au vinginevyo.

Watu hao si wazalendo, wengi wao ni wale wanaofaidika na safari au wanaoishi kwa kutegemea ahsante ya kuusaidia uongozi kuingia madarakan, lakini kamwe hawana uwezo hata kidogo.

Nitaanza na anayeitwa mratibu wa Taifa Stars, Bwana Chacha. Huyu bwana, hajawahi kuwa kiongozi wa juu wa timu yoyote ya daraja la kwanza au Ligi Kuu Bara.

Sasa ndiye mratibu wa Taifa Stars, mtu ambaye anafanya karibu kila kazi ya maandalizi ya kambi ya Taifa Stars ambayo iko ndani na nje ya Tanzania.

Ndiye alisafiri kwenye kufanya maandalizi ya kambi ya Afrika Kusini. Ndiye alisafiri kwenda kufanya maandalizi ya sehemu itakapofikia Taifa Stars kule Algeria na kwangu ninasema yalikuwa ni makosa makubwa.

Soka la sasa, pamoja na utaalamu, angalau uzoefu pia unaweza kuwa chachu. Chacha si mzoefu, hana elimu ya masuala ya soka au si mjuzi wa mipango lakini kila kitu kimewekwa kwake.

Kwangu namuona si mtu anayejua mambo mengi au kumtanguliza kwenda kuandaa kambi ta Taifa Stars dhidi ya Waarabu ni kichekesho kikubwa kabisa!

Chacha anakwenda kuandaa kambi wakati hajawahi hata kuandaa kambi ya timu kama Stand United inayojiandaa kucheza na Yanga au Simba? Ametokea wapi, kwa uzoefu upi na je, kweli anastahili kufanya kazi za Taifa Stars?

Chacha analazimika kuuliza mambo lundo, Chacha ni mgeni katika mambo anayoyafanya lakini ndiye anayefanya majukumu hayo makubwa. Sasa nimeelezwa kuwa amepewa kuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Mashindano. Huu mpira tunaupeleka wapi, sababu za kufikia nafasi hiyo si vigezo, badala yake ni kwa kuwa ni rafiki mkubwa na mwaminifu kwa Malinzi!

Katika maisha yangu, sijawahi kusafiri na timu au Taifa Stars bila ya kazi muhimu na maalum. Ninakwenda safari kwa kuwa ninaijua kazi yangu, ninajua nitaifanya kwa ufasaha.

Sijawahi kusafiri na timu kwa ajili ya kwenda kufanya manunuzi tu yangu, ya rafiki zangu na familia yangu kama ninavyoona viongozi kama Chacha wanavyofanya. Kwangu nakuwa wazi, hana faida sahihi ya kufanya kinachotakiwa na kuisaidia Stars lakini yuko hapo kwa sababu ya uaminifu wake kwa Malinzi au ahsante kwa kiongozi huyo.

Haiwezi kuwa sahihi kiongozi au mtendaji wa TFF awe pale kwa kuwa tu ni mwaminifu kwa mtu au kiongozi. Kwanza lazima awe bora kiutendaji, awe mwaminifu na anayelipenda taifa lake na timu ya taifa, mwaminifu kwa nchi na timu ya taifa na si kwa kiongozi.

Wako waliosema, inawezekana Bwana Chacha anatumika vibaya. Mimi nikasisitiza, “Namjua kwa uadilifu, ni mtu mwema, tatizo ninacholilia ni uwezo wake na nafasi anayopewa. Ndiyo maana tunaanguka halafu tunasingizia hatujakuza vijana. Yako mengi yanayotushusha, moja wapo ni kuwa na watu wenye uwezo mdogo au duni kulingana na nafasi walizopewa kishkaji.”

Kichekesho kingine ambacho nimekishuhudia ndani ya hilo ni ufujaji tu wa fedha. Mfano, kamati ambayo ilikuwa inahusika na timu, ilipanga mambo yawe hivi; timu iondoke na ndege ya kukodi ya Fastjet ambayo wangepanda wachezaji, makocha, viongozi na mashabiki kwenda moja kwa moja kupambana na Waalgeria.

Stars ilipanga kutoka Dar es Salaam, ingetua jijini N’djamena, Chad ndege ‘ingekunywa’ mafuta, baada ya hapo ingeondoka kwenda Marakech, Morocco. Hapo timu ingetulia hadi siku ya mechi, halafu ingeruka dakika 45 kwenda kuwavaa Waalgeria, baada ya hapo ingeondoka kurudi Tanzania.

Lengo lilikuwa ni kukwepa hujuma na fitna za Waalgeria ambao ninaamini lazima ‘waliitekenya’ Taifa Stars kutokana na ilivyoingia Algers kizembe kabisa.

Wakati kamati inashughulikia hilo la Fastjet, tena likiwa katika hatua za mwisho kabisa na makubaliano yamefikiwa, ilipata taarifa TFF ilikuwa imeshalipa tiketi za ndege kutumia Turkish Airways!

Hii ilileta mkanganyiko wa juu kabisa kati ya kamati na TFF. Watu wa kamati walitoa taarifa kwa shirikisho wanachofanya lakini TFF waliendelea kufanya bila ya kuzungumza lolote hadi walipofanikisha.

Mwanakamati mmoja aliyepambana kuwashawishi Fastjet kupunguza bei kwa kiasi cha chini kabisa, alijikuta akimwaga chozi kuhofia heshima yake kuvurugika.

Fastjet baada ya kupewa taarifa hiyo walikasirika kabisa. Waliona ni uswahili wa hali ya juu na mwisho kuna gharama walizokuwa wameingia wakataka walipwe haraka sana.


TFF haikuwa tayari kulipa, yule mjumbe hakuwa na uwezo huo na alikwishavunjika nguvu. Hivyo Mwenyekiti wa Kamati, Faroukh Baghoza akalazimika kutoa mfukoni mwake zaidi ya dola 1,000 (zaidi ya Sh milioni 2.5) ili kufidia gharama.

ZAIDI ENDELEA KUSOMA SEHEMU YA NNE

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic