May 24, 2017



Mshambulizi wa Yanga, Mzimbabwe, Donald Ngoma, amelazimika kubaki nchini kwa ajili ya kusubiria na kujua hatima yake ndani ya timu hiyo kama atakuwepo kwa msimu ujao au la.

Ngoma aliyetua Yanga misimu miwili iliyopita akitokea FC Platinum ya kwao Zimbabwe, amebakisha mwezi mmoja wa kuitumikia timu hiyo ambapo mkataba wake unatarajiwa kufika ukingoni mwezi Juni, mwaka huu wakati timu hiyo ikiwa kwenye mchakato wa usajili mpya.

Mshambuliaji huyo ni miongoni mwa wachezaji wa kimataifa wanaomaliza mikataba, wengine ni Vincent Bossou, Thaban Kamusoko, Haruna Niyonzima na Amissi Tambwe.

Ngoma aliyefunga mabao nane msimu uliomalizika, hivi karibuni amesema kuwa ameshindwa kusafiri kurejea kwao kutokana na kutaka kumalizana na viongozi wake kwa ajili ya mkataba mpya.

“Nasubiri kumalizana na viongozi wangu kwa ajili ya kutambua uwepo wangu msimu ujao maana kama unavyofahamu mkataba wangu unafikia ukingoni, hivyo ningependa kurejea nyumbani nikifahamu kama nitaendelea au itakuwaje.

“Unajua nimekuwa nikisumbuka kwa muda mrefu na majeraha tangu mzunguko wa pili ulivyoanza, lakini namshukuru Mungu nishafanyiwa matibabu ambapo nimeambiwa nitakuwa nje kwa miezi miwili, hivyo mapumziko ya ligi itakuwa moja ya kuupumzisha mwili nikisubiria siku za kurejea uwanjani zifike,” alisema Ngoma.


Aliongeza: “Najua kuna maneno mengi yalikuwa yanaongelewa juu yangu kwamba nimesaini na baadhi ya klabu, jambo ambalo siyo kweli kwani bado nina mkataba na Yanga na nia yangu ni kuitumikia timu hii."

SOURCE: CHAMPIONI

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic