September 11, 2017

UKITAKA uishi huku unapiga hatua zenye mwendo mzuri au ulio sahihi, ni vizuri kama utakubali kila siku unayopata nafasi ya kuishi lazima ujifunze kitu. Nasema kila siku unayopata nafasi kwa kuwa mimi na wewe ni wanadamu, kila siku moja au dakika tunayoishi ni zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu kwa kuwa yeye ndiye mwenye uamuzi wa mwisho katika kila kitu. Hivyo, ni vizuri kuipa thamani kubwa siku au muda unaopewa kuendelea kuwepo duniani. 


Kujifunza ni moja ya thamani hiyo kuliko kutaka kuonekana unajua kitu. Huenda huo ukawa ni ujumbe niliopenda nianze nao katika Metodo ingawa nilicholenga kuzungumzia ni suala hilohilo la kujifunza. Natamani sana kuona Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) na Chama cha Mako cha Tanzania (Tafca) wanaamka na kukumbuka kwa kuwa kuna jambo huwa wanalisahau kwa kiasi kikubwa na wameendelea kulisahau kwa siku nyingi. Suala la kuwafundisha walimu wa makipa kwa ajili ya maendeleo ya soka nchini. Kila kukicha wenzetu ambao kwao mpira umeendelea wanazipa thamani siku wanazoishi kwa kujifunza na kujiimarisha. Katika kozi nyingi za mchezo wa soka zinazotolewa hasa nyumbani Tanzania, makocha wamekuwa wakipewa kozi za pamoja bila ya kuangalia wao watafundisha upande upi. 

Lakini nchi nyingi za Ulaya, Amerika Kusini, Asia na kwingineko ambako mpira umepiga hatua, kuna kozi maalum tena hatua kwa hatua kwa ajili ya makocha wa makipa. Kuwafundisha makochawa makipa, maana yake ni kuwaandaa kwa ajili ya kuzalisha makipa bora ambao watakuwa na kiwango sahihi kwa ajili ya kuzitumikia timu zao. Kuwafundisha makocha “jenero”, si jambo baya. Lakini kocha ambaye anaweza kuwa na faida kidogo kwa makipa ni yule aliyekuwa golikipa halafu akafundishwa kozi ya ukocha wa kawaida. Lakini bado anaweza asiwe msaada sana kwa makipa wake kwa kuwa naye atakuwa hayajui mambo mengi mapya ambayo yanatokea katika mpira kwa sasa. Kadiri siku zinavyosonga mbele, mchezo wa soka unazidi kupiga hatua ya maendeleo. Wafungaji au washambulizi na viungo washambulizi wamekuwa wakifundishwa kila namna ya mbinu kuhakikisha wanakuwa bora kuzisaidia timu zao.


Kuzisaidia timu zao ni kufunga mabao, kufunga ni lazima wategue mtego wa safu za ulinzi za timu pinzani na kufunga. Ili wafanye hivyo ni lazima mpira umpite kipa ambaye ndiye mchezaji wa mwisho. Kama ni hivyo, kipa ameandaliwa vipi? Kwa nyumbani Tanzania, makipa wanaendelea kubaki na mbinu za mwaka 47 kutokana na kutokuwa na mafunzo yanayoendana na wakati ili kuwafanya wawe washindani na kwenda na muda sahihi. Kama mshambuliaji na kiungo mshambuliaji wanapewa mbinu mpya za kumshinda kipa. Tujiulize, kipa anapewa mbinu gani za kisasa kupambana na zile za kisasa za wapinzani wake? Hakuna anayeweza kukataa kuwa makipa wengi sasa wanadaka kwa kutumia vipaji vyao kwa kuwa hata walimu wanaowafundisha
nao wanatumia vipaji vyao pia! Hatuwezi kusema wana mbinu mpya wakati hatujaona mafunzo wanayopewa kuboresha mbinu hizo! 


Kama ni hivyo, vipi tunaweza kuufanya mpira wetu kukamilika kimafunzo na kuwa na ushindani uliokamilika timu zetu zinapocheza tukianzia kwa kipa namba moja, mabeki, viungo hadi washambulizi? Makipa wana mafunzo yao, wanaanza kufundishwa walimu nao wanawafundisha makipa. TFF inapaswa kuliangalia hili ili kuwawezesha makipa tulionao kwenda na wakati na kuachana na kutegemea vipaji. Inawezekana sasa tukaliona halina umuhimu, ushauri wangu vizuri  kushituka mapema kabla hatujaachwa katika kiwango cha kutisha, siku tunashituka, tutajikuta tupo katika dunia ya peke yetu!


MSIMU wa Ligi Kuu Bara tayari umeanza kwa timu 16 katika kampeni ya kuhakikisha wanatwaa ubingwa wa msimu huu mbele ya mabingwa watetezi Yanga ambao wamefanikiwa kuchukua ubingwa huo mara tatu mfululizo. Tangu msimu wa 2014/15, 2015/16 na 2016/17, Yanga wamekuwa mabingwa kitu ambacho ni cha kupongezwa kutokana na nguvu kubwa waliyoitumia mpaka kuweza kutimiza suala hilo. Hii sasa inaonyesha kuwa, msimu huu Yanga watakuwa na wakati mgumu katika mechi zake kwa kuwa ni bingwa mtetezi ambaye kila timu itakayokuwa inakutana nayo itataka kuhakikisha inafanikiwa kuifunga sasa lazima wajipange kwa  kukabiliana na hali zote. Tayari tumeshuhudia katika mechi za kwanza ambazo timu zote zimecheza matokeo yao tumeyaona na inaonyesha wazi jinsi timu zilivyoweza kujipanga kufanya vizuri kwa kuwa kila moja inaonekana kuwa moto hakuna ambayo inadharaulika. Licha ya ligi kusimama kupisha mchezo wa timu ya taifa lakini tumeshuhudia kwenye mechi zilizopigwa juzi Jumamosi na jana Jumapili namna zilivyokuwa ngumu kutokana na matokeo yaliyopatikana kupitia michezo hiyo licha ya kwamba baadhi yao wana vikosi bora walivyovisajili kwa gharama kubwa. Tumeshuhudia Simba ikianza vizuri katika ligi ya msimu huu  kwa ushindi mkubwa wa mabao 7-0 dhidi ya Ruvu Shooting hii ilikuwa kwenye mchezo wao wa kwanza kabisa uliopigwa wiki mbili zilizopita na juzi Jumamosi wakatoa suluhu na Azam FC kwenye Dimba la Chamazi Complex.
Ukiangalia hapo unapata picha halisi ya jinsi ushindani ulivyo mkubwa kwa kila timu kuwa na kiu ya kutaka kufanya vizuri kutokana na maandalizi waliyofanya kwenye pre-seasons. Timu kama Singida United imesajili wachezaji wengi wapya na wenye uzoefu na ligi lakini yenyewe ilianza kwa kupoteza ugenini dhidi ya Mwadui FC, hivyo utaona namna ambavyo ligi ilivyo ngumu haijalishi umesajili kwa fedha kiasi gani lakini uwanjani kila mtu anaona. Azam FC hawakupewa kufanya vizuri hasa kwenye mchezo dhidi ya Simba na Lipuli ilipocheza na Yanga lakini funzo ni kwamba matokeo ya mechi hizo yalikuwaje na kwa nini yawe hivyo?


Jibu lake litakuwa ni kwamba kila timu ilifanya maandalizi ya maana kabla ya kuanza kwa ligi hivyo lolote linaweza kutokea kwa kuwa hakuna mwenye uhakika wa kuanza na kumaliza vyema ligi. Ukweli ligi ni ngumu lazima kila timu ijitume ili kuweza kufikia malengo ingawa bado mapema lakini picha halisi ya ushindani inaonekana kwa timu zote kuonyesha zimejipanga vizuri kwani hakuna mwenye uhakika wa kubaki. Mwisho niwaombe waamuzi kuzingatia kanuni 17 za mchezo wa soka ili bingwa apatikane kwa uhalali maana zimeshaanza kelele kwa baadhi yao kuonekana tatizo kutokana na maamuzi ambayo wamekuwa wakitoa katika baadhi ya mechi. Tusingependa kusikia tena kelele mara kwa mara kwa kitu ambacho mlikaa darasani na mkakisomea wenyewe, chezesheni kwa haki na msitishwe na makelele ya makocha na wachezaji bali fuateni kanuni zilizowekwa.

JUZI Jumamosi kwenye Uwanja wa Azam Complex jijini Dar es Salaam, tulishuhudia mchezo wa Ligi Kuu Bara uliozikutanisha wenyeji Azam dhidi ya Simba. Matokeo ya mchezo huo yalikuwa suluhu. Awali kabla ya mchezo huo, hofu ilikuwa kubwa kwa mashabiki juu ya usalama wao, lakini Jeshi la Polisi Tanzania likawahakikisha kutakuwa na usalama huku likitoa angalizo kwa mashabiki kwamba wawe wastaarabu. Mashabiki walitahadharishwa mapema kwamba wanatakiwa kufuata utaratibu uliowekwa, lakini pia kwa wale watakaofika uwanjani na kukuta uwanja umejaa, basi warudi nyumbani na kushuhudia mechi kupitia luninga. Kikubwa ambacho naweza kuwapongeza mashabiki, walifuata kile ambacho walitahadharishwa mapema, lakini pia jeshi la polisi lilikuwa limejipanga tayari kuweka ulinzi wa kutosha kuhakikisha hakuna uvunjifu wa amani. Mwanzo mpaka mwisho wa mchezo, hakukuwa na vurugu zile ambazo wengi walikuwa na hofu nazo jambo ambalo linadhihirisha kwamba mashabiki wa soka hapa nyumbani wamestaarabika na kuondoa ile dhana inayoonyesha kwamba mchezo wa soka ni wa wahuni. Kumekuwa na dhana hiyo kutokana na kwamba, mara kadhaa kumekuwa na vurugu viwanjani ambazo chanzo chake ni mashabiki, lakini kilichotokea juzi pale Azam Complex, imeondoa dhana hiyo mbaya. Rai yangu ni kwamba, amani kama hiyo iendelee kutokea viwanjani kote ili kuepusha uharibifu wa mali viwanjani kama ilivyotokea Uwanja wa Taifa katika mechi kadhaa kama ile ya Yanga dhidi ya TP Mazembe na ya msimu uliopita iliyowakutanisha Simba na Yanga ambayo ilisababisha uwanja huo kufungwa kutokana na mashabiki kung’oa viti. Kutokana na vurugu kutawala sana viwanjani, siku za nyuma Shirikisho la Soka Tanzania
(TFF), lilishindwa kutoa ruhusa kwa Azam FC kuutumia uwanja wao huo kwa mechi za nyumbani dhidi ya Simba na Yanga. TFF ilikuwa haina imani na usalama wa uwanja huo kwa jinsi ulivyo, kwanza unaingiza idadi ndogo ya mashabiki ambayo ni 7000 tofauti na Uhuru unaoingia zaidi ya mashabiki 23,000 na ule wa Taifa unaochukua watazamaji 60,000. 

Mashabiki wa Simba na Yanga wanapocheza na Azam wanakuwa wengi, hivyo TFF ilikuwa ikihofia kuzuka kwa vurugu kama itatokea mashabiki watakuwa wengi tofauti na uwezo wa uwanja huo. Lakini baada ya jeshi la polisi kujiridhisha juu ya kujipanga kwao kulinda usalama na kuwadhibiti mashabiki, tukaona TFF ikiruhusu kwa mara ya kwanza kutumika na mpaka dakika tisini zinamalizika, Azam ikashindwa kufungana na Simba. Baada ya mchezo huo kumalizika kwa amani, tunatarajia kuona tena Yanga wakienda hapo na mambo yakiwa sawa katika suala zima la usalama kama ilivyo kwa wenzao wa Simba. 

Mwisho kabisa niwaambie Ruvu Shooting, Mtibwa Sugar na Mwadui FC ambao nao walikuwa wanataka kuona mechi zao dhidi ya Simba na Yanga zinachezwa kwenye viwanja vyao, kuvifanyia marekebisho ili kuipata haki yao. Kwa mujibu wa Kaimu Katibu Mkuu wa TFF, Kidao Wilfred, viwanja vya timu hizo ambavyo ni Mabatini, Manungu Complex na Mwadui Complex havina hadhi ya kuchezewa mechi hizo kutokana na kutokuwa na majukwaa ya kutosha. Kama kweli viwanja hivyo vinataka kupata haki kama waliyoipata Azam FC, hawana budi kufuata kile TFF inavyotaka kwani tayari wameambiwa juu ya kuweka majukwaa kwenye viwanja vyao ili hata zile mechi zingine wanazocheza hapo ziweze kuchezwa kwani wasipofanya hivyo, kuna hatari ya kufungiwa viwanja vyao.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic