March 31, 2019


HISTORIA imeandikwa Uwanja wa Taifa kwa namna ambavyo kikosi cha timu ya Tanzania Taifa Stars kilivyofanikiwa kuvunja ule mwiko ambao wengi walikuwa wakifikiria itakuwa ngumu kuvunjwa.

Kufuzu kwa Stars pale kwa kuitungua Uganda mabao 3-0 haikuwa rahisi na wengi wamefurahi kuona safari imeiva hasa kwa vijana wetu wa timu ya Taifa.

Pongezi kwa wachezaji kwa kuonyesha uzalendo na kujituma kuandika historia hicho ni kitu muhimu na cha kujivunia kwa kila mmoja.

Watanzania wamepata kile ambacho walikwa wamekikosa kwa muda mrefu hali inayofanya furaha kuzidi kuongezeka.
Miaka 39 kukatika bila timu yetu kushiriki michuano ya Afcon si haba ni mingi sana hasa kwenye ulimwengu wa michezo.

Ikumbukwe kwamba ni viongozi wengi wamepita wakitazama namna ambavyo soka la Tanzania linakwenda kwa kasi ya kupanda na kushuka ila sasa kuna mabadiliko yameanza kuonekana.

Ilifika wakati kiongozi mkubwa wa nchi aliamua kuita Tanzania kuwa ni kichwa cha mwendawazimu kwa upande wa mpira hakukosea alikuwa sahihi kutokana na matokeo mabovu ila sasa jina limefutwa.

Limefutwa kwanza na yeye mwenyewe aliamua kutengua kauli yake pia wachezaji wamekuwa wakionyesha utofauti kwa kupambana wakiwa ndani ya uwanja.

Ni zamu yetu sasa kufanya makubwa zaidi ya hapa kama ambavyo sera yetu ilikuwa mwendelezo unatakiwa kuwepo isiwe ni nguvu ya soda kisha tukapoteana.

Kufunzu kushiriki Afcon ni suala lingine na kujiaandaa kufanya vizuri ni jambo jingine tofauti kabisa linahitaji maandalizi na sio kukurupuka.

Tumeona namna Bendera ilivyopeperushwa mpaka kufikia hatua ya kuwafunga wapinzani wetu Uganda ambao walikuwa ni vigogo kwenye kundi letu L, si jambo jepesi linapaswa kupongezwa.

Kilichobaki kwa sasa wachezaji na benchi la ufundi kuanza kuchanga karata upya kwa ajili ya michuano hiyo hasa baada ya kupangwa kwenye hatua ya makundi.

Unaambiwa kwamba linaloisha ni dogo kuliko lile linalokuja, wachezaji na benchi la ufundi hawajamaliza vita hivyo nisehemu ya kwanza ya vita maadui wengi wanakuja.

Serikali imeonesha namna ilivyo bega kwa bega na wanamichezo kutokana na pongezi za Rais, John Magufuli, kuna deni ambalo ameliacha kwa wachezaji na watanzania.

Hivyo wachezaji mnapaswa mtambue kwamba kila hatua ambayo mnapita mnatazamwa kwa ukaribu na wengi wanawakubali hasa mkifanya vizuri.

Nafasi ya kuongea na Rais ni kubwa na zawadi ambayo mmepewa si haba inabidi mshukuru kwa vitendo kwa kupata matokeo uwanjani.



Ni fursa adimu kwa nyakati hizi,  kuna waliopambana kwa ajili ya Taifa ila hawakuitwa Ikulu kupewa pongezi namna pmoja na zawadi.

Endapo mtakazana mengi sana mtayavuna kutoka kwa Serikali pamoja na mashabiki ambapo wapo nanyi bega kwa bega mna kazi ngumu ya kufanya kuonyesha thamani ya kile ambacho mmefanyiwa.

Mashabiki wa Tanzania kwa namna ya pekee mmeonyesha uzalendo na nguvu ya umoja inavyoleta matokeo chanya.
Wahenga hawakukosea waliposema umoja ni nguvu na utengano ni udhaifu mmefanya jambo ambalo limeutikisa ulimwengu hasa kwenye medani za soka.

Wingi wenu na kujitokeza kwenu kuwe ni kila siku isiishie kwenye mechi moja tu kwani kwa hatua ambayo Stars imepenya kuna mechi nyingi zinakuja ni wakati wenu kuendelea kujitoa.

Kwa sasa nguvu yenu iwe kwa ajili ya Taifa na mfanye mengi ya maana kwa ajili ya kupeperusha bendera ya Taifa hasa linapokuja suala la utaifa.

Kamati ya hamasa iliyokuwa chini ya Mwenyekiti wake Paul Makonda ilifanya kazi ya kipekee kwa kutoa hamasa ambazo ziliwafanya mashabiki kujitokeza kwa wingi.

Hakuna ambacho watanzania wanaweza kuwapa ila ni shukrani zao na kujitokeza kwao uwanjani ilikuwa ni majibu ya kukubali wito wenu.

Hii inamaanisha tuna nguvu na tunaweza kufanya jambo kubwa endapo tutaamua kushirikiana ndugu Makonda mipango na sapoti isisishie hapo ni lazima iwe na mwendelezo.

1 COMMENTS:

  1. Hongera Taifa stars ila suala la kuisifia timu kupita kiasi mbele ya timu ya Taifa ya Uganda iliyokuwa haina cha kupoteza kitu katika mchezo huo ni jambo la kushangaza. Kuna hata baadhi ya viongozi wa TTF wameshaanza kutoa maneno ya kejeli kwa wadau waliotaka au kupekeza kufanyiwa mabadiliko ya benchi la ufundi la Taifa stars. Amesikika mkurugenzi wa ufundi wa TTF Ame kinje akisema kuwa watu wanaopendekeza kufanyiwa marekebisho benchi la ufundi hasa kocha mkuu kuwa ni watu wenye mihemko. Hata muheahimiwa raisi Magufuli alitamka wazi Taifa stars ilikuwa na matatizo kwenye benchi la ufundi na kwa kiasi fulani ilimvunja moyo kiasi cha mkuu huyo wa nchi kusita kidogo kumalizia kusema kuwa kocha mkuu wa Taifa stars alishindwa kutimiza majukumu yake ipasavyo na nnaimani kabisa kama Magufuli angekuwa ndie raisi wa TTF basi Amunike angelishafungasha virago vyake zamani tu. Binafsi siwezi kumpa Amunike full credit kwa timu ya Taifa stars kufuzu Afcon. Watanzania tunemukuja kutumia nguvu kubwa kupigania kufuzu Afcon katika mchezo ambao ulikuwa pata potea. Madhaifu ya benchi la ufundi bado yapo na wataendelea kuwepo kama wahusika wataendeleza kiburi. Kiburi cha wahusika wanaoisimamia Taifa stars kutokukubali kusikiliza ushauri wa wadau wengine kwa miaka mingi ndicho chanzo cha kufeli kwa Taifa stars. Kwa mfano hivi sasa sherehe za kufuzu Afcon kwa taifa stars zinapaswa kusahaulika kabisa na kinachopaswa kufanywa kwa watanzania ni kuwa katika mikakati mizito ya kuiandaa Taifa stars kwenda kuwa mshindani wa kweli AFCON Misri badala ya kwenda kuwa mshiriki tu. Badala ya viongozi wa TTF kuanza kutumia mitandao ya kijamii kwa ajili ya mipasho na tambo nadhani ni wakati muafaka kwa viongozi hao kutumia mitandao ya jamii kwa ajili ya kusaka wachezaji wenye uwezo wa kuitumikia Taifa stars kwa ajili ya AFCON hasa wale wa kigeni ambao wana asili ya Kitanzania ambao watakuwa tayari kuitumikia stars. Kundi hilo la wachezaji wenye asili ya Tanzania ni kubwa kama watafuatiliwa.TTF vile vile wanatakiwa kufanya kazi kubwa ya kuitafutia Stars mechi ngumu nyingi za kujipima nguvu. Vile vile suala la Abdi Banda sio la kuachiwa kupita hivi hivi inajulikana kuna tofauti kati yake na benchi la ufundi ila Banda ni moja ya matamanio ya watanzania waliowengi kuona vijana wao wanafanya jitihada ya kwenda kucheza nje kwa mafanikio ili kurejesha uzoefu wao nyumbani. Na unapozungumzia moja ya beki bora wa kati kwenye ligi ya Sauzi Africa basi Banda ni miongoni mwao. Banda kitabia ni Msemaji anapoona kuna kitu kinamkwaza wahusika wanatakiwa kuelewa hilo na si kughadhibika peke yake ila ni mchezaji kazi anaejituma na kiraka pia.

    ReplyDelete

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic