October 18, 2019




LEO nchini Sudan, Kocha Mkuu wa timu ya Taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’ Etienne Ndayiragije atakuwa na kazi ngumu ya kupindua meza kibabe mbele ya Sudan kwenye mchezo wa  kutafuta tiketi ya kufuzu michuano ya CHAN ambayo inawahusisha wachezaji wa ndani.

Mchezo huu utapigwa uwanja wa El Merriekh, Omdurman ikiwa na kumbukumbu ya kupoteza kwa kufungwa bao 1-0 uwanja wa Taifa jambo ambalo limeongeza mlima mzito kwa timu ya Taifa kupata ushindi.

Rekodi zinaonyesha kwamba, Ndayiragije hajawa na bahati ya kupata ushindi katika michezo sita ambayo ameiongoza baada ya kukabidhiwa timu kutoka kwa Mnigeria, Emmanuel Ammunike kwa kushindwa kupata ushindi ndani ya dakika 90.

Kwenye michezo hiyo sita safu yake ya ushambuliaji imefunga jumla ya mabao mawili pekee huku ikikubali kufungwa jumla ya mabao matatu ambapo imepoteza mchezo mmoja mbele ya Sudan ambao wanarudiana nao leo, sababu zinazofanya mtihani kuwa mgumu hizi hapa:-

Hajaambulia ushindi ndani ya dakika 90

Ndayiragije kwenye michezo sita aliyoongoza hajaambulia ushindi ndani ya dakika 90 zaidi ya sare na kufungwa.Taifa Stars ilianza kupata sare ya bila kufungana na Kenya kwenye mchezo wa CHAN uwanja wa Taifa, mchezo wa marudio uliopigwa Kenya matokeo ilikuwa ni 0-0 Stars ilishinda kwa penalti 4-1 ikasonga mbele na kukutana na Sudan ambapo ilipoteza mchezo wa kwanza uwanja wa Taifa kwa kufungwa bao 1-0.

Mechi nyingine ilikuwa dhidi ya Burundi kwa ajili ya kusaka tiketi ya kuwania kufuzu makundi ya Kombe la Dunia mchezo wa kwanza ilikuwa sare ya bao 1-1 na mchezo wa marudio uwanja wa Taifa sare ya bao 1-1 na Stars ilishinda kwa penalti 3-0.

Mchezo wake wa sita ilikuwa dhidi ya Rwanda ambao ulikamilika kwa sare ya bila kufungana.

Ubutu wa safu ya ushambuliaji

Mpaka sasa kwenye michuano ya Chan hakuna mshambuliaji ambaye amefunga bao jambo ambalo linampasua kichwa Ndayiragije na benchi nzima la ufundi linaloundwa na Seleman Matola pamoja na Juma Mgunda ambaye aliweka wazi kwamba kuna janga kwenye safu ya ushambuliaji.

Mabao mawili ambayo Stars imefunga yalipachikwa kimiani na wafungaji wanaokipiga nje ya Bongo ambao ni Mbwana Samatta nahodha anayecheza KRC Genk na Simon Msuva anayekipiga Difaa El Jadida ya Morocco.

Pengo la Bocco na Aiyee

John Bocco kwa sasa bado hajarejea kwenye ubora wake kutokana na kusumbuliwa na majeraha ya goti ambayo aliyapata kwenye mchezo dhidi ya Azam FC kukosekana kwake ndani ya kikosi cha Taifa Stars kumekuwa kukiwapa taabu makocha kumtafuta mbadala wake ambae imekuwa ngumu kumpata.

Salum Aiyee anayekipiga KMC naye amekuwa nje ya timu ya Taifa kutokana na kusumbuliwa na majeruhi, licha ya kutokuwa na muda mrefu ndani ya timu ya Taifa ni miongoni mwa washambuliaji wazawa ambao wanalijua lango kwani msimu uliopita alifunga jumla ya mabao 18 jambo linaloongeza ugumu kwa Ndayiragije.

Mfumo wa Ndayiragije

Asili ya Ndayiragije muda mwingi ni kujilinda kwani kwenye mechi sita alizosimia timu ya Taifa ya Tanzania ameambulia sare tano ndani ya dakika tisini na kupoteza mchezo mmoja dhidi ya Sudan ambao ulichezwa uwaja wa Taifa.

Mmachinga anatoa somo hili

Mshambuliaji wa zamani wa timu ya Taifa ya Tanzania, Mohamed Hussein ‘Mmachinga’ ambaye ni Kocha wa timu ya Vijana ya Yanga, alisema kuwa tatizo kubwa inatokana na wachezaji wengi kushindwa kujitambua na kuwa na papara wakiwa eneo la hatari.

“Kuna umuhimu wa kocha kubadili mbinu hasa ukizingatia amekuwa akipata sare michezo yake mingi, tatizo la ushambuliaji lipo kwa wachezaji wetu ila linapaswa litafutiwe dawa na benchi la ufundi, jambo la msingi ni wachezaji kupunguza papara wakiwa eneo la hatari itasaidia kupata matokeo chanya,” alisema.

Julio pia aongeza neno

Jamhuri Kihwelo ‘Julio’ Kocha wa zamani wa Simba na Dodoma FC alisema kuwa wachezaji wa timu ya Taifa wanapaswa wapambane kufa na kupona kupata matokeo chanya licha ya kuwa ugenini nafasi ya kushinda ipo mikononi mwao.

“Ushindi kupatikana ni mbinu na kujituma kwa wachezaji ndani ya uwanja na sio maneno, ninaona kuna uwezekano kwa timu kupata matokeo chanya iwapo wachezaji watajituma na kutimiza majukumu kwa wakati ndani ya uwanja,” alisema Julio.


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic