December 5, 2019



MICHUANO ya Cecafa kwa wanawake ilimalizika  hivi karibunikwenye ardhi ya Bongo na bingwa kuwa Kenya baada ya kuwafunga wenyeji Tanzania Bara mabao 2-0.

Katika michuano hiyo iliyochezwa kwenye Uwanja wa Azam Complex jijini Dar, ilikuwa na msisimko mkubwa sana na timu zilizoingia fainali zilionekana kupambana hadi kufika hapo.

Kama unakumbuka, Tanzania Bara ambayo maarufu ni Kilimanjaro Queens na Kenya, hadi zinafika fainali hazikuwa zimepoteza mechi yoyote. Zilishinda zote kuanzia hatua ya makundi hadi nusu fainali.

Katika fainali, Kenya iliposhinda ikaondoka kwenye michuano hiyo ikiwa na ushindi wa asilimia mia moja kwa kushinda mechi zote tano za michuano hiyo. Wanapaswa kupongezwa kwa hilo.

Kilimanjro Queens nao licha ya kukosa ubingwa huo, nao wanapaswa kupongezwa kwani walifanya kazi kubwa sana. Bahati haikuwa upande wao, wakajikuta wakifungwa fainali.

Maumivu waliyoyapata wachezaji na benchi la ufundi la timu hiyo, ni sawa na maumivu waliyoyapata Watanzania wote kwa jumla kwani hakuna ambaye alitarajia kuona timu hiyo ikilipoteza kombe hilo hapa nyumbani.

Kitu kibaya ni kwamba, Kilimanjaro Queens imelikosa kombe hilo ikiwa bingwa mtetezi baada ya kulitwaa mara mbili mfululizo katika nchi za Rwanda na Uganda. Kama ingelichukua na safari hii, ingekuwa mara ya tatu mfululizo.

Wakati tukizipongeza timu hizo, pia tuzikumbushe Zanzibar, Djibouti na Sudan Kusini kufanya maandalizi kabambe kwenye nchi zao ili wakati mwingine zije zikiwa imara zaidi.

Timu hizo ndizo zilizofanya vibaya zaidi kwenye michuano hiyo na kudhihirisha wazi kwamba hazikuwa zimejipanga.

Naweza kusema kwamba, kilichoibeba zaidi Kilimanjaro Queens ni uwepo wa Ligi Kuu ya Wanawake na Ligi Daraja la Kwanza Wanawake hapa Tanzania.

Ligi hizo zimesaidia sana kuwa na timu imara ambayo ikiendelea kutunzwa, itafika mbali na kushiriki michuano mbalimbali ya kimataifa.

Wakati Kilimanjaro Queens wakifanya yao kwa upande huo, kaka zao, Kilimanjaro Stars nao wanajiandaa kushiriki michuano ya Chalenji itakayoanza Desemba 7, mwaka huu nchini Uganda.

Ni michuano ambayo Kilimanjaro Stars inapaswa kufanya kweli na kuliletea heshima taifa kwa kutwaa ubingwa huo.

Tayari Kocha Mkuu wa Kilimanjaro Stars, Etienne Ndayiragije ametangaza kikosi chenye jumla ya wachezaji 32 kikiwa ni cha awali kabla ya baadaye kufanyika mchujo na kubaki ambao watakwenda kuipeperusha bendera ya nchi kwenye michuano hiyo.

Wachezaji ambao mmeitwa hivi sasa, tambueni kwamba mna jukumu kubwa la kufanya kuhakikisha mnaliletea heshima taifa hili.

Kina dada wamepambana lakini mwisho wa siku wameukosa ubingwa wa Cecafa, kaka zao nanyi piteni njia sahihi ili mrudishe furaha ya Watanzania iliyopotea.

Watanzania tutakuwa nanyi bega kwa bega kuhakikisha mnafanikisha malengo hayo na tayari kuna mipango ya baadhi ya Watanzania wamepanga kwenda Uganda kuishangailia timu hiyo.

Imani yangu ni kwamba, wachezaji watajituma zaidi katika kusaka matokeo mazuri, lakini pia kujitangaza kwani kitakuwa ni kipindi cha usajili wa dirisha dogo hapa nchini.

Dirisha dogo litafunguliwa Desemba 16, mwaka huu na kufungwa Januari 15, mwakani, hivyo wachezaji tumieni vizuri michuano hii kujitangaza zaidi.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic