February 3, 2020


SHIRIKISHO la Soka la Kimataifa (Fifa) limemtaka kiungo wa Simba, Luis Jose Miquissone kuwaandika barua ya kuchagua wapi anataka kucheza kati ya Simba na UD Songo.

Simba ilimsajili Luis katika usajili wa dirisha dogo uliofungwa Januari 15, mwaka huu akitokea Mamelodi Sundowns ambako alikuwa anacheza kwa mkopo kutoka UD Songo ya Msumbiji.

Mpaka sasa Luis hajafanikiwa kucheza mechi za kimashindano zinazotambulika Fifa kutokana na kutopata kibali ‘ITC’ na UD Songo wanadai bado ni mchezaji wao hivyo wamegoma kumruhusu kuichezea Simba.

Katibu Mkuu wa Simba, Dk Arnold Kashembe alisema tatizo la kutopata kibali kwa Luis linatokana na UD Songo kumng’ang’ania wakidai ni mchezaji wao licha ya kumaliza mkataba Januari mwaka huu hali iliyowalazimu wao kwenda Fifa kudai haki yao.

“UD Songo wanamng’ang’ania Luis wakidai bado mchezaji wao, lakini mkataba wake umeisha Januari mwanzoni, hivyo ndio maana kibali chake kimekuwa tatizo kutokana na mvutano uliopo.

“Tumepeleka malalamiko Fifa kupitia TFF ili kupata ufumbuzi wa jambo hilo ili kuweza kumtumia mchezaji akiwa kama mchezaji huru.

“Fifa wametujibu barua yetu juzi ambapo wamemtaka mchezaji mwenyewe aandike barua aamue aende upande gani kati ya UD Songo ama Simba na tayari ameshaandika barua kupitia TFF tumeiwasilisha hivyo tunasubiria majibu, nadhani ndani ya siku mbili hizi tutapata jibu,” alisema Kashembe.

Hivi karibuni, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Simba, Mohammed Dewji alikutana na Rais wa Fifa, Gianni Infantino na kuzungumza naye mambo mbalimbali ya kisoka huku akimkabidhi jezi ya klabu hiyo yenye wa jina la rais huyo.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic