March 21, 2020



WIKI hii naweza kusema ilikuwa chungu kwa viongozi wa timu ndogo na zenye uchumi duni kwenye ligi zetu hapa nchini.

Ndio ilikuwa chungu baada ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) na Bodi ya Ligi kutangaza mechi chache zilizosalia za ligi zitachezwa bila ya mashabiki, inamaana watakosa pesa za viingilio.

Hilo ni pigo kubwa kwa hizo timu ambazo sehemu kubwa zinategemea mapato ya mlangoni kujiendesha kama vile kulipia kambi na safari.

Kazi ipo, tena ni kazi kubwa mno kwa viongozi wa timu hizo ambao hivi sasa najua vichwa vinawauma na hawajui chakufanya maana maamuzi hayo ni machungu kwao.

Wengine waliopata pigo ni wazee wa kupiga ambao ni wazuri wa kufanya manuva ili kupiga mzigo kwenye tiketi na mambo mengine.

Maana kuna watu tunawajua wao wanasafiri na timu kila mkoa hasa timu za Simba na Yanga na kila sehemu unayoenda wao wako getini tu hadi unajiuliza hivi hawa ndio mafundi wa hizo kazi?

Safari hii najua hakuna shida na hakutakuwa na vurugu kwenye milango mikubwa ya kuingia uwanjani hasa kwa sisi wanahabari ambao wenye mpira wao wanatufanya kama karatasi vile, yaani wakishatuandikia hatuna thamani tena.

Hapa sasa najua watu watanielewa kwa nini tunasema tuna mfumo mbaya wa uendeshaji wa klabu zetu ambao mtaji wake mkubwa ni viingilio.

Maana timu zetu hazina mfumo sahihi wa uendeshaji na utafutaji pesa nje ya uwanja zote zinategemea pesa za viingilio na za wadhamini basi kitu ambacho ni kibaya sana.

Wenzetu wameshatoka huko, wako mbali zaidi na zaidi ingawa sisi bado tumeshindwa kufanya hivyo kwa sababu hatuna watu sahihi wanaojua kuifanya hiyo kazi.

Hata hivyo viingilio vyetu bado ni vidogo mno tofauti na wenzetu hapa Bongo ni kama shabiki anaingia bure kuangalia mpira.

Timu inayosafiri kutoka Mtwara hadi Katavi tena kwa basi dogo na ikifika leo kesho inacheza mechi na baada ya mechi inaondoka unadhani itaweza kweli kuhimili vishindo vya kucheza bila mashabiki? Hilo swali linakosa majibu.

Kwanza lazima tukiri maamuzi ya Bodi ya Ligi na TFF ni maamuzi sahihi kabisa kutokana na hali yetu ilivyo na wamethamini uhai wa mashabiki wa soka wa nchi hii kwa sababu ugonjwa wa Corona ni hatari sana.

Mechi chache zimesalia kabla ya msimu huu kumalizika na timu nyingi hivi sasa pesa zimekata maaana wamezunguka sana na sasa nyingi zinategemea pesa za milangoni.

Hata hizo timu tunazoziita timu kubwa lazima nazo zitayumba kiuchumi maana nazo hazina mifumo sahihi ya kutafuta pesa nje ya uwanja na tena timu hizo ndizo zina mafundi wengi wa kuzitafuna hizo pesa za viingilio.

Juzi kati Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dkt Hassan Abbas aliliambia Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) kuwa kwenye mechi ya Yanga na Simba kuna mianya mingi ya upotevu wa mapato na pesa nyingi zinaenda mifukoni mwa watu na sio kwa wamiliki wa uwanja au klabu husika na hapo sasa utapata jibu jinsi watu watakavyoumia.

Lakini hatuna jinsi kutokana na hali ilivyo lazima timu zikubali tu na zijipange kwa msimu ujao kama hali ikirejea kuwa shwari.


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic