August 28, 2020

 


HEKAHEKA za usajili wa wachezaji wapya kwa ajili ya msimu wa 2020/21 ndiyo habari ya mjini kwa sasa, tangu dirisha la usajili lifunguliwe Agosti Mosi na linatarajiwa kufungwa Agosti 31.

 

Tofauti na miaka ya nyuma, dirisha hili linaonekana kuwa la moto likichagizwa na ufinyu wa muda ambao klabu zimepewa ili kukamilisha taratibu za usajili, ikumbukwe kuwa saa 5:59 usiku wa Agosti 31, kwa saa za Afrika Mashariki usajili utafungwa rasmi.

 

Siku zinavyozidi kwenda ndiyo usajili unazidi kuwa mtamu huku ukisindikizwa na vijimisemo vya uchokozi na kutishia amani kama vile; Tetemeko, kombora, bomu, kusimamisha nchi ili mradi tu kumfanya mtu aliyenunua bando kufuatilia usajili ajihisi hajaibiwa.

 

Nazipongeza klabu zote ambazo tayari zimekamilisha na kutangaza wachezaji wao wapya, lakini kwa namna ya pekee  nazipa heko klabu zetu tatu kubwa hapa nchini  Simba, Yanga na Azam kwani inaonekana sajili zao zimekubalika na wadau wa soka nchini.

 

Kama ilivyotabiriwa na kusubiriwa kwa hamu mpambano kati ya Simba na Yanga kwenye soko la usajili umekuwa mkali kiasi cha kuwaacha watu  wakistaajabu, nani alidhani kama nyota wa zamani wa Yanga, Bernard Morrison angesaini Simba? Vipi kuhusu Ofisa Mtendaji Mkuu wa Simba, Senzo Mbatha ambaye naye ameibukia Jangwani? 

 

Wakati tukiendelea kustaajabu ya Simba na Yanga, kuna klabu moja imenishangaza kidogo, hapa nawazungumzia 'Wagosi wa Kaya' Coastal Union chini ya kocha, Juma Mgunda.

 

Kwanini wananishangaza? Ni hivi Coastal mpaka sasa imeondokewa na baadhi ya wachezaji  muhimu wakiwemo, Bakari Mwamnyeto (Yanga), Ibrahim Ame (Simba) na Ayoub Lyanga (Azam). 

 

Kibiashara Coastal wamefanya vizuri kwa kufanikiwa kupiga pesa ndefu, lakini wakati Simba na Yanga zikivunja benki ili kuimarisha vikosi vyao Coastal wao wako bize na shughuli zao nyingine yaani kama vile hili dirisha la usajili haliwahusu.

 

Wanaishi katika dunia yao ya tofauti, nimeona wako mtaani wanatafuta vijana wa kuwarithi wakina Mwamnyeto, ni wazo zuri kwani hata huyo Mwamnyeto alitokea hukohuko lakini wakumbuke katika soka la sasa hii ni sawa na kamali. 

 

Ni mpango huu ndiyo uliwashusha Singida United msimu huu waliamini vijana wa mtaani na wale wa timu B wangekuwa msaada matokeo yake ilibidi wavunje timu na kusajili rundo la wachezaji wapya kwenye dirisha dogo, wakashindwa kuwalipa hatimaye timu ikashuka.

 

Nawakumbusha tu Coastal soka la sasa linahitaji mabavu kwenye soko la usajili hivyo waache ubahiri na kusajili nyota watakaoweza kuwa mbadala sahihi wa wale walioondoka kwani kwa kiwango kilichoonyeshwa na timu hiyo msimu huu litakuwa jambo la hovyo kuiona Coastal ikikosa muelekeo msimu ujao eti kwa kuwa haikufanya usajili makini.

 


 

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic