December 17, 2020


 

PONGEZI kubwa kwa mashabiki wa soka la Tanzania kwa namna ambavyo wanajitoa kwa hali na mali kwa ajili ya kuzipa sapoti timu zao zikiwa uwanjani.

Kwa kufanya hivyo kunaongeza lile joto kwa kila timu kuingia ndani ya uwanja ikisaka ushindi kwa nguvu. Uwepo wa mashabiki unaongeza hamasa na kuwafanya wachezaji wajitume zaidi.

Kila shabiki anapenda kuona timu inafanya vizuri jambo linalomfanya aweze kufika uwanjani. Wengine ni wale ambao wanakaa nyumbani wakitazama kupitia luniga.

Azam TV wamekuwa mabalozi wazuri wa wachezaji wetu na mpira wetu kwa kuonyesha kila kitu moja kwa moja kuhusu mpira wetu.

Kwa kufanya hivyo nao pia wanastahili pongezi kwa sababu wanaifanya Tanzania inazidi kujulikana kwa upande wa soka ndani na nje ya Tanzania.

Kwenye vita ya kutafuta ushindi hapo ndipo kazi inabidi iwe kubwa kwa wachezaji pamoja na benchi la ufundi kufanya vizuri katika kusaka matokeo chanya uwanjani.

Kwa kupitia yale mapungufu ambayo benchi la ufundi limeyaona kwenye mechi zao zilizizopita. Ikiwa walishindwa kuona makosa vizuri wanaweza kukaa kwa kutazama marudio ya picha ya Azam TV.

Kila siku mambo yanazidi kubadilika na teknolojia inakwenda kasi. Hivyo hata mbinu pia zinapaswa zibadilike kwa sababu kinachotafutwa ndani ya uwanja ni matokeo.

Ninapenda pia kuzikumbusha zile timu za Ligi Daraja la Kwanza kuendelea kupambania ndoto zao ili kufikia malengo ambayo yapo kwenye mipango kazi yao.

Ukweli ni kwamba huku kuna kiwanda kizuri cha kutengeneza wachezaji kwa ajili ya kesho ni muhimu kila mmoja akawekeza nguvu ndani ya uwanja kwenye kusaka matokeo.

 Maandalizi mazuri yanahitajika kwa timu inayosaka matokeo mazuri. Mambo mengine ni ya ziada kwani hakuna kinachowezekana kwenye maisha ya mpira ikiwa hakutakuwa na maandalizi mazuri.

 Kila mchezaji akitambua wajibu wake ndani ya uwanja na akiwa nje ya uwanja kwa kufanya mambo ambayo yanaleta matokeo mazuri kwake na timu itakuwa na matokeo mazuri hapo baadaye.

Wachezaji wanapaswa waelewe kwamba mashabiki wanajitokeza kuwapa sapoti ii kuona matokeo mazuri. Hakuna shabiki ambaye anapenda kuona timu yake ikifungwa hivyo hilo ni deni kwa wachezaji.



Makosa ambayo yametokea kwenye mechi zilizopita ni lazima yafanyiwe kazi. Kwa kupata matokeo mazuri kutaongeza mashabiki wengi ndani ya uwanja.

 Wapo mashabiki ambao wamekuwa wakipenda ugomvi ndani ya uwanja. Kwa kufanya hivyo kumekuwa kukigharimu baadhi ya timu kulipa faini kwa kosa la mashabiki.

Jambo hili mashabiki liwekeni kando kabisa kwa mechi zijazo na hata zile ambazo zinachezwa leo na kesho pia. Ni mbaya mashabiki kujiingiza kwenye ugomvi.

Utani kwa mashabiki sawa, kushangilia kwa kuzomea sawa ila kutupa chupa kwa wachezaji ama benchi la ufundi hapana.

Kurusha chupa kwa ajili ya waamuzi baada ya dakika 90 kukamilika hapana tena hapana isiwe hivyo. Kumpiga shabiki mwenzako kisa jezi aliyovaa hapana katika hili.

Utamaduni wa mashabiki wa Tanzania ni ustaarabu na kushangilia hii ni asili. Basi tuna kazi ya kudumisha asili kwa wakati huu ambao tupo ili kudumisha furaha.

Hata benchi la ufundi pia huwa linakuwa kwenye presha pale mashabiki wanaposhangilia na timu imefungwa ama ipo nyuma kwa mabao kadhaa.

Zile kelele za mashabiki zinawafanya wapate nguvu mpya ya kupambana kwa kuwa hawapo peke yao. Wachezaji pia hata wakiwa wamechoka bado wanapata nguvu ya kufanya vizuri kwa sababu ya mashabiki.

Maisha ya mchezaji yanajengwa na kuwa na nidhamu ndani na nje ya uwanja. Ikitokea akakutana na chungu ya mashabiki basi asiwe mkali awe mpole na mtulivu.

Ikiwa mchezaji atakuwa na nidhamu ndani ya uwanja ni rahisi kwake kufikia mafanikio ambayo anayahitaji. Ila kama itatokea hajali masuala ya nidhamu ni rahisi kushuhudia anguko.

Hivyo ni jukumu la kila mchezaji kutazama namna bora ambayo itamfanya aweze kupata namba kule ambako anakwenda kuanza maisha mapya ndani ya soka.

Kwa waamuzi pia ni muhimu kuzingatia sheria 17 za soka katika kutoa maamuzi ili wasiumie wengine kwa yale maamuzi yenu.

 

 

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic