February 27, 2013




Vinara wa Ligi Kuu Tanzania Bara, Yanga wameendeleza kasi yao ya kushinda mfululizo baada ya kuichapa Kagera Sugar kwa bao 1-0.

Yanga imefanikiwa kuibuka na ushindi katika mechi iliyochezwa kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam leo na kufikisha pointi 42.
Yanga inakuwa timu ya kwanza kufikisha pointi zaidi ya 40 msimu huu lakini ikiwa ndiyo dalili za kuelekea kuwavua ubingwa watani wake wa jadi Simba wanaosua katika nafasi ya tatu.

Bao pekee la Yanga leo lilifungwa na kiungo Myarwanda, Haruna Niyonzima na kumfanya awe amefunga mabao mawili katika mechi mbili na kuisaidia Yanga kubeba pointi sita mfululizo.
Niyonzima ndiye aliyefunga bao pekee katika mechi iliyopita ya Yanga dhidi ya Azam FC ambayo ilikuwa ni muhimu kupiga hatua na kuwaacha vijana hao wauza unga wa ngano na sembe.

Yanga sasa iko kileleni kwa tofauti ya pointi sita, jana ilipoteza nafasi nyingi za wazi za kufunga ukiwemo mkwaju wa penalti ambao aliupiga mshambuliaji wake Didier Kavumbagu raia wa Burundi.

Katika mechi nyingine za ligi zilizochezwa leo, Coastal Union ikiwa nyumbani ilishindwa kufurukuta mbele ya Ruvu Shooting na kujikuta ikilazimishwa sare tasa na Kocha Mkuu, Mohammed Morocco akawalaumu vijana wake kwa kupoteza nafasi nyingi za wazi za kufunga.
Mtibwa Sugar ambaye mechi yake ya mwisho iliitwanga Simba kwa bao 1-0, leo imeshikiliwa na Prisons ya Mbeya baada ya kulazimishwa sare isiyokuwa na mabao.

Polisi Moro ambayo imeamka katika mzunguko wa pili wa ligi hiyo, iliendeleza ushindi baada ya kuilaza Mgambo Shooting kwa bao 1-0. Timu hiyo haikushinda hata mechi moja katika mzunguko wa kwanza hali iliyosababisha kocha wake, John Simkoko kutupiwa virago na nafasi yake ikashukuliwa na mkongwe mwingine Adolf Rishard.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic