April 24, 2013




Na Saleh Ally
KUONDOKA kwa aliyekuwa Kocha Mkuu wa Taifa Stars, Marcio Maximo kuliamsha hoja nyingi sana ambazo nyingi hazikuwa na nguvu badala yake zilionyesha upande wa pili wa Watanzania wapenda soka.

Watanzania wengi wapenda soka ni waoga, wanaamini kupita kiasi na wasio na uwezo wa kuthubutu, ndiyo maana wana hofu sana na mabadiliko.

Mara nyingi, mabadiliko hayapatikani bila ya kuwa na watu wanaoweza kujitolea na kupambana bila ya kuwa na uoga. Kawaida waoga hubaki salama lakini bila ya kupiga hatua.


Maximo raia wa Brazil aliyefanya kazi nchini kwa miaka minne, alikuwa mmoja wa makocha ambao hatasaulika nchini kwa mambo mengi likiwemo la mabadiliko.

Alisaidia mengi, lakini yalikuwepo aliyoboronga na wadau wengi wakawa waoga kuona anakosolewa hata alipoboronga, huenda bado kuna hisia za kuwahofia wageni au wazungu ambao tunaamini wanapatia kila kitu.

Uzuri:
Pamoja na kwamba alileta mabadiliko katika kikosi, lakini alikuwa mjanja katika uhamasishaji nje ya uwanja, alitokea kupendwa na mashabiki ambao alitumia muda mwingi kuwahamasisha. Poulsen hana uwezo huo na macho yote katika kazi yake.

Alijitahidi kuchagua kikosi cha wachezaji vijana, ingawa naweza kusema hakuwa mzuri zaidi kwa upande wa kuamini vijana. Zaidi aliwapa zaidi nguvu wakongwe kama Salum Sued, Mecky Maxime, Shadrack Nsajigwa na walicheza vizuri.

Ingawa bado kiasi fulani vijana wachache aliwajenga kama Jerry Tegete na Kiggi Makasi wakati alipokuwa kocha, walifanya vema.

Tatizo:
Alikuwa kocha mwenye gubu, anayenuna na asiyetaka kusamehe. Ugomvi mkubwa ulikuwa ni kuwanunia Athuman Idd ‘Chuji’, Haruna Moshi ‘Boban’ na Juma Kaseja. Mbaya zaidi hakuwa akisema hata sababu ya msingi.

Badala yake alisisitiza hatawaita, kitu ambacho hakikuwa sahihi hata kidogo, kama mtaalamu alilazimika aeleze mambo yake kitaalamu.

Waoga walihofia kumpa changamoto, lakini Tanzania haina waoga tupu, wako waliomueleza na hadi alipomaliza mkataba anabaki na sifa zake na upungufu wake.

Tanzania ilionekana kuyumba baada ya Jan Poulsen kutoka Denmark kushika nafasi, babu huyo kidogo ukali wake ulimuathiri na timu haikufanya vizuri.

Lakini Jan Poulsen ambaye alimpendekeza kwa ajili ya timu za vijana alikuwa bora zaidi na leo mabadiliko makubwa yanaonekana kiuchezaji lakini vijana amewapa zaidi nafasi kuliko hata Maximo.

Asilimia 75 ya kikosi cha Stars ni vijana, hata wakongwe waliopo wanaendelea kukaa benchi ingawa inapobidi anawapa nafasi na wengi wamekuwa wakionyesha uwezo.

Frank Domayo, Simon Msuva, Salum Abubary ‘Sure Boy’, Shomari Kapombe, Waziri Salum, Raadhani Singano ‘Messi’, Jonas Mkude, Christopher Ewards ni kati ya vijana ambao wamewahi kupata auw anaendelea kupata nafasi kutoka kwa Poulsen.

Mwenendo wa Stars iliyo chini ya Poulsen unaleta majibu mawili. Kwanza uzalendo kwa taifa badala ya kocha binafsi. Pili, inaonyesha hivi bila ya kujali jina au mtu, Stars inaweza kusonga mbele.

Mwisho, hakuna timu inayoweza kwenda bila ya mabadiliko. Kwa kuwa wakati wa Maximo ulifikia kikomo, ilikuwa lazima waje wengine na maisha yaendelee.

Mara nyingi mabadiliko yako hivi, yuko anayeanzisha lakini baada ya hapo safari inaendelea na wengine wanaendelea kuyachangia zaidi kama ambavyo ilivyo sasa. Watanzania tunapaswa kujiamini na kujua nini kinatakiwa kwa maslahi ya nchi yetu.

Maximo alifanya kazi yake, sisemi ni mbaya, lakini leo Poulsen anafanya kazi nzuri zaidi na anapaswa kupewa sapoti zaidi. Tunakumbushana tu.







0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic