April 24, 2013


Waliosimama toka kushoto: Madatta Lubigisa, Rajabu Musoma, Beya Simba, Nteze John ‘Lungu’, Kitwana Selemani ‘Popat’, Fumo Felician, Pascal Mayala na Paul Rwechungura.

Waliokaa toka kushoto: George Gole, Khalfan Ngassa, Ally Bushiri, Alphonse Modest, Mao Mkamy ‘Ball Dancer’, Saleh Muhammad, Hamisi Nyembo na Nico Bambaga
 


 Na Saleh Ally
 MWANZONI mwa miaka ya 1990 Pamba  ya Mwanza ilitua na dege mjini Tanga, baada ya saa chache wachezaji wake walikuwa uwanjani tayari kucheza na Coastal Union yenye wachezaji nyota.
Mechi hiyo ilikuwa ngumu na muhimu zaidi kwa Coastal Union kwa kuwa kama ingefungwa, badi ingeteremka daraja, mashabiki walijitokeza kwa wingi Uwanja wa Mkwakwani.

Pamba wakati huo maarufu kama TP Lindanda hawakuwa watu wa mchezo, waliingia uwanjani wakitaka ushindi bila ya kujali Coastal Union wanataka lipi.

Mwisho wa mechi, Coastal Union 0 na Pamba 1, bao pekee likiwa limefungwa na Edward Hizza. Hasira zikawashinda nguvu mashabiki wa Coastal ambao walianza kuwachapa ngumi na mateke wachezaji na viongozi wa Pamba.


Pamoja na Polisi kuingilia haikuwa kazi rahisi, waliondoka uwanjani hapo ndani ya karandika kama vile wao ni mahabusu hata safari siku hiyo ikaahirishwa, wakalazimika kuondoka siku iliyofuata chini ya ulinzi kwenda Dar es Salaam ambako walitua na kujaza mafuta kabla ya kuanza safari ya kurejea Mwanza.

Pamba ya Mwanza au TP Lindanda, wana Kawekamo haikuwa timu ya mchezo. Uwezo wake ulikuwa juu lakini hata uongozi wake ulikuwa wa kitaalamu zaidi kuliko hata klabu kongwe kama Yanga na Simba zinavyoendeshwa.

Pamba ya miaka ile, imefanya mambo mengi ya kusimuliwa kwa mlengo wa mafanikio wakati Yanga na Simba zaidi ni sifa tu lakini hata mambo ya miaka 1980 yaliyofanywa na Pamba, leo hawawezi kufanya!

Kwenda na ndege mkoa mmoja, timu inatua na kucheza halafu wachezaji wanarudi kwenye ndege na kurejea hakikuwa kitu cha ajabu au kigeni kwa Pamba.

Mara mbili wamefanya hivyo, walitua Songea, wakaifunga Majimaji, halafu wachezaji wakaongozana kwenda ukweni ambako mchezaji mwenzao Rajab Risasi alifunga ndoa baada ya hapo wakamchukua ‘mke wao’ na kupanda naye ndege kurejea Mwanza.

Ndege hiyo ya Mwadui, Shinyanya ilikuwa ikiwabeba Pamba kutokana na mkataba maalum kati ya Bodi ya Pamba na uongozi wa mgodi wa Fred Williamsons & Sons.

Ingawa ilikuwa zamani, Pamba waliendesha mambo yao kisasa, leo utaona Arsenal, Manchester City, mabingwa wa England Manchester United na timu nyingine ndiyo wanafanya hivyo.

Arsenal wana mkataba na Shirika la Ndege la Emirates, Man City mkataba wao na Etihad na Man United wako na Turkish Airlines. Pamoja na kujipatia fedha, mashirika hayo yanahusika na usafiri wa wachezaji.

Kupata mabasi kutoka kwa wadhamini ni jambo zuri, lakini timu kubwa za Ulaya hazitaki kuingia gharama ya kuendesha ndege zinaona ni kama kujichanganya.

Ndiyo maana zinaingia mkataba na mashirika ya ndege ili kupata fedha na kusafirishwa wachezaji wake katika mechi muhimu.

Pamba walikuwa wanatoka Mwanza mchana kwenda mkoa mwingine, saa tisa wanakuwa uwanjani kukipiga bila ya uchovu na wanapiga ‘mtu’ halafu wanarudi kwenye ndege na kurejea Mwanza.

Inawezekana Pamba haikuwa na mkataba na mgodi wa Mwadui kama ilivyo kwa Man United au Arsenal. Lakini makubaliano ya kupunguziana au kukubaliana kutumia ndege hiyo kilikuwa ni kitu kinachofanya kazi.

Yanga na Simba wanapaswa kuwa wabunifu, makampuni ya ndege yako lukuki. Wanaweza kufanya mipango na kuingia nao mikataba kwa kuwashawishi kutokana na utendaji au ubora wa kazi zao.

Wakifanikiwa, maana yake wataingiza fedha lakini lakini wataweza kupata usafiri na kupunguza kusafiri na basi zaidi ya kilomita 1,000 kwenda kucheza mechi.

Ubunifu wa Pamba miaka hiyo unaweza kufanyika kipindi hiki lakini ukiwa umeboreshwa kulingana na kipindi chenyewe na ukawa msaada mkubwa.

Usafiri bora ni sehemu ya motisha kubwa kwa wachezaji, ni sehemu ya huduma bora kwa wachezaji kama ilivyo kwa malazi, chakula na hata malipo mazuri.

Pamba waliliona hilo, ndiyo maana timu yao ilikuwa imara na itabaki kuwa gumzo kwenye historia ya soka ya Tanzania milele.

Ubora huo usingekuja kwa ndoto, maneno mengi, ubinafsi na kulalama kwa kutotaka kukosolewa kunakofanywa na viongozi wa timu hizo kongwe ambazo maendeleo ni pale yanapopatikana tu, hakuna mipango.

Inawezekana bado kuna viongozi wanaamini wachezaji kusafiri na ndege ni anasa, badilikeni. Usafiri wa ndege ni kama unavyosafiri na basi au gari binafsi lakini umuhimu na utofauti wake unajulikana.

SOURCE: CHAMPIONI

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic