April 13, 2013



Yanga wameanza kusukuma tuhuma kwa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), kwamba lina njama za kuwafanyia hujuma ili Azam FC iweze kuwafikia katika msimamo wa Ligi Kuu Bara, ikiwezekana kuwapita na kutwaa ubingwa.

Yanga wanaamini Azam FC ikitangulia kucheza mechi yao dhidi ya African Lyon na kushinda, basi pengo litakuwa ni pointi tatu tu na baada ya hapo ‘watawekeza’ nguvu katika mechi yao inayofuatia na ‘kuwamaliza’ ili wawafikie.


Ukiangalia madai ya Yanga, yanaweza kuwa na hoja ya msingi kwa kujiuliza kwa nini TFF wakurupuke na kubadili ratiba haraka bila ya kuzitaarifu klabu katika muda wa kutosha?

Siku 14 kabla ya mechi unaweza kuwa wakati mwafaka, lakini kwa nini leo waibuke na kusema ratiba imebadilishwa na sababu zao za msingi ni Televisheni ya SuperSport kutaka kuonyesha mechi hizo moja kwa moja?

TFF imetangaza Super Week na mechi zilizofanyiwa mabadiliko ni zile za kuanzia Aprili 11 hadi 18, wakati ile ya watani, Yanga na Simba, Mei 18, inabaki kama ilivyo.

Katika Super Week, mabadiliko yapo kwenye mechi ya Azam dhidi ya African Lyon ambayo imesogezwa mbele siku moja hadi Aprili 11, Yanga dhidi ya Oljoro iliyokuwa ichezwe Aprili 10, sasa imekwenda hadi Aprili 13 (kesho).

Azam na Simba imesogezwa siku moja mbele hadi Aprili 14, Coastal Union na JKT Ruvu itakayochezwa Aprili 16 badala ya Aprili 10. Wakati mechi nyingine zilizosogezwa mbele ni Mgambo Shooting na Yanga ambayo imesogezwa siku nne mbele hadi Aprili 17, sawa na ile ya Mtibwa dhidi ya Oljoro.

Yanga wana hoja za msingi kuhusiana na utaratibu kutofuatwa, ingawa ni vigumu kuamini kila wanachokisema kuhusiana na TFF na Azam kwa kuwa ni kitu kinachohitaji uthibitisho zaidi, suala ambalo ni gumu pia.

Lakini kwa TFF ambayo ilitoa hoja yake kwamba inafanya vile kwa lengo la kuipa SuperSport hamu ya kudhamini Ligi Kuu Bara mwakani, lazima iwe na mipango na kuamini hata kama wao ndiyo wapangaji wa ratiba, lakini timu zina haki pia.

Ndiyo, timu zina haki ya kujua ratiba mapema, vivyo hivyo kama kutakuwa na mabadiliko basi zitaarifiwe mapema kwa kuwa zinakuwa katika maandalizi na zinatumia mamilioni ya fedha.

TFF isidanganye kwamba kwa kuwa wao ndiyo wanaosimamia mpira wa Tanzania, basi wanaweza kufanya wanachotaka bila kuangalia wengine wanaathirika vipi.

Lakini pia siamini kampuni kubwa na yenye uzoefu kama SuperSport wamebadilika kiasi hicho na kufanya mambo kwa mtindo wa zimamoto. Nasema hivyo kwa kuwa nimewahi kupata nafasi ya kufanya nao kazi kwa miezi kadhaa, tena makao makuu pale Johannesburg, Afrika Kusini.

Najua namna mpangilio wa kazi zao unavyokwenda, hivyo siamini kama wamebadilika na kushuka kiasi hicho cha kufikia kufanya mambo kwa kubabaisha na kukurupuka ndani ya wiki moja, eti wanataka kuripoti mechi fulani.

Ninaamini kama TFF ingeomba kitu kwao kwa mtindo huo wa kukurupuka, lazima wangeambiwa kuna ratiba ya mechi imepangwa kwa mwaka mzima. Ndiyo maana nashangazwa nao.

Lakini nawashauri TFF kwamba bado hawapaswi kuvuruga tu mambo wanapoona wanaweza kufanya hivyo kwa kuwa wao ndiyo viongozi. Lazima waangalie maumivu ya timu husika.

Lakini pia waondoe lawama kama hizo kwamba wanahusika kuzisaidia baadhi ya timu kwa kuwa mwendo wao na mambo wanayoyafanya ndiyo vinazaa kinachozungumzwa.

Kusaidia ligi ipate mkataba mzuri kutoka SuperSport ni jambo zuri, lakini kufuata utaratibu ni jambo zuri zaidi ambalo lingesaidia pia kuondoa hisia tata na imani za dharau au ubabe kutoka upande mmoja kwenda mwingine.
HOJA
SOURCE: CHAMPIONI NEWSPAPER

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic