May 20, 2013



  Na Saleh Ally
WAZEE wa zamani wa klabu mbili kongwe za Yanga na Simba walikuwa wakiangalia sana mapenzi kama muongozo wa utumishi katika klabu zao.
Dunia inakwenda inabadilika kutokana na utandawazi, utaona mfumo huo wa wazee hao wa zamani unaenda unapotea, ingawa ukichunguza utagundua hata kama waliongozwa na busara, bado walikuwa watu bora waliofikiri mbali zaidi.


Kwa wachezaji wanaocheza siku hizi, suala la mapenzi halina nafasi kubwa na badala yake kazi au fedha ndiyo imechukua nafasi kubwa.


Kama ni fedha, basi si lazima mchezaji awe na mapenzi makubwa kwa timu anayokwenda kuichezea, badala yake weledi inabidi uchukue nafasi zaidi. Kwamba awe mtu makini na anayefanya mambo yake si kwa kufurahisha watu au kutanguliza siasa.


Biashara kati ya Simba na kiungo nyota, Mrisho Khalfan Ngassa, ilikuwa haina umakini, kila upande ulifanya mambo ikionekana wazi siasa na fedha ndizo ziliongoza ‘mchezo’.

Utaona kama ni mapenzi kama yale mapenzi ya wazee wa zamani wa Yanga na Simba, basi Ngassa asingepata nafasi ya kucheza soka Simba, hili ni kosa la viongozi wa Msimbazi kumchukua.


Lakini kama ni suala la utandawazi, basi Ngassa pia hakuwa mtu makini kwa kuwa alijua wazi anakwenda sehemu ambayo hakuhitaji kucheza na badala yake fedha ndizo zilimvutia lakini mwisho akashindwa kuwa ‘professional’.


Simba ilitanguliza siasa, Ngassa akatanguliza fedha na mwisho muunganiko wao ukawa ni wenye mashaka makubwa kila siku zilivyokuwa zikisonga mbele.


Taarifa zilieleza kuwa, Azam FC waliamua kuachana na Ngassa mara baada ya kuibusu na kuivaa jezi ya Yanga huku bado akiwa mchezaji wao, tena alivaa juu ya jezi ya Azam FC.

Lakini ili kumuumiza moyo, wao wakahakikisha kama wakimtoa kwa mkopo, basi haendi Yanga, timu ambayo ameonyesha analazimisha kurudi kwa kuwa ndiyo ilimuuza Azam FC kwa Sh milioni 98.

Wakafanya mazungumzo na Simba, walijua wazi huko asingehitaji kwenda. Wakafanikiwa kwa kuwa Simba nao walikuwa katika hatua za kujibu mapigo ya kuchukuliwa Kelvin Yondani, hivyo ikawa ni siasa na Ngassa akatua Msimbazi huku ikionyesha wazi alijua anakwenda ‘kupumzika’ kwa muda kabla ya kurudi Yanga, hasa kwa kuwa alikuwa hatakiwi tena Azam FC.

Siasa:
Kulikuwa na kila dalili za Simba kulazimisha kumpata Ngassa kama sehemu ya kuwaonyesha mashabiki wao kazi imefanyika.
Lakini ilionekana Simba walimtaka Ngassa ikiwa ni kama sehemu ya kuziba kosa lao la kufanya uzembe na kumuachia beki Kelvin aondoke na kutua Yanga.
Hivyo, pamoja na kuwa na taarifa kwamba Ngassa alizungumza na Yanga na kufikia makubaliano, Simba waliingilia kati kama sehemu ya mashindano ya kukomoana.

Inawezekana kabisa Simba walijua Ngassa hakuhitaji kwenda Msimbazi, lakini wakataka kuonyesha tu. Hiyo ndiyo siasa badala ya maslahi zaidi.
Kumsajili mchezaji aliyechezea Yanga si kitu kibaya, lakini suala la yuko tayari kwa dhati bado linabaki kuwa muhimu badala ya kumlazimisha aipende sehemu kwa ushawishi wa fedha.

Mazungumzo:
Yanga walisema kwamba wao walianza mazungumzo na Ngassa ajiunge nao baada ya mkataba wa Azam FC. Lakini Simba wakaingilia kati na kuzungumza na Azam FC ili wamchukue, kweli wakafanikiwa.
Utaona hapa ni uleule usajili wa kuonyeshana, lakini si mipango hasa ya kipi wanakihitaji na kukiamini. Kwamba ‘kuipiga bao’ Yanga ndiyo kitu muhimu. Siku zote usajili wa namna hii hauna faida na sasa kinachotokea kinaonekana.

Ushahidi:
Ngassa alionyesha hataki kwenda Simba kwa vitendo, aliibusu jezi ya Jangwani katika mechi ya Kombe la Kagame wakati bado ana mkataba na Azam FC.

Alifanya hivyo mbele ya umati wa watu kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar. Vipi Simba siku chache baadaye inamshawishi na kumchukua, wakati hisia zake alizianika hadharani?

Lazima walifanya hivyo si kwa sababu ya uwezo wake, bali ni kuwakomoa Yanga na baadaye uwezo ungefuatia!

Kutomuamini:
Pamoja na kwamba Simba ndiyo walitumia ushawishi mkubwa kwa Ngassa atue Msimbazi huku wakijua wazi hakuwa na mapenzi nako, wao ndiyo waliishi naye maisha ya ‘magutu’!
Magutu ni hali ya kutoaminiana, muda wote walikuwa na hofu na hata uchezaji wake walikuwa wakiufuatilia kwa karibu kuliko mchezaji 
mwingine.

Mara nyingi kila Ngassa alipokosa bao, wapo viongozi wa Simba waliamini amefanya makusudi na mjadala ukaendelea na siku nyingine kukosa huko kukatumika kama kumbukumbu ya makosa.
Sasa kuna haja gani ya kuishi na mtu unayeamini hakuhitaji, zaidi ni kujiongezea maisha ya hofu tu!

Somo kwa Ngassa:
Ngassa ni mmoja wa wachezaji bora waliowahi kutokea Tanzania, hakika anastahili sifa.
Lakini bado kuna haja ya kujifunza uongozi wa soka na kufanya mambo yaende kitaalamu zaidi. 

Kubusu jezi ya Yanga wakati akiwa na mkataba na Azam FC mbele ya watazamaji lukuki hakikuwa kitendo cha kiungwana. Inawezekana mapenzi na Yanga ni kitu binafsi, lakini kazi hasa suala la kuheshimu mikataba lina misingi yake.

Mtu makini anaweza kuwa bora katika heshima ya mkataba alioingia. Lakini bado inakuwa hatari kwa Ngassa kwa maana ya kusaini Yanga akiendelea kuitumikia Simba.

Inawezekana ikaonekana ni kawaida, lakini Ngassa ni mchezaji mkongwe na makini, hakupaswa kufanya hivyo.

Inawezekana kabisa angeyaendesha mambo yake kitaalamu zaidi kuliko alivyofanya hivyo. Kuna haja ya yeye kuyaangalia hayo kwa kutafakari zaidi kwa kuwa hata Yanga siku moja wanaweza kuwa na hofu naye kwamba huenda akasaini na timu nyingine wakati akiwa nao au huenda akaibusu na kuivaa jezi ya timu nyingine tena kwa kuwa kama mapenzi, yana wigo mpana yanaweza kuwa yale ya dhati tu au hata yanayoendeshwa na fedha.

Kilichotokea kwa Ngassa na Simba kinaweza kuonekana ni kitu cha kawaida, lakini ni zaidi ya darasa kwa timu zote zilizohusika na zilizoshuhudia mchezo huo pamoja na mchezaji mwenyewe.

Vizuri siasa isiwe muongozo wa kufanya mambo katika soka, badala yake mipango na uhitaji sahihi ndiyo vitumike kusukuma mambo.

Fedha walizotumia Simba kumpa Ngassa huenda wangeweza pia kuwatengeneza vijana kama ambavyo wamekuwa wakifanya sasa, wasingekuwa katika presha kama ambayo wanaipata na mwisho inawasumbua kwa kuwa kila msimu inaonekana Yanga wanapata ushindi dhidi yao kwa kumchukua mchezaji wanayemhitaji sana!

SOURCE: CHAMPIONI NEWSPAPER


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic