May 20, 2013



Waitaliano wanatumia neno calico derby, wakimaanisha mechi ya watani wa jadi, mfano katika Serie A zinapokuwa zinakutana AC Milan na Inter Milan, kawaida vituko vinakuwa lukuki.

Hapa nyumbani tunasema mechi ya watani wa jadi, zinapokutana Yanga na Simba, hakuna ubishi ndiyo mechi kubwa zaidi kuliko nyingine zote Afrika Mashariki. 

Utaona maandalizi ya mechi hiyo yanakuwa tofauti na nyingine zote, wachezaji wanapata huduma na ofa za kila namna, ili mradi kila upande unataka kushinda katika mechi hiyo bila ya kujali kama ni katika Ligi Kuu Bara, basi ushindi wake ni pointi tatu na mabao mawili kama ilivyo ushindi dhidi ya Ruvu Shooting au Polisi Moro.


Hakuna anayeweza kuzishusha calico derby zirudi na kulingana na mechi nyingine kwa kuwa zina ujazo wa mambo mengi na historia inaonekana kusomeka zaidi zinapofikia kupambana.

Kitu ninachotaka kukizungumzia ni namna mambo ambavyo yamekuwa yakienda, viongozi wa kila upande katika timu hizo wamekuwa wanabadilika na ikiwezekana kumuona kila mtu ni msaliti kwao.

Hisia za kuona kama wanasalitiwa ndiyo zimekuwa muongozo, hali ambayo inafanya kambi za timu hizo kuwa kama ubalozi wa nchi fulani ambao una hofu ya kulipuliwa na mabomu.

Ulinzi unaongezwa, kutoaminiana kuanzia ndani ya kambi hadi nje kunazidi kuongezeka na kwa kifupi hata gredi ya amani inaporomoka kwa kuwa hata kuangaliana kati ya viongozi na wachezaji kunabadilika.

Wakati fulani wachezaji walikuwa wakipokwa simu, hali hiyo imekuwa ikiendelea hadi sasa. Lakini hisia za kumuona kila mmoja ni kama adui hazijawi kupungua na ndiyo maana utaona kila baada ya mechi hiyo, viongozi lazima watakuwa na wa kumuangushia lawama.

Hisia zisizo sahihi ndizo zimekuwa zikiendesha ‘vichwa’ vya viongozi wa soka, pia wanajisahau na kutaka kila mtu azitumikie klabu hizo kwa wakati huo bila ya kujali kwamba soka ni burudani kwa wengine na si kazi kama ilivyo kwao.

Mfano, juzi nilisikia kuna mmoja wa maofisa wa Simba ambaye aliacha kazi klabuni hapo, siku chache zilizopita alionekana katika ofisi ya kiongozi mmoja wa sasa wa Yanga. Imekuwa ni kosa kubwa na analaumiwa kwamba huenda alifika pale kuchukua fedha kwa ajili ya kuwapelekea fedha wachezaji wa Simba ili ipoteze mchezo.

Ukiwauliza waliokuwa wakitoa tuhuma hizo, hakuna hata mmoja mwenye uhakika na kuchukuliwa kwa fedha hizo hizo na kupelekwa, lakini kwa kuwa tu ameonekana naye, basi inaaminika alikwenda kuchukua fedha.
Iko haja ya kutokuwa na hisia hasi ambazo hazijengi pia ni vziuri kumtuhumu mtu kwa ushahidi badala ya hisia kwa kuwa hakuna maana kama wapenda soka watashiriki mchezo huo halafu wasiwe marafiki. Utani si uadui au ugomvi.

Lakini nguvu nyingi zikielekezwa kwenye maandalizi, huenda kutakuwa na mafanikio mengi kuliko hisia za kuhujumiwa kuonekana kama ndiyo muongozo, mbaya zaidi karibu wote inakuwa kama ‘akili’ zimekosa moto na badala yake wanahisi kuhujumiwa kila wakati na maisha yao yanakuwa ni lawama tu.

Kama Yanga na Simba zitaendeshwa kwa hisia tu, basi hazitafanya vizuri kwa kuwa hali halisi ndiyo inapaswa kuchukua nafasi na kufanya mambo kwa uhakika (si kubahatisha), kutasaidia kubadilisha mambo.

Wakati mwingine huwa ninaamini wachezaji wengi hasa Watanzania wamekuwa hawachezi kwa uwezo wao wote mechi za Simba dhidi ya Yanga kwa kuwa wana hofu ya kuonekana wamehujumu, hivyo hata kama kulikuwa na sehemu mchezaji alitaka kujaribu kupita na anaaminianaweza, basi ataacha kwa hofu akipoteza mpira ataonekana ni mhujumu, hivyo anatoa pasi ilimradi huku akiacha kutumia ubunifu alionao kuisaidia timu!



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic