May 14, 2013




*Akumbushia Yanga walivyomtosa na kutua Simba

*Aamua kurudi shule nchini Sweden
Na Saleh Ally
MWANZONI mwa miaka ya 2000, Simba ilikuwa ina kiungo mchezeshaji aliyekuwa kipenzi kikubwa cha mashabiki na wanachama wa klabu hiyo.
Ukimuona anacheza, huenda utafikiri kuwa hana uwezo mkubwa, lakini alianza kucheza soka la Ulaya tangu enzi hizo, wengine wanafuatisha, leo ndiyo maana utaona wanamsifia mtu kama Salum Abubakary ‘Sure Boy’.

Shekhan Rashid Abdallah alikuwa kiungo namba nane, wakati huo namba sita unamkuta ‘mnyama’ Selemani Matola. Ndiyo maana kiungo cha Simba kilikuwa gumzo.


Shekhan alitokea Yanga, alianza kukipiga katika timu ya vijana, lakini baadaye hakupata nafasi kwa kuwa waliokuwa wakifanya usajili walimdharau, huenda kuna kitu kilimponza.
“Inawezekana walinidharau kutokana na wembamba wangu, nilikuwa mwembamba mno. Wakaona sitaweza kuhimili mikiki, ndiyo maana nikatua Simba,” anasema katika mahojiano maalum kutoka Stockholm, Sweden anakoishi.

Tayari Shekhan ni baba wa watoto wawili, Maryam, mwenye mwaka mmoja na miezi mitatu na Jamal, mwenye wiki mbili sasa na yeye ameamua kuendesha familia yake.

“Naweza kusema nimeacha soka, sichezi tena soka la kiushindani. Nimerudi shule, kwa sasa ni mwanafunzi lakini kila ninapopata muda wa mapumziko ninakuwa naichezea timu ya FC Kilimanjaro ambayo inaundwa na Watanzania hapa Sweden.

“Timu inatukutanisha Watanzania na ina malengo, lakini mimi zaidi nakuwa kama kocha na kusaidiana na wenzangu katika kutafuta maendeleo kwa pamoja kwa kuwa tunaishi kama ndugu,” anasema Shekhan.


Familia:
Kweli sasa mimi ni mtu wa familia na nimetupa nguvu zangu zote huku, ni familia yenye furaha, unaweza kusema happy family.
Watoto wangu kweli ni wadogo na sijajua wanataka nini wakikua na siwezi kuwachagua kuwa wanasoka kama hawatataka, lakini nitahakikisha ninawaunga mkono katika kile watakachokuwa wanataka kufanya kwa ajili ya maendeleo ya maisha yao.



Simba kuyumba:
Niko mbali, lakini naona namna mambo yanavyokwenda Simba, kwangu siwezi kusema ina wachezaji wasiojua mpira, nawaona wachezaji wengi na wenye uwezo mkubwa pale.
Tatizo liko kwa uongozi, vizuri ukajirekebisha na kujenga umoja. Kama uongozi hauna umoja, Simba haiwezi ikafanya vizuri hata kidogo. Lazima kuwe na mabadiliko katika hilo na uongozi ndiyo unaotakiwa kufanya vizuri.


Kujirekebisha:
Simba inaweza kurudi katika hali yake, haijafanya vizuri lakini haijaharibu katika kiwango cha kutisha hadi unaweza kusema mambo ni mambo sana.  Lakini kila kitu lazima kianzie kwa uongozi ambako mambo yaliharibika.
Baada ya hapo, hata wachezaji wanapaswa kuwa na umoja ndiyo mambo yatakwenda vizuri, la sivyo kutakuwa hakuna mabadiliko.


Mechi:
Naikumbuka sana mechi ya mwaka 2002, ilikuwa fainali ya Kombe la Tusker, tuliwafunga Yanga mabao 4-1 na kutwaa ubingwa, nilicheza vizuri sana.
Lakini nakumbuka Yanga ilikuwa timu bora wakati huo, sisi pia. Hivyo ushindani ulikuwa mkubwa sana licha ya kufanikiwa kuwafunga mabao mengi.


Kikosi bora:
Simba imekuwa na vikosi vingi sana bora, lakini wakati wetu kikosi bora kilikuwa hiki; kipa ni Mohammed Mwameja, 2. Said Sued ‘Panucci’, 3.Ramadhani Wasso, 4.Amri Said ‘Stam’, 5.Boniface Pawasa ‘Baba P’, 6.Selemani Matola, 7.Steven Mapunda ‘Garincha’, 8. Shekhan Rashid, 9.Nteze John, 10.Yusuf Macho Lwenda, 11.Mark Sirengo au Joseph Kaniki.
Katika kikosi hicho, kama atatoka Nteze au Macho, nje kulikuwa na super sub, Emmanuel Gabriel, maarufu kama Gabriel, nakuambia hautoki hapo, hata kama atakuja TP Mazembe.


Fedha:
Kungekuwa na fedha wakati huo, tungefika mbali sana kwa kuwa tulikuwa na uwezo mkubwa. Lakini kipindi hiki watu wamepata sana fedha lakini ndiyo hivyo.


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic