August 9, 2013



Na Saleh Ally, Zurich
ZIARA ya Ulaya safari hii inaishia hapa katika jiji hili ambalo ni maarufu sana duniani kuhusiana na mambo mengi kama vile amani, lakini ni pamoja na  viongozi wengi wa Afrika kuficha fedha zao hapa baada ya kuziiba.

Unaweza kusema mafisadi wengi wamekuwa wakificha fedha zao hapa, lakini hiyo haikuwa kazi iliyonileta hapa. Ziara ya Ulaya ilianzia hapa kabla ya kwenda Ujerumani na Ufaransa na juzi nilikutana na mmoja wa rafiki zangu ambaye ni wakala wa kuuza wachezaji anayetambuliwa na Shirikisho la Soka la Kimataifa (Fifa).

Katika mazungumzo yetu kuhusiana na wachezaji, alitolea mfano wa wachezaji wawili waliokuwa wanacheza katika timu moja ya vijana ya Ujerumani, mmoja sasa anacheza katika timu ya daraja la tatu na anapata euro 3,000 (Sh milioni 7), wakati mwenzake anacheza Werder Bremen inayoshiriki Bundesliga ambayo anaingiza euro milioni moja (Sh bilioni 2.2 kwa mwaka.

Kati ya wachezaji hao wawili, anayeingiza kiasi kidogo ndiye alikuwa bora zaidi, lakini sasa mambo yamebadilika. Kama hiyo haitoshi alielezea namna rafiki yake ambaye ni meneja wa Thomas Muller wa Bayern Munich alivyokuwa hategemei kama mchezaji wake atakuwa mmoja wa wachezaji bora.

Kwamba rafiki yake huyo aliamini Muller hakuwa na umbo zuri la kumsaidia kuwa mchezaji bora wa kulipwa nchini Ujerumani, aliamini huenda angeishia madaraja ya chini kwa kuwa alikuwa na juhudi sana na ndiyo ungekuwa msaada wake. Lakini sasa ni bora katika soka la kulipwa.

Nilipokuwa nikiendelea na mazungumzo hayo wakati nikipata kahawa katikati ya moja ya mitaa inayopendeza ya Jiji la Zurich, maneno hayo ya rafiki yangu yalinirudisha kwa Shomari Kapombe.

Kapombe amefanya majaribio katika klabu za madaraja ya nne na timu ya pili ya AS Cannes timu ambayo ilimkuza kiungo nyota duniani, Zinedine Zidane na wengine kadhaa.

Kapombe amefanya vizuri na timu hiyo inaonyesha wazi kwamba kweli inamtaka, achana na kwamba kuna msaka vipaji maarufu kama scout kutoka Zaragoza, lakini hali halisi ni kwamba Wafaransa ndiyo wanaoonyesha zaidi kuvutiwa na Kapombe.

Lakini kumekuwa na mgongano wa njia tatu, moja ni kwamba Kapombe anaonyesha wazi anataka kubaki Ufaransa na kucheza soka, Wafaransa wanasema ‘yes’, wanamhitaji lakini watamhitaji kwa mkopo kwa kuwa Tanzania si nchi maarufu kisoka na hawawezi kuweka fedha zao nyingi bila ya kuwa na uhakika.

Walichoahidi Wafaransa ni kwamba wao watakaa na Kapombe na kumuendeleza, wanaamini kwamba baada ya muda watamuuza na kugawana fedha nusu kwa nusu na Simba.

Simba nao inaonekana wanahitaji fedha, hivyo Kapombe kwenda kwa mkopo huenda inaonekana kama wanamtupa. Ninaweza kuwa na wazo tofauti kwamba huenda ikawa hasara kwa sasa kwa Simba lakini faida kubwa itaonekana hapo baadaye.

Bahati ya kucheza Ulaya bado ni biashara kubwa kwa kuwa kama Kapombe kweli atafanya vizuri na wanamuamini anaweza kufanya hivyo, basi vizuri wakikubali na akaenda.

Kama ni msimu mmoja au miwili akiuzwa, basi watapata faida ambayo huenda itakuwa kubwa na itawafungulia soko zaidi.

Akiuzwa katika klabu kubwa ni rahisi kuwatangaza zaidi, huenda watakosa dola 100,000 au 150,000 kwa sasa, halafu wakapata nyingi zaidi ya hizo baada ya miezi 12 ijayo ambapo bado itakuwa faida kubwa, watakuwa wamejitangaza na kutengeneza mtandao mkubwa wa wacheza kuuza wachezaji ikizingatiwa Simba wana vijana wengi.

Atakapoondoka Kapombe, bado watakuwa na nafasi ya kumpa nafasi kijana mwingine ambaye pia ataingia katika nafasi ya kuuzwa kwa kuwa Simba ina wachezaji wengi wanaoweza pia kuziba pengo la Kapombe kwa wakongwe na makinda.

Inawezekana kwa viongozi wa Simba suala hili lisiwe na faida kubwa kwa kuwa wanaweza kuangalia Kapombe anaweza kuuzwa baada ya msimu mmoja au miwili, hivyo wao wanaweza wasiwe pale halafu  ikawa ni sifa ya mwingine, lakini siku ya mwisho itakuwa ni faida ya Simba na wao watakumbukwa kwa mchango wao.

Kikubwa ambacho wanachotakiwa kufanya Simba ni kuwa makini sana katika mikataba watakayoingia (hasa kama watakubali kumuachia kwa mkopo), ili kweli siku ya mwisho kama atauzwa faida hiyo nusu iende kwao badala ya kujikuta wanaambulia patupu.

Biashara ya kuuza wachezaji ina faida na hasara zake, inawezekana Kapombe akabaki Simba na bado siku ya mwisho asiwape faida yoyote. Hivyo kazi kwenu kutafakari.  Huu ni mtazamo wa Saleh Ally.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic