Na Saleh Ally
Hapa nyumbani, rekodi
zinaonyesha soka ndiyo biashara kubwa kuliko nyingine yoyote ile kama utapiga
hesabu za mapato ya siku moja.
Inawezekana kabisa, kama
kuna biashara inaizidi soka basi itakuwa ni ile ya madini na kama tutajumlisha
suala la upatikanaji wake, soka itaendelea kuwa biashara kubwa na yenye faida
ya juu zaidi, nitatoa mfano.
Miaka michache iliyopita
wakati wa mechi za kwanza za ufunguzi wa Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam,
timu ya taifa, Taifa Stars ilicheza na mapato katika mechi hiyo yakafikia hadi
Sh milioni 600.
Unaweza ukatumia mfumo
wowote, lakini fedha hizo zilitengenezwa katika mchezo wa saa moja na nusu tu
kwa kuwa mashabiki waliofika uwanjani walitaka kushuhudia mchezo kwa saa moja
na nusu pekee.
Hakuna mechi nyingine
ambayo imewahi kuingiza mapato zaidi ya hayo ukilinganisha na ile ya Yanga
dhidi ya Simba ambayo iliingiza Sh milioni 500 na ushee, halafu mapato hayo
yakaendelea kuporomoka kila kukicha.
Mapato ya Uwanja wa Taifa
yamekuwa yakizidi kuporomoka kila siku zinavyosonga mbele, hali inayoonyesha
kuwa wale wanaohusika na usimamizi, sasa wameishajua namna ya ‘kuchukua’
mamilioni yanayopatikana kupitia mechi zinazochezwa.
Hakuna sehemu rahisi
kuiba mamilioni kama katika mchezo wa soka kwa kuwa mfumo wake mbovu ndiyo
unajenga magugu yanayowalinda wezi.
Ukiangalia hapa, utaona
mchezo wa soka unavyokwenda nchini ni kwamba unawafaidisha kwa kiasi kikubwa
wale ambao hawavuji jasho, badala yake wajanja ambao wamekaa pembeni.
Viongozi:
Ndani ya klabu hasa za
Yanga na Simba ambazo zinaingiza mapato makubwa, kuna viongozi ambao wamekuwa
wakishiriki katika masuala ya kuhujumu mapato na mara kadhaa wameingia katika
tuhuma na wakati mwingine ikaonekana kila kitu kipo wazi, lakini ‘kubebana’
kunachukua nafasi na hakuna aliyeshitakiwa.
Utaona mapato
yanahujumiwa, lakini hali halisi ni kwamba wahujumu wanafanya kazi pamoja na
baadhi ya viongozi wa klabu hizo ambao wanakuwa wanawahujumu viongozi wenye nia
nzuri.
Anayekataa inawezekana
atakuwa ni mhusika, lakini viongozi wanaofanya hujuma hiyo wametengeneza
mtandao mkubwa ambao ikitokea kiongozi anataka kuwazuia basi wanamtengenezea
zengwe na siku ya mwisho anaonekana ndiye anaihujumu klabu.
Viongozi hao wameugeuza
mchezo wa soka wa Tanzania kuwa mradi na hakuna ubishi kuwa wanawanyoya
wachezaji na viongozi wakweli ambao wanavuja jasho kuufanya mchezo huo uende
kwa mafanikio.
Hawana tofauti na magaidi
wanaowalipua raia wema kwa faida zao, hawa wanawalipua wanaolipa viingilio
wakijua fedha zao zinatumika kuendeleza mchezo wa soka.
TFF:
Ndani ya Shirikisho la
Soka Tanzania (TFF) kumekuwa na watu ambao si waaminifu, wanahusika na uhujumu
wa mapato na kuna wakati fulani kuna viongozi na maofisa wake waliwahi
kuhusishwa na wizi.
Hiyo haikuwa mara ya
kwanza kwamba ndani ya shirikisho hilo, tena tokea likijulikana kama Chama cha
Soka Tanzania (Fat), kumekuwa na kundi linalofanya kazi za uhujumu wa mapato
kwa ajili ya faida ya wachache na si soka kwa jumla.
Vigumu kuwataja majina
kwa kuwa ‘mchezo’ wenyewe unafanywa kama shughuli za uzinzi, kunakuwa na siri
kubwa. Lakini hakuna ubishi, watu hao wanajulikana na wamekuwa wakiendelea na
kazi zao za wizi wa mapato kwenye kila mechi.
Viongozi hao kuhofia
kuchafuka, wamewatanguliza watu fulani ambao wamekuwa wakifanya kazi hiyo kama
wawakilishi wao. Wengine ni magwiji na wanajulikana kwa kazi hiyo.
Rais wa TFF, Leodeger
Tenga hata kama anamaliza muda wake lazima anajua kuna walakini katika suala la
mapato. Alishughulikie kwa kuwa soka haikui bila ya fedha na kama fedha
inaingia na kubaki mikononi mwa wachache, basi ni tatizo.
Ndiyo maana nasema hilo
analijua na anapaswa kulikemea, akikaa kimya maana yake tuingie hofu kwamba
huenda anaulea huo mtandao!
Adui anayeweza kukumaliza
kirahisi ni yule unayemwamini, uliye karibu naye. Wapenda soka wanawaamini
viongozi wa klabu na TFF, pia askari wanaolinda. Lakini wao wanaimaliza soka
wanavyotaka kwa kuwa wanaaminiwa.
Jeshi la Polisi:
Wako askari polisi ambao
si waaminifu, inawezekana wanashiriki moja kwa moja lakini mara nyingi tu
nimewashuhudia wakihusika na kuingiza watu na wao kuchukua fedha kwa faida yao.
Inawezekana hawa wasiwe
katika mtandao lakini wakawa wanahusika moja kwa moja kwa kuwa wana nafasi ya
kukaa milangoni au sehemu fulani ambazo watu wanaweza wakapita.
Wakati mwingine
wanashirikiana na watu kadhaa wasio waaminifu kutoka katika makampuni ya ulinzi
ambao pia wanahusika na uhujumu wa mapato.
Mtandao wa wizi wa
mapato, wahujumu wa mchezo wa soka ni mkubwa na una nguvu sana. Huenda watu
wengi wanawahofia watu hawa kwa kuwa wana nguvu kifedha na hata kwa kuwa na
majina makubwa.
Pia, inaonekana hivi,
Mtanzania anayesimamia kuzipigania fedha za soka ni sawa na kiherehere kwa kuwa
hazimhusu na zinaonekana hazina mwenyewe na kila mmoja anaweza kuchota.
Lakini hali halisi iko
hivi, lazima wenye nafasi ya kuzungumza tufanye kazi ikiwezekana kuwaanika wezi
na wanyonyaji hao ambao wanauumiza mpira wa Tanzania, ndiyo maana wachezaji
wengi hadi wanastaafu wanakuwa hawana kitu na maisha yao ni magumu wakati
walistahili kuishi maisha mazuri baada ya kustaafu.
Kama fedha zingekuwa
zinapatikana kwa wingi zaidi, klabu zikapata fedha nyingi zaidi. Maana yake
wachezaji wangelipwa vizuri zaidi na huenda hata mazingira ya kazi kama
viwanja, sehemu za kuishi zingeboreshwa zaidi.
Sasa mambo ni tofauti,
hayaendi vizuri kwa kuwa fedha nyingi zinapotelewa kwenye mikono ya wajanja
wachache ambao wakati mwingine Yanga au Simba zikifungwa wanalia kwa kisingizio
wanazipenda, kumbe ni unafiki tu. Wanalilia mapato ambayo wanajua yatapungua,
mapenzi ya kinafiki.
Binafsi hakuna
ninayemhofia kwa kuwa sivunji sheria, najua nawaudhi lakini kilio changu ni
faida ya wachache. Nasisitiza umefika wakati wa kukata mirija ya wanyonyaji
hawa na kuingiza nguvu nyingi katika kuhakikisha mapato ya soka yanakua.
Makundi ya wanyoyaji
yanayoongozwa na baadhi viongozi wa klabu, TFF, askari wasio waaminifu yanaweza
kufikia tamati. Kama fedha nyingi au faida inayopatikana kutokana na viingilio
basi iende kwa wahusika zaidi, wachezaji wasiendelee kustaafu na kufa masikini
na wanaotajirika ni matajiri.
Nawaita matajiri kwa kuwa
wengi wao wana uwezo kifedha, lakini wanaiba fedha nyingi zinazotolewa na wenye
uwezo wa chini zaidi. Wengi wanaokwenda uwanjani ni wale wanaochangisha fedha
zao kidogokidogo ili wapate angalau nafasi ya kuona mechi moja kwa wiki.
Wanapotoa fedha hizo, pamoja
na kupata burudani wanajua wanacholipa kinasaidia maendeleo ya mchezo huo ili
waendelee kuburudika. Sasa matajiri wanazidi kuchota fedha zaidi na kujilimbikizia
huku mchezo wa soka ukizidi ‘kukonda’ kutokana na kukabiliwa na umasikini.







0 COMMENTS:
Post a Comment