October 9, 2013




Na Saleh Ally
Mshambuliaji nyota wa Manchester United, Wayne Rooney, anatambuliwa kuwa mmoja wa wanasoka bora zaidi duniani katika kipindi hiki.

Rooney ambaye alichipukia Everton jijini Liverpool, amekuwa gumzo tangu akiwa na umri wa miaka 16, akiwa na Everton mwaka 2002, alifunga bonge la bao dhidi ya Arsenal, dunia ya wanamichezo ikaanza kumzungumzia.

Baada ya hapo, Manchester United ilishindwa kujizuia, Kocha Alex Ferguson akaushawishi uongozi kutoa kitita kikubwa cha pauni milioni 30 kwa mchezaji kinda kama yeye, akasisitiza kwamba hawatajuta kutoa dau hilo, kweli ndivyo ilivyokuwa.

 Achana na alivyoanza hadi kufikia alipo, lakini moja ya upungufu mkubwa alionao Rooney, hasa uwanjani ni kushindwa kudhibiti hasira zake, mara nyingi zimemzidi nguvu na kufikia kufanya uamuzi ambao alijilaumu.

Amewahi kupata kadi nyekundu mara kadhaa kutokana na utukutu wake, aligombana mara kadhaa na aliyekuwa kocha wake, Alex Ferguson na ikafikia hadi kuamua kuandika barua kwamba anataka kuondoka Manchester United.

Vurugu hizo zilisababisha mashabiki wa Manchester United washindwe kujizuia na kumzomea siku alipokabidhiwa kombe la ubingwa wa Ligi Kuu England na kuliinua juu.

Binadamu wanabadilika, takwimu zinazidi kuonyesha Rooney ni kati ya wachezaji bora duniani lakini hasira zake ambazo ni sawa na shetani kwake, sasa amezishinda.

Sakata la kutoelewana na Ferguson hadi ujio wa David Moyes, bado ameendelea kuwa kimya. Wakati wengi wakiendelea kumjadili na mambo mengi yakizagaa, Rooney baba wa watoto wawili, ameonyesha yuko tofauti.

Hakubishana au kupingana na kocha, mchezaji, shabiki wala vyombo vya habari. Badala yake akaendelea kupiga kazi kama kawaida.
Kazi yake ndiyo imewanyamazisha wengi, amecheza mechi sita akafunga mabao matatu huku akiwa na pasi mbili zilizozaa mabao mawili.
Katika mechi hizo sita za msimu wa 2013, Rooney amepiga mashuti 18 yaliyolenga lango na kuwa mmoja wa wachezaji wachache waliofanya hivyo katika Ligi Kuu England.

Kelele zilipungua, lawama zikaanza kuzimika, shangwe zikaongezeka, pongezi zikachanua na hakuna anayesema vibaya tena kuhusu yeye.
Kayamaliza matatizo kiutu-uzima, ameonyesha kazi ni kiboko ya maneno mengi. Huenda hili ni funzo kwa wengine na wanaweza wakautumia mfumo wake huo wa kumshinda shetani na kutoa majibu kwa kuchapa kazi.


Takwimu za Rooney Premiership…








MECHI       MABAO     PASI       MASHUTI
  6                      3              2            18

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic